Matendo ya Mitume 10:1-48

  • Maono ya Kornelio (1-8)

  • Maono ya Petro kuhusu wanyama waliotakaswa (9-16)

  • Petro amtembelea Kornelio (17-33)

  • Petro awatangazia habari njema watu wa mataifa (34-43)

    • “Mungu hana ubaguzi” (34, 35)

  • Watu wa mataifa wapokea roho takatifu na kubatizwa (44-48)

10  Sasa huko Kaisaria kulikuwa na mwanamume aliyeitwa Kornelio, ofisa wa jeshi* wa kikosi* cha Italia.  Alikuwa mtu aliyemheshimu na kumwogopa Mungu, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake, naye aliwapa watu zawadi nyingi za rehema na aliomba dua sikuzote kwa Mungu.  Karibu saa tisa+ mchana* aliona waziwazi katika maono malaika wa Mungu akija na kumwita: “Kornelio!”  Kornelio akamkazia macho, akiwa na hofu, na kumuuliza: “Kuna nini, Bwana?” Akamwambia: “Mungu amesikia sala zako na kuona zawadi zako za rehema, naye anazikumbuka.+  Basi sasa tuma watu huko Yopa wakamwite Simoni anayeitwa Petro.  Mtu huyo ni mgeni wa Simoni, mtengenezaji wa ngozi, aliye na nyumba kando ya bahari.”  Mara tu yule malaika aliyezungumza naye alipoondoka, akawaita wawili kati ya watumishi wake na mmoja wa wanajeshi wake aliyemwogopa Mungu,  naye akawasimulia mambo yote, kisha akawatuma waende Yopa.  Siku iliyofuata, wakiwa safarini karibu kufika kwenye jiji hilo, Petro alipanda kwenye paa la nyumba karibu saa sita* ili kusali. 10  Lakini akahisi njaa sana na akatamani kula. Walipokuwa wakitayarisha mlo, akapata njozi+ 11  naye akaona mbingu imefunguliwa na kitu fulani* kikishuka kama shuka kubwa la kitani, kikiteremshwa duniani kwa ncha zake nne; 12  na ndani yake mlikuwa na kila aina ya wanyama wenye miguu minne, viumbe wanaotambaa wa dunia, na ndege wa angani. 13  Kisha sauti ikamwambia: “Petro, simama, chinja ule!” 14  Lakini Petro akajibu: “Hapana Bwana, kwa maana sijawahi kula kitu chochote kilicho najisi na kisicho safi.”+ 15  Ile sauti ikamwambia mara ya pili: “Acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.” 16  Jambo hilo likatokea mara ya tatu, na papo hapo kile chombo kikarudishwa mbinguni. 17  Petro akiwa bado anashangaa kuhusu maana ya maono hayo, wakati huohuo wale watu waliotumwa na Kornelio waliulizia nyumba ya Simoni nao walikuwa wamesimama langoni.+ 18  Nao wakaita kwa sauti na kuuliza ikiwa Simoni anayeitwa Petro alikuwa mgeni humo. 19  Petro alipokuwa akiwaza kuhusu yale maono, roho+ ikasema: “Tazama! Wanaume watatu wanakutafuta. 20  Basi simama, ushuke na kwenda pamoja nao, usiwe na shaka kamwe, kwa sababu nimewatuma.” 21  Kisha Petro akashuka kutoka ghorofani akawaambia wale wanaume: “Mimi ndiye mnayenitafuta. Kwa nini mmekuja hapa?” 22  Wakajibu: “Kornelio,+ ofisa wa jeshi, mwanamume mwadilifu anayemwogopa Mungu na mwenye sifa njema katika taifa lote la Wayahudi, alipewa maagizo na Mungu kupitia malaika mtakatifu kwamba awatume watu wakuite uje nyumbani kwake ili wasikie mambo utakayosema.” 23  Basi akawakaribisha na kukaa nao. Siku iliyofuata Petro akaondoka pamoja nao, na baadhi ya akina ndugu wa huko Yopa wakaenda pamoja naye. 24  Kesho yake akafika Kaisaria. Bila shaka, Kornelio alikuwa akiwatarajia naye alikuwa amekusanya watu wake wa ukoo na rafiki zake wa karibu. 25  Petro alipokuwa akiingia, Kornelio akamlaki, akapiga magoti miguuni pake, na kumsujudia.* 26  Lakini Petro akamwinua, akisema: “Simama; mimi pia ni mwanadamu tu.”+ 27  Alipokuwa akizungumza naye akaingia na kuwakuta watu wengi wamekusanyika. 28  Akawaambia: “Mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kushirikiana au kumkaribia mtu wa jamii nyingine,+ lakini Mungu amenionyesha kwamba sipaswi kumwita mtu yeyote najisi au asiye safi.+ 29  Basi nilipoitwa nilikuja bila kupinga. Kwa hiyo ninawauliza: ‘Kwa nini mmeniita?’” 30  Ndipo Kornelio akasema: “Siku nne zilizopita wakati kama huu, nilikuwa nikisali katika nyumba yangu saa tisa;* wakati huohuo mwanamume aliyevaa mavazi yanayong’aa akasimama mbele yangu 31  na kusema: ‘Kornelio, sala yako imesikiwa na kukubaliwa, naye Mungu amezikumbuka zawadi zako za rehema. 32  Kwa hiyo, tuma watu waende Yopa wakamwite Simoni anayeitwa Petro. Mtu huyu ni mgeni katika nyumba ya Simoni, mtengenezaji wa ngozi, kando ya bahari.’+ 33  Mara moja nikawatuma watu kwako, nawe umefanya vizuri kuja hapa. Basi sote tupo mbele za Mungu ili kuyasikia mambo yote ambayo Yehova* amekuamuru useme.” 34  Ndipo Petro akaanza kuzungumza, akasema: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi,+ 35  lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.+ 36  Alituma ujumbe kwa wana wa Israeli akiwatangazia habari njema ya amani+ kupitia Yesu Kristo—huyu ndiye Bwana wa wote.+ 37  Mnajua habari iliyozungumzwa kotekote huko Yudea, kuanzia Galilaya+ baada ya ubatizo aliohubiri Yohana: 38  kumhusu Yesu aliyetoka Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa roho takatifu+ na nguvu, naye akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi,+ kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.+ 39  Nasi ni mashahidi wa mambo yote aliyofanya katika nchi ya Wayahudi na huko Yerusalemu; lakini walimuua kwa kumtundika kwenye mti. 40  Mungu alimfufua siku ya tatu+ na kumfunua,* 41  si kwa watu wote, bali kwa mashahidi waliochaguliwa awali na Mungu, kwetu sisi, tuliokula na kunywa pamoja naye baada ya kufufuliwa kutoka kwa wafu.+ 42  Pia, alituamuru tuwahubirie watu na kutoa ushahidi kamili+ kwamba yeye ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa mwamuzi wa walio hai na wafu.+ 43  Manabii wote walitoa ushahidi+ kumhusu, kwamba kila mtu anayemwamini hupokea msamaha wa dhambi kupitia jina lake.”+ 44  Petro alipokuwa akizungumza kuhusu mambo hayo, roho takatifu ikaja juu ya wote waliokuwa wakisikia lile neno.+ 45  Nao waamini* waliotahiriwa ambao walikuwa wamekuja pamoja na Petro wakashangaa, kwa sababu zawadi ya bure ya roho takatifu ilikuwa ikimiminwa pia juu ya watu wa mataifa. 46  Kwa maana waliwasikia wakizungumza lugha* za kigeni na kumtukuza Mungu.+ Ndipo Petro akauliza: 47  “Je, kuna yeyote anayeweza kuwazuia hawa waliopokea roho takatifu kama tulivyoipokea wasibatizwe+ kwa maji?” 48  Ndipo akawaamuru wabatizwe katika jina la Yesu Kristo.+ Kisha wakamwomba akae pamoja nao siku kadhaa.

Maelezo ya Chini

Ofisa aliyesimamia wanajeshi 100.
Kikosi cha jeshi la Roma chenye wanajeshi 600.
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Tnn., “chombo cha aina fulani.”
Au “kumwinamia.”
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Au “kumfanya aonekane.”
Au “waaminifu.”
Tnn., “ndimi.”