Hamia kwenye habari

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Wanakataa Kutiwa Damu Mishipani?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Wanakataa Kutiwa Damu Mishipani?

Maoni yasiyo ya kweli

Uwongo: Mashahidi wa Yehova hawakubali matibabu au madawa yanayotolewa na madaktari.

 Ukweli: Tunajitahidi kutafuta matibabu bora kwa kadiri inavyowezekana kwa ajili yetu na familia zetu. Tunapokuwa wagonjwa, tunaenda kwa madaktari ambao wanaweza kututibu na kufanya upasuaji bila kutia damu. Tunathamini maendeleo ambayo yamefanywa kuhusiana na mbinu za matibabu. Kwa kweli, matibabu yasiyohusisha damu yamewasaidia si Mashahidi tu, bali pia watu wengine. Sasa katika nchi nyingi, mgonjwa yeyote anaweza kuchagua matibabu yasiyohusisha damu ili kuepuka magonjwa yanayosababishwa na kutiwa damu, au makosa ya kibinadamu.

 Uwongo: Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba imani inatosha kumponya mtu.

 Ukweli: Sisi hatuponyi watu kimuujiza.

 Uwongo: Matibabu yasiyohusisha kutiwa damu mishipani ni ghali sana.

 Ukweli: Matibabu yasiyohusisha kutiwa damu si ghali sana. *

 Uwongo: Mashahidi wengi, kutia ndani watoto, hufa kila mwaka kwa sababu ya kukataa kutiwa damu mishipani.

 Ukweli: Maneno hayo hayana msingi. Madaktari hufanya upasuaji mgumu kama vile upasuaji wa moyo, upasuaji wa mifupa, na upandikizaji wa viungo bila kutumia damu. * Kwa kawaida, wagonjwa wanaokataa kutiwa damu kutia ndani watoto,hupona haraka au sawa tu na wale ambao wanakubali kutiwa damu. * Kwa hiyo, hakuna mtu anayeweza kusema kwa uhakika kwamba mgonjwa atakufa kwa sababu ya kukataa kutiwa damu au ataishi kwa sababu ya kukubali kutiwa damu.

Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanakataa kutiwa damu mishipani?

 Mashahidi hukataa damu kwa sababu ya imani yao ya kidini na si kwa sababu ya matibabu. Katika Agano la Kale na vilevile Agano Jipya tunaamriwa tujiepushe na damu. (Mwanzo 9:4; Mambo ya Walawi 17:10; Kumbukumbu la Torati 12:23; Matendo 15:28, 29) Pia, Mungu huona damu kuwa inawakilisha uhai. (Mambo ya Walawi 17:14) Kwa hiyo, tunaepuka damu si kwa sababu ya kutii pekee, bali pia tunamheshimu Mungu kwa sababu ndiye Mpaji wa uhai.

Kubadili maoni

Upasuaji mgumu unaweza kufanywa bila kutumia damu

 Zamani, madaktari wengi waliona mbinu za kuepuka kutiwa damu kuwa zinazopita kiasi, na hata zinazohatarisha uhai, lakini maoni hayo yamebadilika katika miaka ya karibuni. Kwa mfano, mwaka 2004, makala iliyochapishwa katika gazeti la elimu ya kitiba lilisema kwamba “mbinu nyingi zilizobuniwa ili kuwatibu wagonjwa ambao ni Mashahidi wa Yehova zitakubaliwa na wengi katika miaka ijayo.” * Makala katika kitabu Heart, Lung and Circulation katika mwaka 2010 ilisema “‘upasuaji usiohusisha damu’ haupaswi kufanywa kwa Mashahidi wa Yehova pekee, bali unapaswa kuwa sehemu muhimu ya upasuaji.”

 Sasa maelfu ya madaktari ulimwenguni pote hutumia mbinu zinazopunguza kuvuja kwa damu wakati wa upasuaji. Mbinu hizo zinatumiwa hata katika nchi zinazoendelea na hata wagonjwa wengi ambao si Mashahidi wa Yehova huzitumia.

^ Ona kitabu Transfusion and Apheresis Science, Buku la 33, Na. 3, uku. 349.

^ Ona vitabu The Journal of Thoracic and Cardiovascular Surgery, Buku la 134, Na. 2, uku. 287-288; Texas Heart Institute Journal, Buku la 38, Na. 5, uku. 563; Basics of Blood Management, uku. 2; na Continuing Education in Anaesthesia, Critical Care & Pain, Buku la 4, Na. 2, uku. 39.

^ Ona vitabu The Journal of Thoracic and Cardiovascular Surgery, Buku la 89, Na. 6, uku. 918; na Heart, Lung and Circulation, Buku la 19, uku. 658.

^ Continuing Education in Anaesthesia, Critical Care & Pain, Buku la 4, Na. 2, uku. 39.