Ona video zinazopatikana

Biblia Imebadilishwa ao Kugeuzwa?

Biblia Imebadilishwa ao Kugeuzwa?

 Hapana. Wakati tunalinganisha maandishi ya zamani tunaona kwamba Biblia haikubadilika hata kidogo hata kama imefanyiwa kopi kwa maelfu ya miaka kwenye vyombo vyenye kuharibika.

Je, hilo linamaanisha kuwa makosa hayakufanywa hata kidogo wakati walikuwa wanafanya kopi za Biblia?

 Maelfu ya maandishi ya Biblia yamepatikana. Maandishi fulani kati ya maandishi hayo yako na tofauti mbalimbali, na hilo linaonyesha kuwa makosa yalifanywa wakati wa kufanya kopi. Mengi kati ya makosa hayo hayako makubwa na hayabadilishe maana ya maandishi. Hata hivyo, makosa fulani ya maana yamepatikana, na inaonekana kuwa makosa fulani kati ya hayo yalifanywa kwa kupenda miaka mingi yenye imepita ili kujaribu kubadilisha ujumbe wa Biblia. Tuone mifano mbili:

  1.   Kwenye 1 Yohana 5:7, tafsiri fulani za Biblia za zamani ziko na maneno haya: “mbinguni, Baba, Neno, na Roho Mtakatifu: na watatu hawa ni moja.” Lakini, maandishi yenye kutumainika yanaonyesha wazi kwamba maneno hayo hayakuwa katika maandishi ya kwanza. Yaliongezwa kisha. * Kwa hiyo, tafsiri za sasa za Biblia zenye kutumainika zimeondoa maneno hayo.

  2.   Jina la pekee la Mungu linapatikana maelfu ya mara katika maandishi ya zamani ya Biblia. Lakini, tafsiri nyingi zimeliondoa na kuweka majina ya cheo kama vile “Bwana” ao “Mungu” nafasi penye palipaswa kuwa jina hilo.

Namna gani tunaweza kuwa hakika kwamba makosa mengi zaidi hayatapatikana?

 Kufikia wakati huu, maandishi mengi sana yamevumbuliwa na hilo limefanya ikuwe mwepesi zaidi kuliko wakati mwengine wowote kutambua makosa. * Kulinganishwa kwa kopi hizo kumeonyesha namna gani leo kwamba ujumbe wa Biblia hauna makosa?

  •   Wakati alizungumuzia Maandishi ya Kiebrania (yenye kuitwa na watu wengi “Agano la Kale”), William Green, mutu wenye elimu alisema hivi: ‘Tunaweza kuhakikisha kwamba hakuna kitabu kingine cha zamani kimeandikwa hivyo bila makosa kutoka katika maandishi ya zamani.’

  •   Kuhusu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ao “Agano Jipya,” Bruce, mutu mwenye elimu ya Biblia alisema hivi: ‘Kila mara ushuhuda wa maandishi yetu ya Agano Jipya unakuwa mwingi zaidi kuliko ushuhuda wa maandishi ya waandikaji wengi wa zamani, na hakuna mutu mwenye anaweza kujaribu kupinga maandishi hayo.’

  •   Frederic Kenyon, mutu mwenye kuheshimiwa kwa sababu ya elimu yake juu ya maandishi ya Biblia alisema kwamba mutu ‘anaweza kuchukua Biblia nzima katika mikono yake na kusema bila kuogopa ao kusitasita kwamba anashika Neno la Mungu la kweli, lenye lilipitishwa bila upotezo mukubwa kutoka kizazi mupaka kizazi wakati wa karne nyingi.’

Ni sababu gani zingine zenye kuhakikisha kwamba ujumbe wa Biblia umefikia watu bila makosa?

  •   Wayahudi na Wakristo wenye walifanya kopi ya maandishi walilinda habari zenye kufunua wazi makosa makubwa yenye watu wa Mungu walifanya. * (Hesabu 20:12; 2 Samweli 11:2-4; Wagalatia 2:11-14) Walilinda pia maandiko ya Biblia yenye kulaumu kukosa kutii kwa taifa la Wayahudi na yenye kufunua wazi mafundisho ya uongo ya wanadamu. (Hosea 4:2; Malaki 2:8, 9; Mathayo 23:8, 9; 1 Yohana 5:21) Kwa kufanya kopi za habari hizo sawasawa, watu wenye walifanya kopi hizo walionyesha kuwa ni wenye kutumainika na waliheshimia sana Neno takatifu la Mungu.

  •   Kwa kuwa Mungu aliongoza waandikaji wa Biblia kupitia roho yake, haipatane na akili kusema kama angeilinda pia ili isikuwe na makosa? * (Isaya 40:8; 1 Petro 1:​24, 25) Zaidi ya hilo, haiko tu watu wa zamani ndio alipenda wafaidike nayo, lakini alipenda sisi pia tufaidike nayo leo. (1 Wakorintho 10:11) Kwa kweli, ‘mambo yote yenye yaliandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tukuwe na tumaini.’​—Waroma 15:4.

  •   Yesu na wanafunzi wake walitaja maandiko yenye yalikuwa katika kopi za Maandiko ya Kiebrania bila kuwa na mashaka ikiwa maandishi hayo ya zamani yalikuwa ya kweli ao hapana.​—Luka 4:​16-​21; Matendo 17:​1-3.

^ Maneno hayo hayapatikane katika Codex Sinaiticus, Codex Alexandrinus, katika Maandishi ya Vatican ya 1209, katika Vulgate ya kwanza ya Kilatini, katika tafsiri ya Kisiria ya Philoxenia-Harclea, ao katika Peshitta ya Kisiria.

^ Kwa mufano, zaidi ya kopi 5 000 za maandishi ya Kigiriki, yenye kuitwa Agano Jipya, ao Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yamepatikana.

^ Biblia haionyeshe kwamba wanadamu wenye Mungu alitumia kama wajumbe wake hawangefanya makosa. Inaonyesha waziwazi hivi: ‘Hakuna mwanadamu asiyetenda zambi.’​—1 Wafalme 8:​46.

^ Biblia inasema kwamba hata kama Mungu hakuandikisha maandishi yote ya Biblia neno kwa neno, aliongoza mawazo ya wanadamu wenye waliiandika.​—2 Timotheo 3:​16, 17; 2 Petro 1:​21.