Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kuacha Kugombana

Jinsi ya Kuacha Kugombana

TATIZO

Je, wewe na mwenzi wako mnashindwa kuzungumzia mambo kwa utulivu? Je, kila mara una wasiwasi kwa sababu hujui ikiwa jambo lolote utakalosema au kufanya litamkasirisha mwenzi wako na hivyo kusababisha ugomvi mkubwa?

Kama hali iko hivyo, uwe na uhakika kwamba hali hiyo inaweza kuboreshwa. Lakini kwanza unahitaji kujua sababu inayofanya wewe na mwenzi wako mgombane mara nyingi.

KWA NINI HILI HUTUKIA

Kutoelewana.

Mwanamke mmoja anayeitwa Jillian * akiri hivi: “Nyakati nyingine mimi humwambia mume wangu jambo fulani lakini nashindwa kulisema kama nilivyokusudia. Au ninakuwa na uhakika kwamba nilimwambia jambo fulani, kumbe niliota eti nilimwambia. Hilo limewahi kutokea!”

Kuwa na maoni tofauti.

Hata iwe wewe na mwenzi wako mnapatana kadiri gani, maoni yenu kuhusu mambo fulani yatatofautiana. Kwa nini? Kwa sababu hakuna watu wawili wanaofanana kabisa—jambo hilo linaweza kufanya ndoa iwe yenye kupendeza au iwe na matatizo. Kwa wenzi wengi, jambo hilo linaleta matatizo katika ndoa.

Kuiga mfano mbaya wa wazazi.

Mwanamke anayeitwa Rachel anasema: “Wazazi wangu waligombana mara nyingi na walitupiana maneno yasiyo na heshima. Kwa hiyo nilipoolewa nilizungumza na mume wangu kwa njia ileile ambayo mama yangu alizungumza na baba yangu. Sikuwa nimejifunza jinsi ya kuonyesha heshima.”

Kiini cha tatizo.

Mara nyingi, kiini cha ugomvi mkali si tukio lililouchochea. Kwa mfano, ugomvi unaoanza na maneno “Sikuzote wewe huchelewa!” huenda usimaanishe eti mtu anahitaji kufuata wakati, bali huenda mwenzi mmoja akahisi kwamba mwenzake hamjali.

Hata sababu iwe nini, ugomvi wa mara kwa mara unaweza kuathiri vibaya afya yenu na hata unaweza kuongoza kwenye talaka hatimaye. Basi, mnawezaje kuzuia ugomvi?

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Njia nzuri ya kuzuia magombano ni kutambua visababishi visivyoonekana wazi vinavyouchochea. Wakati ambapo mambo yametulia, wewe na mwenzi wako jaribuni zoezi lifuatalo.

1. Kila mmoja wenu aandike kwenye karatasi jambo lililofanya mgombane hivi karibuni. Kwa mfano, mume anaweza kuandika hivi, “Ulishinda siku nzima na rafiki zako na hukunipigia simu kuniambia ulikuwa wapi.” Mke anaweza kuandika hivi, “Ulikasirika kwa sababu nilishinda na rafiki zangu.”

2. Mkiwa na mtazamo unaofaa, zungumzieni mambo yafuatayo: Je, jambo hilo lilikuwa zito sana? Je, jambo hilo lingeweza kuachiliwa? Katika visa fulani, ili kudumisha amani, inaweza kuwa bora kukubali kwamba mna maoni tofauti na kufunika mambo kwa upendo.​—Kanuni ya Biblia: Methali 17:9.

Ikiwa wewe na mwenzi wako mnaona kwamba jambo hilo lilikuwa dogo, kila mmoja aombe msamaha, kisha mwache kulizungumzia au hata kulifikiria.​—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 3:13, 14.

Ikiwa jambo hilo linaonekana kuwa zito sana kwa mmoja wenu au ninyi wote wawili, chukueni hatua inayofuata.

3. Andika jinsi ulivyohisi wakati mlipogombana, na mwenzi wako pia afanye vivyo hivyo. Kwa mfano, mume anaweza kuandika hivi, “Nilihisi kwamba unapendelea kuwa na rafiki zako kuliko kuwa nami.” Mke anaweza kuandika hivi, “Nilihisi kwamba unanitendea kama mtoto ambaye anapaswa kumwarifu baba yake kila wakati mahali alipo.”

4. Mbadilishane karatasi zenu, na kila mmoja asome maelezo ya mwenzake. Mlipokuwa mkigombana, ni nini hasa kilichokuwa kikimhangaisha mwenzi wako? Zungumzeni jinsi kila mmoja wenu angeshughulika na tatizo hilo bila ugomvi.​—Kanuni ya Biblia: Methali 29:11.

5. Zungumzieni mambo ambayo mmejifunza kupitia zoezi hili. Mnaweza kutumiaje yale mliyojifunza kusuluhisha au kuzuia ugomvi usitokee wakati ujao?

^ Majina yamebadilishwa.