Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAONI YA BIBLIA

Maskini

Maskini

Je, Mungu anawajali maskini?

“Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa . . . Kwa maana [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’”Waebrania 13:5.

JINSI MUNGU ANAVYOONYESHA KWAMBA ANAJALI

Mwabudu wa Yehova Mungu anapopatwa na shida, Mungu hutumia njia mbalimbali kuonyesha kwamba anamjali. Njia moja ni utegemezo wenye upendo wa Wakristo wenzake. * Andiko la Yakobo 1:27 linasema hivi: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao.

Wakristo wa karne ya kwanza walisaidiana. Kwa mfano, ilipotabiriwa kwamba kungekuwa na njaa kali katika nchi ya Yudea, Wakristo katika jiji la Antiokia huko Siria waliamua “kupeleka misaada kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea.” (Matendo 11:28-30) Kwa kufanya hivyo, Wakristo wenzao wenye uhitaji walipata mahitaji muhimu. Msaada huo uliotolewa kwa hiari ulionyesha upendo wa Kikristo kwa matendo.​—1 Yohana 3:18.

Maskini wanaweza kufanya nini ili kuboresha hali yao?

“Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”​—Isaya 48:17, 18.

MUNGU HUTUSAIDIA KUBORESHA HALI YETU

Mamilioni ya watu wamegundua kwamba hekima ya Biblia ina faida sikuzote na inatoa mwongozo bora. Methali 2:6, 7 inasema: “Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi. Naye atawawekea wanyoofu hazina ya hekima inayotumika.” Watu wanapotafuta na kutumia hekima hiyo, wao hufaidika.

Kwa mfano, wanaepuka mazoea yenye kudhuru na yanayogharimu pesa nyingi kama vile kutumia dawa za kulevya na kunywa kupita kiasi. (2 Wakorintho 7:1) Pia wao huwa wanyoofu na wafanyakazi wenye bidii na hivyo kuongeza uwezekano wa kupata kazi au kuwa wafanyakazi wanaothaminiwa. Waefeso 4:28 inasema hivi: “Mwizi asiibe tena, bali afanye kazi ya bidii, . . . ili awe na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.”

Je, kuna mifano yoyote inayoonyesha kwamba hekima ya Biblia huwasaidia maskini?

“Hekima ya Mungu inathibitishwa kuwa njema kutokana na matendo yake.”​—Mathayo 11:19, Biblia Habari Njema.

MIFANO INAYOTHIBITISHA HEKIMA YA BIBLIA INA FAIDA

Wilson anayeishi Ghana, alikuwa akifanya kazi ya kibarua. Siku yake ya mwisho kazini, alipokuwa akisafisha gari la mkurugenzi mkuu, Wilson alipata pesa fulani ndani ya buti la gari. Msimamizi wake alimwambia achukue pesa hizo. Lakini Wilson, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alikataa kuiba pesa hizo. Badala yake, alimrudishia meneja pesa hizo. Badala ya kufutwa kazi, Wilson aliajiriwa na baadaye akapandishwa cheo na kuwa ofisa mkuu.

Barani Ulaya, Géraldine alifutwa kazi kwa sababu mwajiri wake hakuwapenda Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, mama ya mwajiri huyo alimwambia binti yake kwamba alikuwa amefanya kosa kubwa. Alimwambia hivi: “Hutapata mfanyakazi mnyoofu na mwenye bidii isipokuwa awe Shahidi wa Yehova.” Binti yake alifanya uchunguzi kuwahusu Mashahidi, na akamwajiri tena Géraldine.

Sarah, mama asiye na mwenzi, anayeishi Afrika Kusini alijionea mwenyewe jinsi Biblia inavyowachochea watu wapendane. Alipopatwa na shida, washiriki wa kutaniko lake walimpa yeye na familia yake chakula na kumsaidia na usafiri. Baadaye watoto wake walisema, “Tuna wazazi wengi katika kutaniko.”

Kuna mifano mingine mingi inayothibitisha kwamba hekima ya Biblia huwasaidia maskini. Inatukumbusha maneno haya ya Methali 1:33: “Kwa habari yake mtu anayenisikiliza [mimi Yehova], yeye atakaa salama.” Hilo ni kweli kabisa!

^ Katika nchi fulani, serikali huwapa maskini msaada wa kifedha. Katika nchi ambapo hakuna uandalizi huo, watu wa ukoo wanapaswa kuchukua daraka la kuwatunza watu wa familia wenye uhitaji.​—1 Timotheo 5:3, 4, 16.