Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAMBO TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA HISTORIA | TANGAZO

Je, Tangazo Hili Lilikubaliwa na Mungu?

Je, Tangazo Hili Lilikubaliwa na Mungu?

“Ikiwa hamufanye hivyo, . . . kwa musaada wa Mungu, nitakuja kwenu kwa nguvu, na nitawapiganisha kila mahali na kadiri ninavyoweza, nitawatia chini ya mamlaka ya Papa na Mufalme wa Espanye; na nitachukua bibi zenu na watoto wenu na kuwafanya kuwa watumwa, . . . na nitachukua mali zenu na kuwaumiza kadiri nitakavyoweza. . . . Vifo na mateso yote mutakayopata yatakuwa juu ya vichwa vyenu, wala si juu ya Mufalme wa Espanye ao juu yetu.”

HILO ni moja kati ya matangazo ya kipumbavu sana ambayo serikali imewahi kutoa. Maneno hayo ni sehemu ya tangazo linalojulikana kwa jina la el Requerimiento katika Kihispania, ambalo wavamizi ao washambuliaji wa Espanye walipaswa kusoma kwa sauti kubwa kati ya mwaka wa 1501 na 1600, walipofika katika Amerika wakiwa na kusudi la kushambulia.

Wakoloni hao wa Espanye walikuwa kwa kweli wakiwatangazia wakaaji wa inchi za Amerika nini, na kwa sababu gani?

Wakaaji wa Inchi za Amerika Walilazimishwa Kuwa Wakatoliki

Kisha tu Colomb kufika Amerika katika mwaka wa 1492, inchi ya Espanye na Portugal, kila moja ilidai kwamba ina haki ya kutawala maeneo hayo mapya. Kwa sababu mataifa yote hayo mawili yalimuona papa kuwa mwakilishi wa Kristo hapa duniani, yalipokuwa na ugomvi kati yao yalikuwa yakiita papa ili ayasaidie yasikilizane. Chini ya uongozi wa papa, kanisa liligawia Espanye na Portugal maeneo hayo mapya, lakini mbele ya kufanya hivyo inchi hizo mbili ziliombwa kutuma wamisionere ili waende kuwalazimisha wakaaji wa inchi za Amerika wawe wakatoliki.

Mashambulizi yalipokuwa yakiendelea, utawala wa Espanye ulitafuta njia za kutetea kisheria vitendo vya wakoloni hao. Utawala wa Espanye ulisema kama kwa kuwa papa aliongozwa na Mungu alipowapatia maeneo hayo, wakoloni walikuwa huru kuwatendea wakaaji wa inchi namna wanavyotaka, kuwanyanganya mali yao na kuzuia uhuru wao.

Utawala wa Espanye uliandika tangazo fulani ili kuwajulisha wakaaji wa inchi za Amerika uamuzi wa papa. Wakaaji wa inchi walilazimishwa kukubali Ukristo na kutawaliwa na mufalme wa Espanye. Wakuu wa Espanye walifikiri kwamba walikuwa na haki ya kupigana na wakaaji na haki ya kumutendea vibaya mukaaji yeyote wa inchi ambaye angekataa, na walifikiri pia kwamba Mungu aliwaunga mukono.

“Jeuri iliruhusiwa kwa sababu fulani, basi watu walitenda kama wenye kurukwa na akili. Kwa hiyo, wakubwa wa Espanye walitunga visababu ili kuonyesha kwamba vitendo hivyo vilikuwa vya haki.”​—Francis Sullivan, profesa wa teolojia ambaye alikuwa Muyeswiti

“Tangazo Lenye Kuleta Haya, Lenye Kukufuru, na Lisilo la Haki”

Tangazo hilo lilisomwa ili kutuliza zamiri ya watawala wa Espanye na kutetea mashambulizi hayo ya kikoloni. Mara kwa mara, wakoloni hao wa Espanye walisoma tangazo hilo wakiwa katika mashua mbele waanze mashambulizi na pia wakiwa kwenye inchi kavu, walilisomea watu ambao hawakuelewa luga za Ulaya. Wakati mwengine, walisoma tangazo hilo katika vijiji vyenye nyumba za misonge, vilivyobaki ukiwa kwa kuwa wakaaji wa inchi walikuwa wemekwisha kukimbia kwa sababu ya woga.

Damu ilimwangika sana kwa sababu ya kuwalazimisha watu wawe wakatoliki. Kwa mufano, katika mwaka wa 1550 huko Chili, Waaraukania 2 000 walichinjwa katika mapigano. Kuhusu Waaraukania ambao hawakufa, mukoloni Pedro de Valdivia alimuambia mufalme hivi: “Nilitoa ruhusa ya kukata mikono na pua za watu 200 waliokamatwa katika mapigano. Niliwatendea hivyo kwa sababu walikataa kutii amri ambazo niliwatumia mara nyingi.” *

Labda kusoma tangazo hilo kulituliza zamiri za wakoloni hao. Hata hivyo, lilishindwa kuleta maendeleo yoyote katika dini ya Espanye. Bartolomé de las Casas, misionere aliyekuwa mutawa, ambaye aliishi kati ya mwaka wa 1501 na 1600 alijionea matokeo mabaya ya Tangazo hilo, aliandika hivi: “Tangazo hilo lilikuwa lenye kuleta haya, lenye kukufuru, na lisilo la haki, la kipumbavu na la ovyo sana! Tangazo hilo lilichafua sana kanisa la Kikristo.” Muandikaji wa habari Gonzalo Fernández de Oviedo alisema kwa uchungu kwamba mauaji hayo ya wakaaji wa asili wa Amerika yaliwafanya waone Ukristo kuwa dini ya bure sana.

Je, ni Mungu ndiye anapaswa kulaumiwa kwa sababu ya mauaji hayo ambayo wakubwa wa siasa na wa dini walidai kwamba waliyafanya kwa jina la Mungu? Biblia inasema hivi: ‘Hasha, Mungu wa kweli hatende kwa uovu, na Mweza-Yote kutenda isivyo haki!’​—Ayubu 34:10.

^ Kulingana na vyanzo fulani vya habari, tangazo el Requerimiento liliondolewa katika mwaka wa 1573.