Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA

Sababu Gani Tunanunua Vitu?

Sababu Gani Tunanunua Vitu?

Katika uchunguzi uliofanywa duniani pote mwaka wa 2012, nusu ya watu walioulizwa walikubali kwamba wananunua vitu ambavyo hawahitaji kabisa. Watu wawili kati ya watatu wanafikiri kwamba watu wananunua vitu vingi sana. Labda wana haki ya kufikiri hivyo. Watu wengi wamejiingiza katika madeni mengi ambayo wanashindwa kulipa. Wachunguzi wanasema kwamba kununua vitu vingi kunaweza kumufanya mutu awe na mikazo mingi na kukosa furaha! Basi, sababu gani tunanunua vitu vingi hivyo?

WATU wanaofanya matangazo ya biashara wanaendelea kutushawishi sisi ambao ni wanunuaji ili kununua vitu vingi zaidi. Watu hao wanaofanya matangazo ya biashara wana kusudi gani? Kusudi lao ni kuchochea watu wafikie kununua vitu ambavyo hawahitaji kabisa. Watu hao ambao wanafanya matangazo wanajua kwamba watu wanaweza kufikia kununua vitu ikiwa wanashawishiwa. Kwa hiyo, matangazo ya biashara na namna watu wanavyoitikia kununua vitu kwa uwingi, yote hayo yanakusudiwa kuchochea sana watu wanunue.

Kitabu kimoja (Why People Buy Things They Don’t Need) kinasema hivi: “Kwa kawaida, wakati mutu anapanga kununua kitu fulani, anawazia​-wazia namna atakavyokitafuta, namna atakavyokipata, na mwishowe kukinunua ili kiwe chake.” Wachunguzi fulani wa mambo ya biashara wanawaza kwamba wanunuaji wanaweza kuchangamuka sana wanaponunua vitu na hilo linaweza kuwafanya wasisimuke sana. Bwana Jim Pooler, muchunguzi wa mambo ya biashara alieleza hivi: “Ikiwa muuzishaji anatambua jambo hilo, anaweza kutumia nafasi hiyo ili kumushawishi mutu anunue vitu bila kufikiri.”

Unaweza kufanya nini ili usidanganywe na ujanja wa wale wanaofanya matangazo ya biashara? Acha kusisimuka, lakini uchunguze ikiwa ahadi zilizo katika matangazo ya biashara zinapatana na ukweli wa mambo.

AHADI: “Ukinunua Kitu Hiki, Maisha Yako Yatakuwa Mazuri”

Kwa kawaida, kila mutu anataka kuwa na maisha mazuri. Wale wanaofanya matangazo ya biashara wanatuahidi kwamba tamaa zetu zote zinaweza kutoshelezwa kwa kununua vitu vinavyofaa; kwa mufano, wanasema kwamba tunaweza kuwa na afya nzuri, kuwa salama, kuwa na uhusiano muzuri pamoja na wengine, na kuepuka mikazo.

UKWELI WA MAMBO:

Kadiri tunakuwa na vitu vingi zaidi, ndivyo hali ya maisha yetu inavyobadilika. Itatuomba wakati na feza za zaidi ili kushugulikia vitu vingi zaidi. Mikazo inaongezeka kwa sababu ya kuwa na madeni, na tunakosa wakati wa kuwa pamoja na familia na marafiki.

Kanuni: ‘Hata wakati mutu ana vitu vingi uzima wake hautokane na vitu alivyo navyo.’​—Luka 12:15.

AHADI: “Ukinunua Kitu Hiki, Utakuwa Mutu wa Hali ya juu na Mwenye Sifa”

Watu wengi hawakubali kwamba wananunua vitu ili kujionyesha. Lakini, bwana Jim Pooler anasema hivi: “Kwa kawaida, wakati watu wananunua vitu wanachochewa hasa na roho ya kushindana na marafiki, majirani, wafanya​-kazi wenzao na watu wa jamaa.” Ndiyo sababu, mara nyingi matangazo ya biashara yanaonyesha vitu vinavyopendwa na matajiri ao watu wenye kujulikana sana. Matangazo hayo yanatolea wanunuaji wazo hili: “Wewe pia unaweza kuwa hivyo!”

UKWELI WA MAMBO:

Kujilinganisha na wengine kunamufanya mutu asitosheke. Mutu anapofikia kutimiza tamaa fulani, tamaa nyingine inajitokeza.

Kanuni: ‘Anayependa feza hatatosheka na feza.’​—Mhubiri 5:10.

AHADI: “Ukinunua Kitu Hiki, Utaonyesha Wengine Wewe Ni Nani”

Kitabu kimoja (Shiny Objects) kinaeleza hivi: “Kwa kawaida mutu anawaonyesha wengine yeye ni nani (ao angetaka kuwa nani) kwa kutumia vitu alivyo navyo na kuvionyesha.” Wale wanaofanya matangazo ya biashara wanajua hilo na wanabandika alama fulani kwenye vitu, zaidi sana vitu vya bei kali, ili kuonyesha kwamba vitu hivyo ni kwa ajili ya watu wa maisha ya hali ya juu na wa maana sana.

Wewe unajiona namna gani na unataka watu wakuone namna gani? Je, unapenda kuonekana kuwa mutu anayefuatilia mitindo? Kama mwana-muchezo? Iwe unataka kuwa mutu wa hali fulani, watu wanaofanya matangazo ya biashara wanakuahidi kwamba unaweza kuwa mutu wa hali fulani kwa kununua tu kitu fulani.

UKWELI WA MAMBO:

Hakuna kitu ambacho mutu anaweza kununua kinachoweza kumubadilisha ao kumufanya awe na sifa zenye kuvutia kama vile sifa ya kutumainika na ya uaminifu.

Kanuni: ‘Kujipamba kwenu kusiwe . . . kujivika mapambo ya zahabu ao kuvaa mavazi ya inje, bali kuwe yule mutu wa siri wa moyoni.’​—1 Petro 3:3, 4.