Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MUSAADA KWA FAMILIA | KULEA WATOTO

Wakati Kijana Wako Mwanamuke Ana Mahangaiko

Wakati Kijana Wako Mwanamuke Ana Mahangaiko

TATIZO

Kijana wako mwanamuke anasema kwamba ana mahangaiko. Unajiuliza kwa kushangaa, ‘Miaka 13 tu alisha kuwa na mahangaiko? Angali mudogo sana kujua mahangaiko ni nini!’ Lakini, mbele ya kumuambia kijana wako mwanamuke mambo hayo, fikiria sababu fulani ambazo zinaweza kufanya maisha yaonekane kuwa yenye kusumbua kwa kijana mwanamuke ambaye angali mudogo hivyo.

SABABU GANI JAMBO HILO LINATOKEA?

Mabadiliko ya mwili. Kijana mwanamuke anapoingia katika kipindi cha mwili wake kuanza kukomaa, hilo linaweza kumuletea mahangaiko, zaidi sana ikiwa anaingia katika kipindi hicho mbele ao nyuma ya vijana wenzake. Anna, * aliye na miaka 20 sasa, anasema hivi: “Nilikuwa wa kwanza kati ya vijana wenzangu wanawake kuvaa kifunga​-maziwa, na hilo lilinifanya nikose amani. Nilipojilinganisha na marafiki wangu, nilijisikia kuwa mutu wa ajabu-ajabu, asiyefanana na wengine!”

Mabadiliko ya moyoni. Karen, aliye sasa na miaka 17, anakumbuka hivi: “Nilivurugika sana kwa kuwa sikujua sababu gani nilikuwa mwenye furaha wakati wa muchana, lakini usiku nilikuwa ninalia sana. Sikujua nilikuwa na shida gani. Ni kama vile sikuweza kuzuia mawazo yangu ya moyoni.”

Mwanzo wa kuona kipindi cha mwezi. Kijana mwanamuke anayeitwa Kathleen anasema hivi: “Hata ikiwa mama yangu alinitayarisha, nilishituka sana nilipoingia kwa mara ya kwanza katika kipindi cha kuona mwezi. Nilioga maji mara nyingi kwa siku kwa sababu nilijisikia kuwa muchafu kila wakati. Tena, ndugu zangu wakubwa watatu walikuwa wananichekelea bila huruma. Walikuwa wanafikiri kwa njia fulani kwamba vipindi vyangu vyote vya kuona mwezi vilikuwa vya kuchekesha.”

Kusumbuliwa na marafiki. Marie, aliye na miaka 18 sasa, anakumbuka hivi: “Nilipokuwa na miaka kati ya 12 na 14, marafiki wenzangu walinisumbua sana. Watoto wa masomo yetu walimutendea bila huruma mutoto yeyote aliyejifanya kuwa tofauti nao.” Anita, aliye na miaka 14 anasema hivi: “Kwa miaka yangu, ni jambo la lazima kujisikia kuwa unakubaliwa na kikundi cha marafiki wenzako na kujisikia kuwa unaachwa kunavunja moyo sana.”

JAMBO UNALOWEZA KUFANYA

Umutie moyo kijana wako mwanamuke azungumuze juu ya mahangaiko yake. Kwanza, anaweza kujizuia kuzungumuza. Lakini uwe muvumilivu na ufuate shauri la Biblia la kuwa “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.”​—Yakobo 1:19.

Chukua kwa uzito mahangaiko ya kijana wako mwanamuke. Kumbuka kwamba yeye hajaona mambo mengi katika maisha, na hivyo hajapitia mambo mengi ya kulinganisha na mahangaiko yake na hajajua namna ya kushinda mahangaiko hayo.​—Kanuni ya Biblia: Waroma 15:1.

Usimupatie kijana wako mwanamuke kazi nyingi kisha masomo. Kulingana na kitabu kimoja, vijana walio na kazi nyingi “mara nyingi wanaoyesha alama za mahangaiko, zaidi sana alama kama vile maumivu ya kichwa na maumivu ya tumbo.” (Teach Your Children Well)​—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 1:9, 10.

Uhakikishe kwamba kijana wako mwanamuke analala vya kutosha. Mara nyingi kulala ndilo jambo la kwanza ambalo vijana wanazarau. Lakini, bila kulala vya kutosha, uwezo wa kufikiri wa kijana wako mwanamuke utapunguka, na hivyo hataweza kushinda mahangaiko.​—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 4:6.

Umusaidie kijana wako mwanamuke kupata njia nzuri za kuepuka mahangaiko. Kufanya mazoezi ya mwili kunasaidia vijana fulani wanawake kupunguza mahangaiko. Biblia inasema kwamba “mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” (1 Timotheo 4:8) Vijana wengine wanawake wanaona kuwa kuandika mambo yanayowasumbua kunawasaidia kushinda mahangaiko yao. Brittany aliye na miaka 22 anakumbuka hivi: “Wakati nilikuwa mudogo, nilikuwa ninaandika matatizo ambayo sikuweza kushinda. Kufanya hivyo kulinisaidia nielewe namna nilivyojisikia juu ya tatizo fulani, na kwa hiyo ilikuwa vyepesi kwangu kushinda tatizo hilo ao kuliacha tu.”

Uwe mufano muzuri. Namna gani wewe unashugulikia mahangaiko? Je, unangoja mahangaiko yawe mengi kupita uwezo wako na kuogopa wakati unapoyashugulikia? Unajichosha kwa kufanya kazi nyingi sana, na kukosa kujipangia wakati wa kufanya mambo ya maana zaidi katika maisha? Andiko la Wafilipi 4:5 linasema hivi: “Usawaziko wenu na ujulikane.” Kumbuka kwamba kijana wako anaona mufano wako na anajifunza kutokana na mufano huo, iwe katika mambo mazuri ao mambo mabaya.

^ Majina yamebadilishwa katika habari hii.