Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAMBO TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA HISTORIA | Konstantino

Konstantino

Konstantino

Konstantino alikuwa mutawala wa kwanza Muroma aliyejiita kuwa Mukristo. Kwa kujiita kuwa Mukristo, alikuja kuwa na ushawishi mukubwa sana juu ya historia ya ulimwengu. Aliamini dini hiyo iliyokuwa inateswa zamani na akaifanya kuwa Ukristo wa uongo. Kwa hiyo, kulingana na kitabu fulani, dini hiyo iliyojiita ya Kikristo ikakuwa “chombo chenye nguvu zaidi katika mambo ya jamii na ya kisiasa,” chombo ambacho kilifikia kuwa na ushawishi mukubwa zaidi katika historia yote. (The Encyclopædia Britannica)

SABABU gani ni vizuri ujue habari ya mutawala wa zamani wa Roma? Ikiwa unapendezwa na Ukristo, ni vizuri ujue kwamba ujanja wa kisiasa na wa kidini wa Konstantino ulishawishi sana mafundisho na matendo ya makanisa mengi kuanzia wakati wake mupaka leo hii. Acheni tuone namna gani.

MAKANISA YALIKUBALIWA KISHERIA NA KISHA YALITUMIWA VIBAYA

Katika mwaka wa 313 kisha kuzaliwa kwa Yesu, Konstantino alitawala Ufalme wa Roma wa Mangaribi, wakati huohuo Lisinio na Maksiminio walitawala Ufalme wa Mashariki. Konstantino na Lisinio waliwapatia watu wote uhuru wa dini, na hata Wakristo pia. Konstantino alilinda Ukristo akiamini kwamba dini italeta umoja katika ufalme wake. *

Konstantino alichukizwa sana kuona kwamba makanisa yaligawanyika kwa sababu ya magomvi. Akiwa na nia ya kupatanisha makanisa hayo, aliunda mafundisho “ya kweli” na kisha akalazimisha watu wayafuate. Ili Konstantino awapende, maaskofu walilegeza musimamo wao na wale waliofanya hivyo hawakulipishwa tena kodi na walipewa misaada fulani. Mwanahistoria Charles Freeman alisema hivi: “Kujua mafundisho ‘ya kweli’ ya Ukristo kuliwezesha watu kupata njia ya mbinguni na pia kupata utajiri mwingi duniani.” Kwa hiyo, viongozi wa dini wakakuwa watu wenye uwezo mwingi katika mambo ya dunia. Mwanahistoria Arnold Hugh Martin Jones anasema kwamba “Kanisa lilipata mulinzi, lakini lilipata pia bwana.”

“Kanisa lilipata mulinzi, lakini lilipata pia bwana.”—Mwanahistoria Arnold Hugh Martin Jones

HUO ULIKUWA UKRISTO WA AINA GANI?

Mapatano ya Konstantino pamoja na maaskofu yalitokeza dini iliyokuwa na aina mbili ya mafundisho, mafundisho ya Kikristo na mafundisho ya kipagani. Ingepaswa tu kuwa hivyo, kwa sababu Konstantino hakuwa na kusudi la kuanzisha mafundisho ya kweli ya kidini, lakini kusudi lake lilikuwa kutokeza dini nyingi. Kwa vyovyote, alikuwa mutawala mupagani. Mwanahistoria mumoja aliandika kwamba, ili kufurahisha pande zote mbili, Konstantino aliamua “kutokuwa wazi katika matendo yake na katika mambo ya serikali kwa ujumla.”

Hata kama alisema kuwa anatetea Ukristo, Konstantino aliendelea kuunga mukono dini ya kipagani. Kwa mufano, aliendelea kufanya uaguzi na kuchunguza nyota, matendo ya uchawi ambayo Biblia inakataza. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Kwenye Munara wake wa Ukumbusho ulio katika muji wa Roma, Konstatino anaonyeshwa akiwa mwenye kutolea miungu ya kipagani zabihu. Aliendelea kuabudu mungu-jua kwa kuchapisha sanamu ya mungu huyo kwenye feza za kichele na kuendeleza ibada ya mungu huyo. Katika siku za mwisho za maisha yake, Konstantino aliruhusu hata watu wa muji mudogo wa Umbria, katika inchi ya Italia, wamujengee hekalu yeye na familia yake na waweke makuhani ili watumike humo.

Konstantino alichelewesha kwa muda murefu ubatizo wake wa “Kikristo.” Alibatizwa wakati kulibakia tu siku chache mbele ya kufa kwake katika mwaka wa 337 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Watu wengi wenye elimu wanaamini kwamba alichelewesha ubatizo wake ili aendelee kuunga mukono Ukristo na dini za kipagani katika ufalme wake kupitia siasa. Bila shaka, habari ya maisha yake na kuchelewesha ubatizo wake, yote hayo yanatokeza maulizo juu ya sababu ya kweli iliyomufanya ajiite kuwa Mukristo. Hata hivyo, jambo moja ni la hakika: Kanisa ambalo Konstantino alifanya likubaliwe na sheria lilikuja kuwa chombo chenye nguvu kisiasa na kidini, liliacha mambo ya Kristo na kufuata mambo ya dunia. Yesu alisema juu ya wafuasi wake hivi: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14) Kanisa hilo, lililokuwa sasa sehemu ya ulimwengu, lilitokeza dini nyingi sana.

Mambo hayo yote yana maana gani kwetu? Yanamaanisha kwamba hatupaswi kukubali tu mafundisho ya kila dini, lakini tunapaswa kuyachunguza ili kuona ikiwa yanapatana na Biblia.​—1 Yohana 4:1.

^ Sababu ya kweli iliyomufanya Konstantino aamini Ukristo imeleta ubishi mwingi sana, kwanza kwa sababu, kulingana na kitabu fulani, “alifanya mambo yaliyoonyesha waziwazi kwamba anaunga mukono ibada ya kipagani, hata mwishoni mwa utawala wake.”