Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 KICHWA

Kupambana na Hali ya Kuchoka Mwili na Akili

Kupambana na Hali ya Kuchoka Mwili na Akili

ANIL alikuwa mwenye kuchoka sana. Alikuwa amekubali kazi mupya kwa sababu ingemuletea sifa kubwa sana na mushahara muzuri. Lakini sasa alitumika mupaka usiku sana na hata Siku ya Posho na Siku ya Yenga, wakati fulani alitumika saa 80 kwa juma. Anasema hivi: “Kazi haikupangwa vizuri na nilipaswa kushugulikia mambo yote. Nilijiuliza, ‘Nimefanya nini? Ikiwa mambo hayabadilike, nitakufa.’” Anil alichoka mwili na akili.

Kuchoka mwili na akili kwa sababu ya kazi ni tofauti na mikazo inayotokana na kazi ya kila siku. Mutu aliye katika hali hiyo anajisikia mwenye kuchoka kila siku na mwenye kusumbuka sana na mwenye kuishiwa nguvu. Wale walio katika hali hiyo wana muelekeo wa kuacha kufikiria kazi yao, wanaanza kuichukia, na hawatumike tena muzuri. Uchunguzi unaonyesha kwamba matatizo mengi ya akili na ya mwili yanatokana na hali ya kuchoka mwili na akili.

Sababu gani watu wanachoka mwili na akili? Mara nyingi kwa sababu ya kutumika sana. Kwa sababu ya matatizo ya feza, wakubwa fulani wa kazi wanaomba wafanya kazi wao watumike saa nyingi, mara nyingi kwa mushahara mudogo. Teknolojia inasaidia watu kujua kila wakati mambo yanayoendelea kwenye kazi yao, na hilo linafanya iwe vigumu kutofautisha wakati wa kazi na wakati wa kufanya mambo ya kipekee. Kwa wengine, uwezekano wa kupoteza kazi, kutojua vizuri kazi ao kufikiri kwamba unatendewa isivyo haki kunafanya wachoke mwili na akili. Pia sababu ingine ni kushugulikia mambo yanayoweza kufanywa baadaye na kutoelewana na wafanyakazi wengine.

Mutu anaweza pia kujichokesha yeye mwenyewe. Watu fulani wanajiingiza katika mambo mengi ili tu kufuatia kazi ambayo wanataka kufanya katika maisha ao kupata feza nyingi. Watu hao wanaweza kujifanya watumwa wa kazi na kwa hiyo wanaanza kujisikia wenye kuchoka mwili na akili.

Ikiwa umechoka mwili na akili kwa sababu ya kazi, unaweza kufanya nini? Kwa kweli, ikiwa umeingia katika hali zinazopita uwezo wako, unaweza kufikiri kwamba haiwezekane kubadili hali hiyo. Lakini, mambo 4 yanayofuata yanaweza kukusaidia upambane na hali ya kuchoka mwili na akili. Kuna mambo mengi unayoweza kufanya.

 1. CHUNGUZA MAMBO YA MAANA SANA KWAKO.

Ni mambo gani yaliyo ya maana sana kwako? Watu wengi wanatia pa nafasi ya kwanza uhusiano wa familia na afya nzuri. Ikiwa unachoka mwili na akili, hilo linaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya uhusiano wako na familia yako na juu ya afya yako.

Kuamua ni mambo gani utakayoshugulikia kwanza kutakusaidia uchukue maamuzi makubwa na ukubali kuacha mambo mengine. Kwa mufano, unaweza kutambua kwamba kazi yako imeanza kukuchokesha mwili na akili. Lakini unaweza kuwaza, ‘Siwezi kutafuta kazi ingine ao kutumika saa kidogo; Ninahitaji feza!’ Kwa kweli, kila mutu anahitaji feza, lakini unahitaji kiasi gani cha feza na na hilo litakuwa na matokeo gani juu ya mambo unayoona kuwa ya maana sana?

Ufanye angalisho ili usianze kufikiri kwamba mambo ambayo wengine wanaona kuwa ya maana ndiyo wewe pia unapaswa kuona kuwa ya maana. Mambo ambayo bwana wako wa kazi anaona kuwa ya maana sana na yale ambayo wewe unaona kuwa ya maana inatofautiana. Wengine wanaweza kuamua kutia kazi pa nafasi ya kwanza katika maisha yao, lakini hilo halimaanishe kama wewe pia unapaswa kuwaiga.

KANUNI YA BIBLIA: ‘HATA WAKATI MUTU ANA VITU VINGI UZIMA WAKE HAUTOKANE NA VITU ALIVYO NAVYO.’—LUKA 12:15

2. RAHISISHA MAISHA YAKO.

Ili kupunguza mikazo na kupata wakati kwa ajili ya mambo ya maana sana, unaweza kufikiria kutumika saa kidogo, unaweza kumuomba bwana wako wa kazi apunguze kazi unayofanya, ao unaweza kuamua kubadili kazi. Iwe utachukua uamuzi gani, labda itakuwa muzuri ubadili namna yako ya kutumia feza na namna yako ya kuishi. Lakini inawezekana kufanya hivyo, na si vigumu kadiri unaweza kuwazia.

Katika inchi nyingi, kompanyi moja ambayo kusudi lake kubwa ni kuuza na kuuzisha vitu inafanya watu wafikiri kwamba furaha inatokana na feza na utajiri. Lakini kwa kweli, mambo hayako hivyo. Kuishi maisha mepesi kunaweza kumusaidia mutu awe na uhuru mwingi na kutosheka zaidi. Ili kujitayarisha kwa ajili ya maisha mepesi, punguza garama zako na uanze kuweka feza. Jikaze kupunguza ao kulipa madeni yote. Zungumuza na familia yako kuhusu ulazima wa kubadili maisha yenu na uwaombe wakutegemeze.

KANUNI YA BIBLIA: ‘TUKIWA NA CHAKULA NA KITU CHA KUJIFUNIKA, TUTARIZIKA NA VITU HIVYO.’—1 TIMOTHEO 6:8

 3. USIKUBALI KAZI YOTE.

Ikiwa unapewa kazi nyingi ao kuna matatizo fulani yanayoendelea katika kazi yako, zungumuza na bwana wako wa kazi. Kila mara inapowezekana, muelezee mambo yatakayokufaidi wewe na bwana wako wa kazi. Hakikishia bwana wako wa kazi kwamba unapenda kazi yako, na umuelezee mambo ambayo uko tayari kufanya; lakini umuambie waziwazi yale ambayo hauna uwezo wa kufanya.

Tumia hekima na uone mambo namna yalivyo. Ikiwa unataka kutumika saa kidogo, pengine bwana wako wa kazi atakuomba ukubali kulipwa mushahara mudogo. Fikiria mbele ya wakati mambo kama vile kupoteza kazi, na uone utafanya nini kama inakuwa hivyo. Kumbuka kwamba kuna tumaini la kupata kazi ingine wakati ungali unatumika.

Hata wakati mumefanya mapatano pamoja na bwana wako wa kazi, unaweza kuombwa tena kufanya kazi nyingi zaidi. Ni nini inaweza kukusaidia uendelee kushikamana na uamuzi wako? Heshimia mapatano ambayo umefanya. Kufanya hivyo kunaweza kukutolea nafasi ya kuomba bwana wako wa kazi aheshimu pia mapatano muliyofanya, kutia ndani kuendelea kukupatia kiasi cha kazi kulingana na mapatano yenu.

KANUNI YA BIBLIA: “ACHENI TU NENO LENU NDIYO LIMAANISHE NDIYO, SIYO YENU, SIYO.”—MATHAYO 5:37

 4. PUMUZIKA VYA KUTOSHA.

Hata wakati hakuna matatizo makubwa katika kazi yako, unaweza kuendelea kupambana na matatizo fulani, watu wagumu, na hali zisizofurahisha. Kwa hiyo ni vizuri kuchukua wakati wa kutosha ili kupumuzika na kujifurahisha kidogo. Kumbuka kwamba si lazima utumie feza nyingi ili kujifurahisha wewe na familia yako.

Zaidi ya kazi yako, pendezwa na wengine na uanzishe urafiki nao, epuka kufikiri kwamba kazi fulani ao kutumika sana ndiko kunakufanya kuwa mutu wa maana. Sababu gani? Kitabu kimoja kinasema hivi: “Tabia zako nzuri ni za maana sana kuliko feza zako.” (Your Money or Your Life) Ikiwa kazi yako ndio inakufanya kuwa mutu wa lazima, basi itakuwa vigumu kwako kuwa na maoni yanayofaa kuhusu daraka la kazi katika maisha yako.

KANUNI YA BIBLIA: ‘KONZI MOJA YA PUMUZIKO NI AFAZALI KULIKO KONZI MBILI ZA KAZI NGUMU NA KUFUATILIA UPEPO.’—MHUBIRI 4:6

Unaweza kabisa kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili kupambana vizuri na hali ya kuchoka mwili na akili? Inawezekana. Anil, ambaye tulizungumuzia mwanzoni mwa habari hii, alifanya hivyo. Anasema: “Nilizungumuza na bwana wangu wa kazi wa zamani, nilimuuliza ikiwa anaweza kunipatia tena kazi, na alikubali. Nilisikia haya kuonana tena na wafanya-kazi wenzangu wa zamani kisha mimi kuwaambia kwamba nimepata kazi nzuri zaidi. Na nilikubali mushahara kidogo. Lakini nilipata amani ya akili, na nilikuwa na wakati mwingi wa kupitisha na familia yangu na kufanya mambo mengine yaliyo ya maana zaidi.”