Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kushugulikia Madeni

Kushugulikia Madeni

Mambo Ya Kufanya Ili Kuwa Na Furaha Katika Familia

Kushugulikia Madeni

Giannis * alisema hivi: “Biashara yangu ilihomba wakati wa matatizo ya feza yaliyotokea huko Grèce, kwa hiyo hatukuwa tena na uwezo wa kulipia nyumba na kadi zetu za mikopo. Sikuweza kulala usiku kwa sababu ya mahangaiko.”

Katerina alisema hivi: “Tulipenda sana nyumba yetu, na singeweza kukubali kabisa kuipoteza. Mara nyingi mimi na Giannis tulibishana juu ya namna tulipaswa kushugulikia deni letu.”

DENI linaweza kuleta mahangaiko katika familia ao hata kuiharibu. Kwa mufano, mutafiti Jeffrey Dew alivumbua kama bibi na bwana walio na deni hawapitishe wakati mwingi pamoja, wana ugomvi mwingi, na hawana furaha. Tukilinganisha mabishano juu ya feza na madeni na mabishano juu ya mambo mengine, imeonekana kama mabishano juu ya feza yanadumu, yanatokeza malalamiko na mapigano, na mara nyingi yanaleta mabishano juu ya mambo mengine. Kwa hiyo, haishangaze kuona kama kukosa kuelewana juu ya feza ndiyo sababu kubwa inayofanya watu wavunje ndoa huko États-Unis d’Amérique.

Madeni mengi yanaleta matatizo ya afya, kama vile kukosa usingizi, maumivu ya kichwa, maumivu ya estoma, matatizo ya moyo, na kushuka moyo. Mwanamuke mumoja anayeitwa Marta anasema hivi: “Bwana yangu, Luís, alishuka moyo sana kwa sababu ya deni tulilokuwa nalo na kwa hiyo, alikuwa analala karibu muchana muzima. Mwanaume niliyetumainia sikuzote hangeweza tena kunisaidia.” Watu fulani wanashindwa hata kuvumilia mahangaiko yanayotokana na deni. Kwa mufano, kulingana na programu moja ya radio na televizyo ya Angleterre (BBC), mwanamuke mumoja wa India alijiua aliposhindwa kulipa madeni yaliyofikia dola 840 za Amerika. Alikopa feza hizo ili kumutunzisha mutoto wake.

Utafanya nini ikiwa familia yako ina mahangaiko kwa sababu ya deni? Tuchunguze matatizo fulani ambayo familia nyingi zinapambana nayo ili kushugulikia madeni na tuone kanuni za Biblia zinazoweza kukusaidia kushinda matatizo hayo.

TATIZO LA 1: Nilimuambia bibi yangu kama kosa ni lake, naye aliniambia kama kosa ni langu.

Lukasz anasema hivi: “Nilimuambia bibi yangu kama anatumia feza vibaya, naye pia alinitupia kosa kwa kusema kama tungekuwa na feza nyingi ikiwa nilitumika kwa muda wa mwaka muzima.” Bibi na bwana wanaweza kufanya nini ili madeni yasiwatenganishe?

Siri: Kutenda kwa umoja ili kushugulikia deni. Kumukasirikia bwana ao bibi yako hakuwezi kuwasaidia kwa jambo lolote​—hata kama si wewe uliyekamata deni. Shauri la Biblia linalotolewa katika andiko la Waefeso 4:31 linasaidia watu leo kuliko wakati mwengine wowote. Linasema hivi: ‘Uchungu wote wenye uovu na hasira na gazabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.’

Mugombanishe deni kuliko kujigombanisha ninyi wawili. Bwana mumoja anayeitwa Stephanos anaeleza namna yeye na bibi yake walivyotenda kwa umoja, anasema hivi: “Tuliona deni kuwa adui yetu sisi wawili.” Kutenda huko kwa umoja kunapatana na andiko la Methali 13:10, ambalo linasema hivi: ‘Kwa sababu ya kimbelembele mutu anasababisha tu pambano, lakini wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.’ Kuliko kushugulikia deni wewe mwenyewe, uzungumuzie waziwazi jambo hilo pamoja na bwana ao bibi yako na kisha mutende kwa umoja.

Watoto wenu wanaweza pia kusaidia. Baba mumoja anayeitwa Edgardo, wa huko Argentine, anaeleza jambo lililotokea katika familia yake kwa kusema hivi: “Mutoto wangu wa mwisho alitaka tumununulie kinga mupya, lakini tulimufasiria kama hatuna uwezo wa kuinunua. Kwa hiyo, tulimupatia kinga iliyokuwa ya tate (nkambo) yake mwanaume, na akaifurahia sana. Niliona lazima ya kutenda kwa umoja katika familia.”

MUJARIBU KUFANYA HIVI: Mupange wakati ili kuzungumuzia madeni yenu waziwazi na kwa utulivu. Kila mutu akubali makosa ambayo labda amefanya. Kuliko kukazia akili mambo yaliyopita, mujaribu kukubaliana juu ya kanuni za Biblia zitakazowasaidia kuchukua maamuzi mazuri juu ya feza wakati unaokuja.​—Zaburi 37:21; Luka 12:15.

TATIZO LA 2: Wakati inaonekana kuwa vigumu kulipa deni.

Enrique anasema hivi: “Nilikuwa na deni kubwa kwa sababu ya biashara yangu, deni hilo likakuwa tena kubwa zaidi wakati kulikuwa matatizo ya feza huko Argentine. Kisha bibi yangu alihitaji kupasuliwa. Nilijisikia kuwa singeweza tena kulipa deni hilo, ni sawa vile nilinaswa katika mutego.” Mwanaume mumoja anayeitwa Roberto, wa huko Brezil, alipoteza feza zake zote katika biashara fulani na alikuwa na madeni kwenye benki 12. Anasema hivi: “Nilikuwa ninasikia haya sana kukutana na marafiki wangu. Nilijisikia kama mutu aliyeshindwa katika muchezo.”

Unaweza kufanya nini ikiwa unajisikia kuwa mwenye kuvunjika moyo sana, mwenye kosa, ao ikiwa unasikia haya kwa sababu ya deni lako?

Siri: Upange namna ya kutumia feza zako. *

1. Ujue kiasi cha feza ulizo nazo. Andika feza zote zinazotoka na kuingia katika familia yenu kwa muda wa majuma mawili ao mwezi mumoja, ikiwa ni jambo lenye kufaa zaidi. Kwenye karatasi hiyo, uongeze pia garama ambazo haufanye kwa ukawaida, kama vile garama za kodi, mavazi, ao matunzo, na ukadirie feza unazotumia kwa ajili ya mambo hayo kila mwezi.

2. Uongeze mapato yako. Zaidi ya kazi yako, unaweza kufanya kazi zingine kama vile kufundisha mwanafunzi fulani nyumbani kwao, kufuga wanyama, ao kufanya biashara fulani nyumbani kwako. Angalisho: Usiache kazi zako zichukue nafasi ya mambo ya maana zaidi, kama vile mambo ya kiroho.

3. Upunguze garama zako. Ununue kitu ikiwa unakihitaji kabisa, si kwa sababu tu kimepunguzwa bei. (Methali 21:5) Enrique, aliyetajwa hapo juu, anasema hivi: “Ni vizuri kungojea mbele ya kununua kitu fulani, kwa sababu kungojea kutakusaidia kuamua ikiwa unahitaji kitu hicho kabisa ao unakitaka tu.” Ona mapendekezo fulani:

● Makao: Ikiwezekana, uhamie katika nyumba ambamo utalipa feza kidogo kwa mwezi. Upunguze garama zako za lazima kwa kutumia vizuri maji, umeme (courant), na vitu vingine.

● Chakula: Unapoenda mahali fulani, ufunge chakula chako kuliko kununua chakula kwa ukawaida. Ununue vitu mahali ambapo vinapunguzwa bei. Joelma anayeishi huko Brezil anasema hivi: “Ninapunguza garama zangu kwa kununua matunda na mboga za majani kwenye soko za barabarani mbele wale wanaouzisha wafunge vitu vyao.”

● Usafirishaji: Ikiwezekana, utumie aina ya usafirishaji isiyoomba feza nyingi ao utembee kwa miguu.

Ukiisha kupunguza garama, unaweza kutumia vizuri feza zako.

4. Ujue deni ulilo nalo na utende. Kwanza, ujue faida ya kurudisha kwa kila mukopo, kodi unazopaswa kulipa, matokeo ya kuchelewa kulipa mukopo ao kukosa kuulipa. Uchunguze vizuri sana maneno yaliyo kwenye kadi za mikopo, kwa sababu wale waliokukopesha wanaweza kudanganya. Kwa mufano, shirika fulani la mikopo huko États-Unis d’Amérique lilionyesha kama faida ya kurudisha kwa mukopo ilikuwa 24%, ijapokuwa ilikuwa zaidi ya 400%.

Tena, ujue namna utakavyolipa madeni yako. Namna moja ni kulipa kwanza mikopo inayoomba kurudisha faida nyingi. Namna nyingine ni kulipa kwanza mikopo inayoomba kurudisha faida kidogo, kwa sababu hautahangaika sana ikiwa hauna madeni mengi ya kulipa kila mwezi. Ikiwa una mikopo inayoomba kurudisha faida nyingi, unaweza kuchukua mukopo mwengine unaoomba kurudisha faida kidogo ili kukusaidia kulipa mikopo ya kwanza.

Mwishowe, ikiwa unashindwa kurudisha faida ulizoombwa, ujaribu kuzungumuza na wale waliokukopesha. Unaweza kuwaomba wakuongezee siku ao wakupunguzie faida unazoombwa kurudisha. Watu fulani waliokukopesha wanaweza hata kukubali kukupunguzia faida unazoombwa kurudisha ikiwa unaweza kuzilipa zote palepale. Useme kweli na kwa heshima unapowafasiria tatizo lako la feza. (Wakolosai 4:6; Waebrania 13:18) Uandike makubaliano yote. Hata ikiwa wale waliokukopesha hawakubali ombi lako la kwanza, usichoke, uendelee kuwaomba wakupunguzie ikiwa ni lazima.—Methali 6:1-5.

Unaposhugulika na feza, uwe tayari kukubali hali yoyote inayoweza kutokea. Hata mipango mizuri zaidi inaweza kukosa kuwa na matokeo mazuri kwa sababu ya hali ambazo haukutazamia. Biblia inaonyesha kama mara nyingi feza ‘zinajifanyia mabawa kama yale ya tai na kuruka kuelekea mbinguni.’​—Methali 23:4, 5.

MUJARIBU KUFANYA HIVI: Mukiisha kupanga namna ya kutumia feza zenu, muzungumuzie jambo ambalo kila mumoja anaweza kufanya ili kupunguza garama ao kuongeza mapato ya familia. Kuona namna kila mutu anavyojinyima kunaweza kuwasaidia muungane mukono katika kushugulikia madeni.

TATIZO LA 3: Madeni yanachosha akili zetu.

Mutu anapojikaza kushugulikia madeni, anaweza kusahau mambo ya lazima zaidi maishani. Mwanaume mumoja anayeitwa Georgios alisema hivi: “Tatizo kubwa ni kwamba madeni yetu ndilo lilikuwa hangaiko la kwanza katika maisha yetu. Mambo ambayo tulipaswa kutia pa nafasi ya kwanza ndiyo tulitia pa nafasi ya pili.”

Siri: Usitie feza pa nafasi ya kwanza. Hata ujikaze namna gani, inawezekana uendelee kuwalipa wale waliokukopesha kwa miaka mingi. Lakini, unaweza kuchagua namna utakavyoshugulikia hali zako. Kuliko kujihangaisha sana juu ya feza, ni vizuri kufuata shauri hili la Biblia: ‘Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutarizika na vitu hivyo.’​—1 Timotheo 6:8.

Kurizika na hali yako kutakuwezesha ‘kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:10) Kati ya ‘mambo hayo ya maana zaidi’ kuna urafiki wako pamoja na Mungu na urafiki wako pamoja na familia yako. Georgios, aliyetajwa hapo juu, anasema hivi: “Hata ikiwa hatujamaliza kulipa madeni yetu yote, madeni hayako tena hangaiko la kwanza katika maisha yetu. Sasa tuna furaha zaidi katika ndoa yetu kwa sababu tunapitisha wakati mwingi pamoja na watoto wetu, na sisi wawili pia, na tunapitisha wakati mwingi katika mambo ya kiroho.”

MUJARIBU KUFANYA HIVI: Muandike mambo ya lazima sana kwenu ambayo feza haziwezi kununua. Kisha, muone namna gani munaweza kuongeza wakati na nguvu munazotumia juu ya kila jambo.

Madeni yanaleta mahangaiko, na inaomba kujinyima ili kushugulika nayo; lakini bidii ambayo mutu anafanya si ya bure. Bwana mumoja anayeitwa Andrzej, wa huko Polonye, anasema hivi: “Nilipojua kama bibi yangu alimukopesha mufanyakazi mwenzake feza nyingi sana na kama mufanyakazi huyo alikufa bila kulipa feza hizo, hali ilichacha sana katika nyumba yetu.” Lakini anapokumbuka namna yeye na bibi yake walivyoshugulikia tatizo hilo, anasema hivi: “Sasa sisi ni wenye kuungana zaidi—si kwa sababu ya tatizo hilo, lakini namna tulivyotenda kwa umoja ili kulishugulikia.”

[Maelezo ya chini]

^ Majina fulani yamebadilishwa.

^ Ili kupata habari zingine, usome habari yenye kichwa “Jinsi ya Kupangia Matumizi ya Pesa Zako” katika Amkeni! ya Mwezi wa 9, 2011 iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

UJIULIZE . . .

▪ Ninaweza kufanya nini ili kusaidia familia yangu ishugulikie madeni?

▪ Tunaweza kufanya nini ili deni lisiwe hangaiko kubwa katika maisha ao lisiharibu urafiki katika familia yetu?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Deni linaweza kuleta mahangaiko katika familia ao hata kuiharibu

[Picha katika ukurasa wa 20]

Katika familia, kila mutu ajue namna mbalimbali za kushugulikia madeni

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kurizika kunaleta furaha ambayo feza haziwezi kuleta