Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Tunapaswa Kusali kwa Watakatifu?

Je, Tunapaswa Kusali kwa Watakatifu?

NI NANI kati yetu ambaye hajapata mahangaiko na kusikia uhitaji wa kumuendea mutu fulani ili kumuomba musaada? Kulingana na mambo yanayoleta mahangaiko, tunaweza kumuendea rafiki aliye mwenye huruma na aliye na ujuzi juu ya tatizo ambalo tunapambana nalo. Kuwa mwenye huruma na mwenye ujuzi zaidi juu ya tatizo hilo kunamufanya awe rafiki ambaye tunatamani kumuendea.

Watu fulani wanaweza kufikiri hivyo kuhusu sala. Kuliko kumukaribia Mungu ambaye anaonekana kuwa juu sana na mwenye kuogopesha, wanajisikia vizuri kusali kwa mumoja wa watakatifu. Wanafikiri watakatifu wanaweza kuwaelewa vizuri kwa sababu wamepatwa na majaribu na mateso ambayo yanapata wanadamu. Kwa mufano, watu ambao wamepoteza kitu fulani ambacho wanaona kuwa cha maana wanaweza kuona vizuri kusali kwa “Mutakatifu” Antoine wa Padua ambaye wanaamini kuwa mulinzi wa vitu vilivyookotwa ao kuibwa. Ikiwa wanaombea munyama anayegonjwa, wanaweza kuamua kusali kwa “Mutakatifu” Francis wa Assisi ao kwa “Mutakatifu” Yuda Thadayo ikiwa wanavunjika moyo.

Basi, namna gani tunaweza kujua ikiwa kusali kwa watakatifu ni jambo linalolingana na maandiko? Kwa kuwa wakati tunasali tunazungumuza na Mungu, tunapaswa kujiuliza hivi: Je, Mungu anasikiliza sala zetu? Tunapaswa pia kujiuliza hivi: Mungu anajisikia namna gani watu wanaposali kwa watakatifu?

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA KUHUSU KUSALI KWA WATAKATIFU

Zoea la kusali kwa watakatifu linategemea fundisho la kwamba watakatifu wanaweza kuwaombea wengine, linalofundishwa na Kanisa la Katoliki. Kulingana na kitabu kimoja (New Catholic Encyclopedia), wazo kubwa ni kwamba “ili kupata rehema ni vizuri kuombewa na mutu ambaye machoni pa Mungu ana haki ya kufanya hivyo.” Kwa hiyo, watu wanaosali kwa watakatifu wanafanya hivyo wakiwa na tumaini la kupata kibali cha pekee kupitia watakatifu hao kwa sababu ya cheo chao chenye kuheshimika mbele za Mungu.

Je, Biblia inakubali fundisho kama hilo? Watu fulani wanasema kwamba mutume Paulo ndiye alianzisha fundisho la kusali kwa watakatifu katika maandishi yake. Kwa mufano, aliwaandikia Wakristo wa Roma hivi: ‘Sasa nawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia Bwana wetu Yesu Kristo na kupitia upendo wa roho, kwamba mujikaze pamoja nami katika sala kwa Mungu kwa ajili yangu.’ (Waroma 15:30) Paulo aliposema hivyo, je, alikuwa akiwaomba Wakristo wenzake wawe wapatanishi kati yake na Mungu? Hapana. Ingekuwa hivyo, Paulo, aliyekuwa mutume wa Kristo, ndiye wangeomba awe mupatanishi kati yao na Mungu. Paulo alikuwa anaonyesha kwamba ni jambo lenye kufaa kumuomba Mukristo mwenzetu asali kwa Mungu kwa ajili yetu. Hilo ni tofauti kabisa na kusali kwa mutu fulani anayeaminiwa kuwa mbinguni ili ajulishe Mungu maombi yetu. Sababu gani tunasema hivyo?

Katika Injili ya mutume Yohana, Yesu anasema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Tena anasema hivi: ‘Lolote mutakalomuomba Baba kwa jina langu, atawapa ninyi.’ (Yohana 15:16) Yesu hakusema kwamba sala zetu zinapaswa kumuendea yeye na kwamba yeye angetusemea kwa Mungu. Lakini, ili sala zetu zisikiwe, tunapaswa kusali kwa Mungu kupitia Yesu na si kupitia mutu mwengine yeyote.

Wakati wanafunzi wa Yesu walimuomba awafundishe namna ya kusali, Yesu aliwajibu hivi: ‘Wakati wowote munaposali, semeni, Baba, jina lako na litakaswe.’ (Luka 11:2) Kwa kweli, “wakati wowote,” ao kila wakati tunaposali, tunapaswa kuelekeza sala zetu kwa Mungu mwenyewe, si kwa Yesu ao mutu mwengine yeyote. Kwa sababu ya fundisho hilo la Yesu lililo wazi, ni jambo lenye kueleweka kusema kwamba sala zetu zinapaswa kuelekezwa kwa Mungu kupitia Yesu Kristo na si kupitia kwa mupatanishi yeyote ao “watakatifu.”

Sala ni sehemu ya maana sana ya ibada yetu, na kumuabudu mutu mwengine yeyote isipokuwa Mungu hakupatane na mafundisho ya Biblia. (Yohana 4:23, 24; Ufunuo 19:9, 10) Ndiyo maana tunapaswa kuelekeza sala zetu kwa Mungu peke yake.

JE, UNAPASWA KUOGOPA KUMUKARIBIA MUNGU?

Katika Mafundisho yake ya Mulimani, Yesu alitoa mufano wa mutoto ambaye anamuomba baba yake kitu fulani cha kula. Je, baba angeweza kumupatia mutoto wake jiwe mahali pa mukate? Ao nyoka mwenye sumu mahali pa samaki? (Mathayo 7:9, 10) Haiwezekane baba mwenye upendo afanye jambo kama hilo!

Kama vile baba na mutoto wake, Mungu anataka tuzungumuze naye

Wazia mufano huohuo ukiwa muzazi. Wazia mutoto wako ana jambo fulani la kukuomba ambalo anataka kupata kabisa. Umejikaza kulinda uhusiano pamoja naye, na sikuzote umekuwa mwenye kukaribiwa kwa urahisi. Hata hivyo, kwa kuwa anaogopa bila sababu namna utatenda, anamuomba mutu mwengine amusemee kwako. Utajisikia namna gani? Na namna gani ikiwa anazoea kuzungumuza na wewe kupitia mutu mwengine na kuna mambo yanayokuonyesha kwamba ataendelea kufanya hivyo. Je, utafurahia mupango huo? Hapana kabisa. Wazazi wenye upendo wanataka watoto wao wawakaribie moja kwa moja na wanataka watoto wajisikie huru kuwaomba kitu chochote wanachohitaji.

Ili kuonyesha jambo la kujifunza kutokana na mufano wa mutoto anayemuomba baba yake chakula, Yesu aliwauliza watu hivi: ‘Kwa hiyo, ikiwa ninyi, mujapokuwa waovu, munajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo nzuri, je, Baba yenu aliye mbinguni hatawapa hata zaidi vitu vyema wale wanaomuomba?’ (Mathayo 7:11) Bila shaka, muzazi ana hamu kubwa ya kumupatia mutoto wake vitu vizuri. Baba yetu wa mbinguni ana hamu kubwa hata zaidi ya kusikiliza na kujibu sala zetu.

Mungu anataka tumukaribie moja kwa moja katika sala ikiwa tunalemewa na makosa yetu wenyewe. Hawapatie watu wengine daraka la kusikiliza sala zetu. Biblia inamutia moyo kila mumoja wetu hivi: ‘Mutupie Yehova muzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.’ (Zaburi 55:22) Kuliko kutegemea kupatanishwa na Mungu kupitia watakatifu ao kupitia mutu mwengine yeyote, tunapaswa kuwa na maoni mazuri juu ya Yehova Mungu.

Baba yetu wa mbinguni anahangaikia kila mumoja wetu kipekee. Anapenda kutusaidia kuhusu magumu yetu na anatualika tumukaribie. (Yakobo 4:8) Sisi ni wenye furaha kabisa kuwa na nafasi ya kumukaribia Mungu na Baba yetu, aliye ‘Musikiaji wa sala’!​—Zaburi 65:2.