Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Ni Nani Aliyemuumba Mungu?

Ni Nani Aliyemuumba Mungu?

Ufikirie baba anayezungumuza na mutoto wake mwanaume aliye na miaka saba. Anamuambia mutoto wake hivi: “Zamani, zamani sana, Mungu aliumba dunia na kila kitu kilicho ndani yake, na aliumba jua, mwezi, na nyota.” Mutoto huyo mwanaume anawaza juu ya jambo hilo kwa muda mufupi kisha anauliza, “Baba, ni nani aliyemuumba Mungu?”

Baba anamujibu, “Hakuna mutu aliyemuumba Mungu. Amekuwako siku zote.” Maelezo hayo mepesi yanamufurahisha mutoto huyo wakati huo. Hata hivyo, anapoendelea kukomaa, ulizo hilo linaendelea kumupendeza. Anaona kwamba ni vigumu kuelewa namna gani mutu anaweza kuwa bila mwanzo. Anaona hivyo kwa sababu hata ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Anajiuliza, ‘Mungu alitoka wapi?’

Biblia inajibu ulizo hilo namna gani? Kwa kweli, Biblia pia inatoa jibu linalofanana na jibu la baba katika mufano wetu. Musa aliandika hivi: ‘Ee Yehova, kabla ya kuzaliwa kwa milima, ao kutokezwa kwa dunia na inchi yenye kuzaa kana kwamba kwa maumivu ya kuzaa, tangu wakati usio na kipimo mupaka wakati usio na kipimo wewe ni Mungu.’ (Zaburi 90:1, 2) Nabii Isaya naye alisema hivi: ‘Je, haujajua ao, je, haujasikia? Yehova, Muumba wa miisho ya dunia, ni Mungu mupaka wakati usio na kipimo’! (Isaya 40:28) Vilevile, barua ya Yuda inaeleza kwamba Mungu amekuwapo “kwa umilele wote uliopita.”—Yuda 25.

Maandiko hayo yanatuonyesha kwamba Mungu ni ‘Mufalme wa umilele,’ kama vile mutume Paulo anavyoeleza. (1 Timotheo 1:17) Hilo linaonyesha kwamba Mungu amekuwako siku zote, hata iwe tunafikiria miaka ngapi iliyopita. Na ataendelea kuwapo wakati unaokuja. (Ufunuo 1:8) Kwa hiyo, kwa kuwa amekuwapo milele hilo linahakikisha kwamba yeye ni Mweza-Yote.

Sababu gani tunaona kuwa ni vigumu kuelewa wazo hilo? Kwa sababu maisha yetu ni mafupi, tunaelewa wakati kwa njia tofauti kabisa na namna Yehova anavyouelewa. Kwa sababu Mungu ni wa milele, kwake miaka elfu ni kama siku moja. (2 Petro 3:8) Kwa mufano: Je, panzi anayeishi tu siku 50, anaweza kuelewa urefu wa maisha yetu wa miaka 70 ao 80? Hawezi kabisa kuelewa! Hata hivyo, Biblia inaeleza kwamba tuko kama panzi inapotulinganisha na Muumbaji wetu Mukubwa. Hata uwezo wetu wa kufikiri unaonekana kuwa kidogo sana unapolinganishwa na uwezo wake. (Isaya 40:22; 55:8, 9) Kwa hiyo, kuna utu ao namna ya kuwa ya Yehova ambayo wanadamu hawaelewe kabisa.

Hata ikiwa wazo la kwamba kuna Mungu wa milele linaweza kuwa ngumu kuelewa, tunaona kwamba wazo hilo linapatana na akili. Ikiwa kuna mutu fulani aliyemuumba Mungu, mutu huyo anapaswa kuwa ndiye Muumba. Lakini, Biblia inasema kwamba ni Yehova tu ndiye ‘aliyeumba vitu vyote.’ (Ufunuo 4:11) Zaidi ya hilo, tunajua kwamba wakati fulani ulimwengu haukuwa. (Mwanzo 1:1, 2) Ulimwengu ulitoka wapi? Muumbaji wake alipaswa kuwa kwanza. Aliishi pia mbele ya kuumbwa kwa viumbe vyote vyenye akili, kama vile Mwana wake muzaliwa-pekee na malaika. (Ayubu 38:4, 7; Wakolosai 1:15) Kwa hiyo, ni wazi kwamba aliishi kwanza peke yake. Haiwezekane kwamba aliumbwa kwa sababu hakuna kitu kilikuwapo ambacho kingemuumba.

Kuwapo kwetu na kuwapo kwa ulimwengu wote muzima kunahakikisha kwamba kuna Mungu wa milele. Yule aliyeumba ulimwengu wetu mukubwa, Yule aliyeweka sheria za kuuongoza, anapaswa kuwa alikuwapo sikuzote. Ni kwa sababu hiyo tu ndipo alipulizia vitu vingine vyote pumuzi ya uzima.—Ayubu 33:4. ▪