Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Nilikuwa Ninapiganisha Ukosefu wa Haki na Jeuri

Nilikuwa Ninapiganisha Ukosefu wa Haki na Jeuri
  • ALIZALIWA MWAKA WA: 1960

  • INCHI: LEBANONI

  • ALIKUWAFUNDI KATIKA MUCHEZO WA KUNG FU

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilikomalia katika muji wa Rmaysh, ulio karibu na mupaka wa Israeli na Lebanoni, wakati wa vita ya kiraia. Ninaendelea kukumbuka vizuri milipuko ya mabomu yaliyotegwa katika udongo na watu wengi wasio na kosa waliopoteza mikono na miguu yao. Maisha yalikuwa magumu, na watu walikuwa wanauana na walikuwa wenye jeuri (kupigana na kuumizana).

Familia yetu ilikuwa katika Kanisa la Wamaronite, moja kati ya Makanisa ya Kikatoliki ya Mashariki. Sikuzote, baba alifanya kazi nyingi akihangaikia familia yetu ya watu 12, lakini mama alifanya yote ili tuende naye kwenye kanisa. Kisha wakati fulani, nilianza kuona kwamba kama jamii kwa ujumla, dini pia ilishindwa kusaidia watu walio wazaifu.

Nilipokuwa na miaka kati ya 13 na 19, nilipendezwa na muchezo wa kung fu. Nilifuata mafunzo magumu na nikakuwa na ufundi wa kupigana kwa kutumia mikono na miguu na katika kutumia silaha mbalimbali za michezo ya kupigana. Niliwaza, ‘Siwezi kumaliza vita, lakini ninaweza kujaribu kuzuia watu wenye kupigana na kuumizana.’ Wakati niliona watu wawili wakipigana, mara moja niliwaachanisha. Nilikuwa ninafoka kwa vyepesi na nilikasirika haraka. Watu katika eneo lote la kusini mwa inchi ya Lebanoni waliniogopa, kwa sababu nilikuwa ninapiganisha ukosefu wa haki na jeuri.

Katika mwaka wa 1980, nilijiunga na kikundi cha kung fu katika muji wa Beirut. Mabomu, makombora, na roketi vilianguka kila siku, lakini sikuacha kuenda kwenye mazoezi yangu. Maisha yangu yote yalikuwa tu kula, kulala, na kuishi kama Bruce Lee, muchezaji mukubwa wa kung fu aliye Muchina na Muamerika. Niliiga namna yake ya kutengeneza nywele, namna yake ya kutembea, na namna yake ya kulalamika anapocheza kung fu. Sikuwa na sura ya kicheko hata siku moja.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Nilikuwa na kusudi la kuwa muchezaji wa kung fu wa hali ya juu katika inchi ya China. Siku moja mangaribi, nilipokuwa nikifanya mazoezi sana ili kutayarisha safari yangu kuenda China, nilisikia watu wanagonga kwenye mulango. Rafiki yangu mumoja alikuja na Mashahidi wa Yehova wawili. Nilikuwa mwenye kuvalia mavazi meusi ya mazoezi, na jasho ilikuwa ikiteremuka kwenye mwili wangu. Niliwaambia, “Sijue kitu  chochote juu ya Biblia.” Sikujua hata kidogo kwamba kuanzia wakati huo na kuendelea, maisha yangu yangebadilika.

Mashahidi hao walinionyesha kupitia Biblia sababu gani wanadamu wenyewe hawawezi hata kidogo kumaliza kabisa ukosefu wa haki na jeuri. Walinifasiria kwamba Shetani Ibilisi ndiye anayeleta matatizo kama hayo. (Ufunuo 12:12) Nilipendezwa na amani na uhakika ambao Mashahidi wa Yehova walionyesha. Na niliguswa moyo wakati walinifundisha kwamba Mungu ana jina. (Zaburi 83:18) Walinionyesha pia andiko la 1 Timotheo 4:8, linalosema hivi: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo; lakini ujitoaji-kimungu ni wenye faida kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.” Maneno hayo yalikuwa na matokeo makubwa katika maisha yangu.

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba sikuonana tena na Mashahidi wa Yehova, kwa kuwa watu wa familia yangu waliwaambia wasirudi tena. Hata hivyo, niliamua kuacha muchezo wa kung fu na kuanza kujifunza Biblia. Ndugu zangu hawakupendezwa na wazo hilo, lakini niliamua kuwatafuta tena Mashahidi wa Yehova ili wanifundishe Biblia.

Niliendelea kuwatafuta Mashahidi wa Yehova lakini sikuwapata. Wakati huohuo, nilihuzunishwa sana na kifo cha gafula cha baba yangu, na matukio mengine yenye kuhuzunisha yaliyopata familia yetu. Nilikuwa nimeanza kutumika kwenye kompanyi ya ujenzi, na siku moja mufanyakazi mwenzangu anayeitwa Adel alinisimamisha na kuniuliza sababu gani nilionekana kuwa mwenye huzuni. Alianza kunieleza juu ya tumaini la Biblia la ufufuo. Miezi kenda baadaye, Shahidi huyo mwenye upendo, mwenye kuhangaikia wengine alinifundisha Biblia kwa uvumilivu.

Funzo lilipoendelea, nilianza kuona ulazima wa kufanya mabadiliko makubwa katika namna yangu ya kuwa. Haikuwa vyepesi kufanya hivyo. Nilikuwa mwenye hasira sikuzote na nilichokozeka kwa vyepesi. Kupitia Biblia nilijifunza namna ya kuzuia hasira yangu na kuacha kutimiza kila tamaa inayojitokeza. Kwa mufano, andiko la Mathayo 5:44 lina shauri hili la Yesu: ‘Muendelee kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.’ Na andiko la Waroma 12:19 linaonya hivi: ‘Musijilipizie kisasi wenyewe. Kwa maana imeandikwa: Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’ Maandiko hayo na maandiko mengine yalinisaidia pole kwa pole kupata amani katika moyo wangu.

FAIDA AMBAYO NIMEPATA:

Hata ikiwa mwanzoni watu wa familia yangu hawakupendezwa na uamuzi wangu wa kujifunza na Mashahidi wa Yehova, wamefikia kuwaheshimu Mashahidi wa Yehova. Mumoja kati ya ndugu zangu amejiunga na mimi katika ibada ya Yehova, na Mama alitetea imani yetu kwa wengine mupaka alipokufa.

Nimebarikiwa pia kwa kumupata Anita, bibi muzuri tena mwaminifu, ambaye ni mufanyakazi mwenzangu mupendwa katika utumishi wa wakati wote. Kuanzia mwaka wa 2000, mimi na Anita tunaishi katika muji wa Eskilstuna, Suède, ambako tunasaidia kufundisha Biblia watu wanaosema Kiarabu.

Ningali ninahangaikia watu wanaosumbuliwa na jeuri. Lakini kujua sababu inayofanya kuwe jeuri na kujua kwamba hivi karibuni Mungu ataimaliza kunaniletea furaha ya kweli na amani.—Zaburi 37:29.

Mimi na bibi yangu tuna furaha sana katika mahubiri. Tunapenda kuwafundisha wengine juu ya Yehova