Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Magonjwa ya Mlipuko?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Magonjwa ya Mlipuko?

Jibu la Biblia

 Biblia ilitabiri kwamba magonjwa (magonjwa yanayoenea sana, kutia ndani ya mlipuko) yangetokea katika siku za mwisho. (Luka 21:11) Magonjwa hayo ya mlipuko, au tandavu, si adhabu kutoka kwa Mungu. Kwa kweli, kupitia Ufalme wake, Mungu ataondoa matatizo yote ya afya hivi karibuni, kutia ndani magonjwa ya mlipuko.

 Je, Biblia ilitabiri kuhusu magonjwa ya mlipuko?

 Biblia haitabiri magonjwa hususa ya mlipuko, kama vile ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19), UKIMWI, au homa ya Hispania. Lakini inatabiri kuhusu “magonjwa” (au “tauni,” UV) na “ugonjwa hatari.” (Luka 21:11; Ufunuo 6:8) Matukio hayo ni sehemu ya ishara ya “siku za mwisho,” inayorejelewa pia kuwa “umalizio wa mfumo wa mambo.”—2 Timotheo 3:1; Mathayo 24:3.

 Je, Mungu amewahi kuwaadhibu watu kwa magonjwa?

 Biblia inaripoti pindi fulani ambazo Mungu alitumia magonjwa kuadhibu watu. Kwa mfano, aliwapiga watu fulani kwa ukoma. (Hesabu 12:1-16; 2 Wafalme 5:20-27; 2 Mambo ya Nyakati 26:16-21) Hata hivyo, matukio hayo machache hayakuwa magonjwa ya mlipuko ambayo yaliambukiza pia watu wasio na hatia. Badala yake, matukio hayo yalikuwa hukumu hususa dhidi ya watu waliokuwa wamemwasi Mungu moja kwa moja.

 Je, magonjwa ya mlipuko leo ni adhabu kutoka kwa Mungu?

 Hapana. Watu fulani wanadai kwamba Mungu anatumia magonjwa ya mlipuko na magonjwa mengine kuwaadhibu watu leo. Hata hivyo, Biblia haiungi mkono wazo hilo. Kwa nini?

 Sababu moja ni kwamba baadhi ya waabudu wa Mungu—wa nyakati za kale na wa sasa—wamewahi kusumbuliwa na magonjwa. Kwa mfano, Timotheo, aliyekuwa mwanamume mwaminifu, alisumbuliwa na “ugonjwa . . . wa mara kwa mara.” (1 Timotheo 5:23) Lakini Biblia haisemi kwamba hilo lilionyesha hakuwa na kibali cha Mungu. Vivyo hivyo leo, baadhi ya watumishi waaminifu wa Mungu huwa wagonjwa au huambukizwa magonjwa. Mara nyingi, magonjwa hayo huwapata kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa.—Mhubiri 9:11.

 Sababu nyingine ni kwamba Biblia inafundisha wakati wa Mungu wa kuwaadhibu wakosaji bado haujafika. Badala yake tunaishi katika “siku ya wokovu”​—yaani, kipindi cha wakati ambacho Mungu ametoa mwaliko kwa wanadamu wote wanaotaka wamkaribie na kuokolewa. (2 Wakorintho 6:2) Njia moja anayotutolea mwaliko huo ni kupitia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo ina ujumbe wenye kupendeza​—“habari njema ya Ufalme.”​—Mathayo 24:14.

 Je, magonjwa ya mlipuko yatakwisha?

 Ndiyo. Biblia inatabiri kwamba hivi karibuni sana hakuna mtu atakayekuwa mgonjwa. Ufalme utakapotawala, Mungu ataondoa matatizo yote ya afya. (Isaya 33:24; 35:5, 6) Ataondoa kuteseka, maumivu, na kifo. (Ufunuo 21:4) Atawafufua wale ambao wamekufa ili wafurahie afya nzuri duniani chini ya hali kamilifu.—Zaburi 37:29; Matendo 24:15.

 Mistari ya Biblia kuhusu magonjwa

 Mathayo 4:23: “Kisha [Yesu] akaenda katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuwaponya watu kila aina ya ugonjwa na kila aina ya udhaifu.”

 Maana: Miujiza ya Yesu ilionyesha kwa kiasi kidogo kile ambacho Ufalme wa Mungu utawafanyia wanadamu hivi karibuni.

 Luka 21:11: “Kutakuwa na . . . magonjwa.”

 Maana: Matatizo ya afya yaliyoenea ni ishara ya siku za mwisho.

 Ufunuo 6:8: “Tazama! farasi wa rangi ya kijivu, na yule aliyeketi juu yake alikuwa na jina Kifo. Na Kaburi lilikuwa likimfuata kwa ukaribu. Nao wakapewa mamlaka . . . ili kuua kwa . . . ugonjwa hatari.”

 Maana: Unabii kuhusu wapanda-farasi wanne wa Ufunuo unaonyesha kwamba magonjwa ya mlipuko yangetokea katika siku zetu.