Hamia kwenye habari

Ni Nini Ishara ya “Siku za Mwisho”?

Ni Nini Ishara ya “Siku za Mwisho”?

Jibu la Biblia

 Biblia inafafanua matukio, hali, na mitazamo ambayo ingetambulisha “umalizio wa mfumo wa mambo,” au “mwisho wa dunia.” (Mathayo 24:3; Union Version) Biblia inakiita kipindi hicho “siku za mwisho” au “wakati wa mwisho.”​—2 Timotheo 3:1; Danieli 8:19; Biblia Habari Njema.

Ni nini baadhi ya mambo ambayo Biblia ilitabiri kuhusu “siku za mwisho”?

 Biblia ilitabiri mambo mengi ambayo yangetukia wakati uleule na kuwa “ishara” ya kutambulisha siku za mwisho. (Luka 21:7) Ona mifano kadhaa:

 Vita. Yesu alitabiri: “Taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Pia, Ufunuo 6:4 ilitabiri kwamba mpanda-farasi wa mfano anayewakilisha vita, ‘angeondoa amani duniani.’

 Njaa kali. Yesu alitabiri: “Kutakuwa na upungufu wa chakula.” (Mathayo 24:7) Kitabu cha Ufunuo kilitabiri kuhusu mpanda-farasi mwingine wa mfano, ambaye angeleta njaa kali katika sehemu nyingi duniani.​—Ufunuo 6:5, 6.

 Matetemeko makubwa ya ardhi. Yesu alisema kwamba kutakuwa na “matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali.” (Mathayo 24:7; Luka 21:11) Matetemeko hayo makubwa yangesababisha kuteseka na vifo vingi kuliko wakati mwingine wowote ulimwenguni pote.

 Magonjwa. Yesu alisema kungekuwa na milipuko ya magonjwa na “tauni.”​—Luka 21:11, Union Version.

 Uhalifu. Ingawa uhalifu umekuwepo kwa karne nyingi, Yesu alitabiri kwamba katika siku za mwisho, kutakuwa na “kuongezeka kwa uasi sheria.”​—Mathayo 24:12.

 Kuharibu dunia. Ufunuo 11:18 inatabiri kwamba wanadamu ‘wangeiharibu dunia.’ Wangeiharibu dunia si kwa kufanya mambo mabaya tu, bali pia kwa kuharibu mazingira.

 Mitazamo Inayozorota. Katika 2 Timotheo 3:1-4, Biblia ilitabiri kwamba watu kwa ujumla wangekuwa “wasio na shukrani, wasio washikamanifu, . . . wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, waliojaa kiburi.” Ilitabiriwa kwamba watu wangeonyesha mitazamo hiyo kwa kiwango kikubwa sana hivi kwamba kipindi hicho kingeitwa kwa usahihi, “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”

 Kuvunjika kwa familia. Katika 2 Timotheo 3:2, 3 Biblia ilitabiri kwamba watu wengi hawangekuwa “na upendo wa asili” kuelekea familia yao na watoto wangekuwa “wasiotii wazazi.”

 Upendo wa wengi kumwelekea Mungu ungepungua. Yesu alitabiri: “Upendo wa wengi utapoa.” (Mathayo 24:12) Yesu alimaanisha kwamba upendo wa watu wengi kumwelekea Mungu ungepoa. Vilevile, 2 Timotheo 3:4, inasema kwamba katika siku za mwisho, watu hao wangekuwa “wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.”

 Unafiki wa kidini. Katika 2 Timotheo 3:5, Biblia ilitabiri kwamba watu wangedai wanamwabudu Mungu lakini kihalisi hawangeishi kulingana na viwango vyake.

 Kuongezeka kwa uelewaji wa unabii wa Biblia. Kitabu cha Danieli kilitabiri kwamba katika “wakati wa mwisho,” watu wengi wangeweza kupata ujuzi mwingi wa kweli za Biblia, kutia ndani kuelewa unabii unaohusiana na siku za mwisho.​—Danieli 12:4.

 Kazi ya kuhubiri inayofanywa ulimwenguni pote. Yesu alitabiri: “Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.”​—Mathayo 24:14.

 Kuongezeka kwa kutojali na dhihaka. Yesu alitabiri kwamba watu wengi wangepuuza uthibitisho ulio wazi kwamba mwisho unakaribia. (Mathayo 24:37-39) Isitoshe, 2 Petro 3:3, 4 ilitabiri kwamba baadhi ya watu wangedhihaki uthibitisho huo na kuupuuza kabisa.

 Unabii wote watimia. Yesu alisema kwamba unabii wote huo ungetimia kwa wakati uleule katika siku za mwisho, si mambo machache tu, bali unabii wote.​—Mathayo 24:33.

Je, tunaishi katika “siku za mwisho”?

 Ndiyo. Hali za ulimwenguni na pia mfuatano wa matukio katika Biblia unaonyesha kwamba siku za mwisho zilianza mwaka wa 1914, Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipoanza. Ili kuona jinsi hali za ulimwengu zinavyothibitisha kwamba tunaishi katika siku za mwisho, tazama video ifuatayo:

 Mwaka wa 1914, Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mbinguni, na jambo la kwanza ulilofanya ni kumfukuza Shetani Ibilisi na roho waovu kutoka mbinguni na kuwazuilia duniani. (Ufunuo 12:7-12) Uvutano wa Shetani juu ya wanadamu unaonekana wazi kupitia mitazamo mibaya na mambo mabaya wanayotenda na hivyo kufanya siku za mwisho ziwe “hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”​—2 Timotheo 3:1.

 Watu wengi wanafadhaishwa na siku hizi ngumu. Wana wasiwasi kwamba jamii inaendelea kuzorota. Wengine hata wanahofia kwamba wanadamu wataangamizana.

 Hata hivyo, wengine ambao wanahangaishwa na hali za ulimwengu wana tumaini kwa ajili ya wakati ujao. Wana hakika kwamba Ufalme wa Mungu utachukua hatua ili kukomesha matatizo ulimwenguni. (Danieli 2:44; Ufunuo 21:3, 4) Wanasubiri kwa hamu Mungu atimize ahadi zake na wanapata faraja katika maneno haya ya Yesu: “Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”​—Mathayo 24:13; Mika 7:7.