Kwa Waroma 6:1-23

  • Uhai mpya kupitia ubatizo katika Kristo (1-11)

  • Msiache dhambi itawale katika miili yenu (12-14)

  • Kuacha utumwa wa dhambi na kuwa watumwa wa Mungu (15-23)

    • Mshahara wa dhambi​—⁠kifo; Zawadi ya Mungu​—⁠uzima (23)

6  Basi tuseme nini? Je, tuendelee kuwa katika dhambi, ili fadhili zisizostahiliwa ziongezeke?  La hasha! Kwa kuwa tulikufa kuhusiana na dhambi,+ tunawezaje kuendelea kuishi tena katika dhambi?+  Au je, hamjui kwamba sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu+ tulibatizwa katika kifo chake?+  Basi tulizikwa pamoja naye kupitia ubatizo wetu katika kifo chake,+ ili kama vile Kristo alivyofufuliwa kutoka kwa wafu kupitia utukufu wa Baba, vivyo hivyo sisi pia tunapaswa tutembee katika hali mpya ya uzima.+  Ikiwa tumeungana pamoja naye katika mfano wa kifo chake,+ hakika sisi pia tutaunganishwa pamoja naye katika mfano wa ufufuo wake.+  Kwa maana tunajua kwamba utu wetu wa zamani ulitundikwa mtini pamoja naye,+ ili mwili wetu wenye dhambi usiwe na nguvu,+ ili tusiendelee kuwa watumwa wa dhambi.+  Kwa maana yule ambaye amekufa ameondolewa* hatia ya dhambi yake.  Isitoshe, ikiwa tumekufa pamoja na Kristo, tunaamini kwamba tutaishi pia pamoja naye.  Kwa maana tunajua kwamba Kristo, kwa kuwa sasa amefufuliwa kutoka kwa wafu,+ hatakufa tena;+ kifo si bwana juu yake tena. 10  Kwa maana kifo alichokufa, alikufa kuhusiana na dhambi* mara moja kwa wakati wote,+ lakini uhai anaoishi, anaishi kuhusiana na Mungu. 11  Vivyo hivyo ninyi, mjihesabu kuwa wafu kuhusiana na dhambi lakini walio hai kuhusiana na Mungu kupitia Kristo Yesu.+ 12  Kwa hiyo, msiruhusu dhambi iendelee kutawala kama mfalme katika miili yenu inayoweza kufa+ hivi kwamba mzitii tamaa zake. 13  Wala msiendelee kuitoa miili yenu* kwa dhambi kuwa silaha za ukosefu wa uadilifu, bali jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai kutoka kwa wafu, pia toeni miili yenu* kwa Mungu kuwa silaha za uadilifu.+ 14  Kwa maana dhambi haipaswi kuwa bwana juu yenu, kwa kuwa ninyi hamko chini ya sheria+ bali chini ya fadhili zisizostahiliwa.+ 15  Tuseme nini basi? Je, tufanye dhambi kwa sababu hatuko chini ya sheria bali chini ya fadhili zisizostahiliwa?+ La hasha! 16  Je, hamjui kwamba mkijitoa kwa yeyote kuwa watumwa watiifu, ninyi ni watumwa wa yule mnayemtii,+ ama watumwa wa dhambi+ inayotokeza kifo+ au wa utii unaotokeza uadilifu? 17  Lakini shukrani kwa Mungu kwamba ingawa wakati fulani mlikuwa watumwa wa dhambi, sasa mmekuwa watiifu kutoka moyoni kwa kielelezo cha fundisho mlilokabidhiwa. 18  Ndiyo, kwa kuwa mliwekwa huru kutoka katika dhambi,+ mmekuwa watumwa wa uadilifu.+ 19  Ninazungumza kwa maneno ya kibinadamu kwa sababu ya udhaifu wa miili yenu; kwa maana kama mlivyovitoa viungo vyenu kuwa watumwa wa mambo machafu na uasi sheria unaotokeza uasi sheria, basi sasa vitoeni viungo vyenu viwe watumwa wa uadilifu unaotokeza utakatifu.+ 20  Kwa maana mlipokuwa watumwa wa dhambi, mlikuwa huru kuhusiana na uadilifu. 21  Basi, mlikuwa mkizaa matunda gani wakati huo? Mambo ambayo sasa mnayaonea aibu. Kwa maana mwisho wa mambo hayo ni kifo.+ 22  Hata hivyo, sasa, kwa vile mliwekwa huru kutoka katika dhambi na kuwa watumwa wa Mungu, mnazaa matunda katika utakatifu,+ na mwisho ni uzima wa milele.+ 23  Kwa maana mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,+ lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele+ kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.+

Maelezo ya Chini

Au “amefunguliwa; amesamehewa.”
Yaani, kuondoa dhambi.
Tnn., “viungo vyenu.”
Tnn., “viungo vyenu.”