Hamia kwenye habari

Yerusalemu Jipya Ni Nini?

Yerusalemu Jipya Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Maneno “Yerusalemu Jipya,” yanayopatikana mara mbili katika Biblia, ni jiji la mfano linalowakilisha kikundi cha wafuasi wa Yesu ambao wanaenda mbinguni kutawala pamoja naye katika Ufalme wa Mungu. (Ufunuo 3:12; 21:2) Biblia inaonyesha kwamba kikundi hicho kinaweza pia kuitwa bibi harusi wa Kristo.

Mambo yanayotusaidia kutambulisha Yerusalemu Jipya

  1.   Yerusalemu Jipya liko mbinguni. Kila wakati ambapo Biblia inataja Yerusalemu Jipya, inaonyesha kwamba jiji hilo linashuka kutoka mbinguni, ambako malaika wanalinda malango ya jiji hilo. (Ufunuo 3:12; 21:2, 10, 12) Pia, ukubwa wa jiji hilo unaonyesha kwamba haliwezi kuwa duniani. Jiji hilo lina umbo la mraba wenye ukubwa wa “stadia 12,000” au kilomita 2,200 hivi. a (Ufunuo 21:16) Hilo linamaanisha kwamba kila upande ungekuwa umeinuka kwa kimo cha kilomita 560 hivi angani.

  2.   Yerusalemu Jipya limefanyizwa na kikundi cha wafuasi wa Yesu, bibi harusi wa Kristo. Yerusalemu Jipya linaitwa “bibi harusi, mke wa Mwanakondoo.” (Ufunuo 21:9, 10) Katika ufafanuzi huo wa mfano, Mwanakondoo anawakilisha Yesu Kristo. (Yohana 1:29; Ufunuo 5:12) “Mke wa Mwanakondoo,” bibi harusi wa Kristo, anawakilisha Wakristo watakaounganishwa na Yesu mbinguni. Biblia inalinganisha uhusiano uliopo kati ya Yesu na Wakristo hao na ule wa mume na mke. (2 Wakorintho 11:2; Waefeso 5:23-25) Isitoshe, mawe ya msingi ya Yerusalemu Jipya yameandikwa “majina 12 ya mitume 12 wa Mwanakondoo.” (Ufunuo 21:14) Habari hiyo inatusaidia kuthibitisha utambulisho wa Yerusalemu Jipya, kwa kuwa Wakristo wanaoenda kuishi mbinguni ‘wamejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii.’​—Waefeso 2:20.

  3.   Yerusalemu Jipya ni sehemu ya serikali. Yerusalemu la kale lilikuwa mji mkuu wa Israeli, mahali ambapo Mfalme Daudi, mwana wake Sulemani, na wazao wao walitawala wakiwa wameketi “kwenye kiti cha ufalme cha Yehova.” (1 Mambo ya Nyakati 29:23) Hivyo, Yerusalemu, ambalo liliitwa “jiji takatifu,” liliwakilisha utawala wa Mungu kupitia ukoo wa Daudi. (Nehemia 11:1) Vivyo hivyo, Yerusalemu Jipya, ambalo pia linaitwa “jiji takatifu,” limefanyizwa kwa wale wanaojiunga na Yesu mbinguni ‘kutawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’​—Ufunuo 5:9, 10; 21:2.

  4.   Yerusalemu Jipya linawaletea baraka watu walio duniani. Yerusalemu Jipya linaonyeshwa “likishuka kutoka mbinguni kwa Mungu,” jambo linaloonyesha kwamba Mungu atalitumia kubadili mambo nje ya mbinguni. (Ufunuo 21:2) Maneno hayo yanahusianisha Yerusalemu Jipya na Ufalme wa Mungu ambao Mungu hutumia kutimiza kusudi lake “duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Kusudi la Mungu kwa watu wanaoishi duniani linatia ndani baraka zifuatazo:

    •   Kuondolewa kwa dhambi. “Mto wa maji ya uzima” unatiririka kutoka Yerusalemu Jipya na kumimina maji yake kwenye “miti ya uzima” ambayo matunda yake yamekusudiwa “kuponya mataifa.” (Ufunuo 22:1, 2) Uponyaji huo wa kimwili na kiroho utaondoa dhambi na kuwawezesha watu kupata uhai mkamilifu, kama Mungu alivyokusudia awali.​—Waroma 8:21.

    •   Uhusiano mzuri kati ya Mungu na wanadamu. Dhambi imetufanya tutenganishwe na Mungu. (Isaya 59:2) Kuondolewa kwa dhambi kutafanya unabii huu utimie kikamili: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao.”​—Ufunuo 21:3.

    •   Watu hawatateseka tena wala kufa. Kupitia kwa Ufalme wake, Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”​—Ufunuo 21:4.

a Stadia kilikuwa kipimo kilichotumiwa na Waroma kinacholingana na mita 185.