Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 2

Jinsi ya Kuwa Mnyenyekevu

Jinsi ya Kuwa Mnyenyekevu

MAANA YA KUWA MNYENYEKEVU

Watu wanyenyekevu huwaheshimu wengine. Hawana majivuno wala hawatazamii kutendewa kwa njia ya pekee. Wao hupendezwa kikweli na wengine na wako tayari kujifunza kutoka kwao.

Nyakati fulani, unyenyekevu huonekana kama udhaifu. Lakini ukweli ni kwamba, sifa hiyo humwezesha mtu kutambua upungufu wake na mambo asiyoweza kutimiza.

KWA NINI UNYENYEKEVU NI MUHIMU?

  • Unyenyekevu husaidia kuwa na uhusiano mzuri na wengine. “Kwa ujumla watu wanyenyekevu huanzisha urafiki kwa urahisi zaidi.” Vilevile “ni rahisi kwao kuelewana na kushirikiana na watu wa namna zote.”​—Kitabu The Narcissism Epidemic.

  • Unyenyekevu utamsaidia mtoto wako atakapokuwa mtu mzima. Mtoto wako akijifunza kuwa mnyenyekevu, atanufaika sasa na wakati ujao. Kwa mfano, sifa hiyo itamsaidia anapotafuta kazi. Dakt. Leonard Sax aliandika hivi: “Ni vigumu sana kwa kijana mwenye kiburi na ambaye hatambui udhaifu wake kufanikiwa kwenye mahojiano ya kazi. Lakini inaelekea kwamba kijana ambaye kweli anatamani kujua kile ambacho mwajiri anatazamia, ataajiriwa.” *

JINSI YA KUMZOEZA MTOTO KUWA MNYENYEKEVU

Msaidie mtoto wako ajione kuwa mtu wa kawaida.

KANUNI YA BIBLIA: “Mtu akifikiri yeye ni kitu wakati yeye si kitu, anajidanganya mwenyewe.”​—Wagalatia 6:3.

  • Epuka kutumia misemo inayopotosha. Misemo kama “Ndoto zako zote zitatimia” na “Unaweza kutimiza chochote unachotaka” inaweza kuonekana kuwa yenye kutia moyo, lakini mara nyingi mambo huwa hayaendi hivyo. Kuna uwezekano mkubwa kwamba mtoto wako atafanikiwa ikiwa atajiwekea malengo ya kawaida, na kujitahidi kuyafikia.

  • Unapompongeza mtoto wako, taja mambo hususa. Kumsifia tu mtoto hakutamsaidia kuwa mnyenyekevu. Mwambie kihususa kile kilichokupendeza.

  • Usimruhusu mtoto wako atumie sana mitandao ya kijamii. Kwa kawaida kwenye mitandao ya kijamii, watu hujivuna na kujisifia kwa sababu ya uwezo wao na mambo wanayotimiza. Hivyo sivyo unyenyekevu ulivyo.

  • Mzoeze mtoto wako kuomba msamaha upesi. Msaidie mtoto wako kutambua makosa yake na kuyakubali.

Msaidie awe mwenye shukrani.

KANUNI YA BIBLIA: “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani.”​—Wakolosai 3:15.

  • Kuuthamini uumbaji. Watoto wanapaswa kuuthamini uumbaji na kuelewa jinsi ambavyo tunautegemea ili tuendelee kuishi. Tunahitaji hewa, maji, na chakula. Tumia mifano kama hiyo kumsaidia mtoto wako athamini na kuvutiwa na vitu vyote vyenye kupendeza na kustaajabisha, vilivyoumbwa na Mungu.

  • Kuwathamini watu. Mkumbushe mtoto wako kwamba, kwa njia moja au nyingine, kila mtu anamzidi kitu fulani, na hivyo badala ya kuwaonea wivu wengine kwa sababu ya ustadi na uwezo wao, anapaswa kujifunza kutoka kwao.

  • Kuonyesha shukrani. Wafundishe watoto wako kusema asante​—“asante” inayotoka moyoni. Kuwa na roho ya shukrani ni msingi wa unyenyekevu.

Msaidie mtoto wako kuona thamani ya kuwatumikia wengine.

KANUNI YA BIBLIA: “Kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi, huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.”​—Wafilipi 2:3, 4.

  • Mpangie mtoto wako kazi za nyumbani. Kutompa mtoto kazi za nyumbani, ni kama kumwambia, ‘Mambo yako ni muhimu zaidi!’ Kazi za nyumbani zinapaswa kufanywa kwanza, halafu kucheza baadaye. Msaidie aone jinsi ambavyo kazi za nyumbani huwanufaisha wengine na jinsi watakavyothamini na kumheshimu kwa kuzifanya.

  • Mchochee athamini kuwatumikia wengine. Kufanya hivyo kutamsaidia akomae kiakili. Kwa hiyo, mzoeze mtoto wako kutambua watu wenye uhitaji. Halafu kwa pamoja, zungumzieni jinsi ya kuwasaidia. Muunge mkono na umpongeze anapowatumikia wengine.

^ fu. 8 Maelezo hayo yametolewa kwenye kitabu, The Collapse of Parenting.