Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Kuwafundisha Watoto Unyenyekevu

Kuwafundisha Watoto Unyenyekevu

CHANGAMOTO

  • Mtoto wako ni mwenye kiburi licha ya kwamba ana umri wa miaka kumi tu!

  • Anatarajia kila mtu amtendee kwa njia ya pekee.

Unajiuliza, ‘Kwa nini anajiendesha kwa njia hii? Ningependa ahisi ana thamani lakini asijione kuwa bora kuliko watu wengine!’

Je, mtoto anaweza kufundishwa unyenyekevu bila kumfanya ajione hafai au hana thamani?

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Katika miaka ya karibuni, wazazi wamehimizwa kuwapatia watoto wao kila kitu wanachotaka; kuwasifu sana, hata ikiwa hawajafanya chochote kinachostahili kusifiwa; kutowarekebisha na kutowatia nidhamu. Wengi walidhani kwamba watoto wangeweza kuwa na maoni yanayofaa kuhusu thamani yao ikiwa wangechochewa kujiona kuwa wa pekee. Lakini matokeo yamefunua nini? Kitabu kimoja (Generation Me) kinasema hivi: “Badala ya kuwasaidia watoto wawe na tabia nzuri na wenye furaha, harakati za kuwafanya watoto wajiamini zimetokeza kundi kubwa la watoto wenye ubinafsi.”

Watoto wengi ambao wamezoea kusifiwa kupita kiasi, wanapokuwa watu wazima wanashindwa kutenda kwa njia inayofaa wanapokatishwa tamaa, wanapokosolewa, au wanapokosea. Kwa kuwa wamefundishwa kukazia fikira mapendezi yao wenyewe, wanashindwa kujenga mahusiano yanayodumu pamoja na wengine. Matokeo ni kwamba wengi wao wanashuka moyo na kuwa watu wenye wasiwasi.

Watoto hutambua thamani yao kikweli, si kwa kuambiwa mara kwa mara kwamba wao ni bora, bali kwa kutimiza mambo hususa. Ili wafanye hivyo, mengi yanahusika zaidi tu ya kujiamini. Wanahitaji kujifunza, kujizoeza, na kuboresha kwa makini stadi hususa. (Methali 22:29) Wanapaswa pia kujali mahitaji ya watu wengine. (1 Wakorintho 10:24) Yote hayo yanahitaji unyenyekevu.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Mpongeze mtoto ikiwa tu anastahili. Binti yako akifaulu mtihani, mpongeze. Ikiwa amepata alama za chini, usikimbilie kumlaumu mwalimu. Kufanya hivyo hakutamsaidia ajifunze unyenyekevu. Badala yake, mfundishe jinsi anavyoweza kupata matokeo mazuri wakati ujao. Mpongeze tu anapotimiza jambo hususa.

Mrekebishe kila inapohitajika. Hii haimaanishi kwamba unapaswa kumkosoa mtoto wako kila anapokosea. (Wakolosai 3:​21) Hata hivyo, anapofanya makosa mazito anahitaji kurekebishwa. Unapaswa kufanya vivyo hivyo ikiwa anaonyesha mtazamo mbaya. Usipomrekebisha, mambo hayo yatakita mizizi.

Kwa mfano, tuseme mtoto wako ana mwelekeo wa kujisifu. Asiporekebishwa, atakuwa mwenye kiburi na kuanza kuwatenga wengine. Kwa hiyo mweleze kwamba kujisifu kunafanya aonekane kuwa mtu mbaya na huenda kukasababisha aaibike. (Methali 27:2) Mweleze pia kwamba mtu mwenye maoni yenye usawaziko kujihusu haoni uhitaji wa kuwatangazia watu uwezo wake. Ukifanya hivyo kwa upendo, utamfundisha unyenyekevu kwa njia ambayo haitamfanya ajihisi hafai.​—Kanuni ya Biblia: Mathayo 23:12.

Mwandae mtoto wako kwa ajili ya changamoto za maisha. Kumpa mtoto wako kila kitu anachotaka kunaweza kufanya ahisi ni haki yake kupata vitu hivyo. Kwa mfano, ikiwa mtoto wako anataka kitu ambacho hauna uwezo wa kukinunua, mweleze umuhimu wa kuishi kulingana na bajeti. Ikiwa itabidi kuahirisha likizo au tafrija, unaweza kumweleza kwamba ni kawaida kukatishwa tamaa maishani na kumwonyesha jinsi ambavyo wewe hukabiliana na hali kama hizo. Badala ya kuwakinga watoto wako kutokana na magumu yote ya maisha, waandae kwa ajili ya changamoto watakazokabili watakapokuwa watu wazima.​—Kanuni ya Biblia: Methali 29:21.

Mchochee kuwa mkarimu. Mthibitishie mtoto wako kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Jinsi gani? Mkiwa pamoja, mnaweza kuandika orodha ya watu wanaohitaji kusaidiwa kufanya ununuzi, marekebisho mbalimbali, au wanaohitaji usafiri. Kisha nenda naye unapowasaidia baadhi ya watu hao. Acha mtoto wako aone furaha na uradhi unaopata unaposhughulikia mahitaji ya wengine. Ukifanya hivyo, utamfundisha unyenyekevu kupitia mfano wako, ambayo ndiyo njia bora zaidi ya kufundisha.​—Kanuni ya Biblia: Luka 6:38.