Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kuonyesha Uthamini

Jinsi ya Kuonyesha Uthamini

CHANGAMOTO

Ili ndoa ifanikiwe, ni muhimu kila mmoja aonyeshe kwamba anamthamini mwenzake. Hata hivyo, wenzi wengi wa ndoa hawaoni sifa nzuri za mume au mke waliye naye, kwa hiyo hawazithamini. Katika kitabu Emotional Infidelity, mshauri mmoja anasema kwamba, wenzi wengi wanaoenda kumwona “wanakazia fikira zaidi mambo ambayo wanakosa [katika ndoa zao] kuliko yale wanayopata. Wanakuja ofisini kwangu kuniambia yale wanayotaka yabadilike na si mambo wanayotaka yabaki kama yalivyo. Kosa ambalo kila mmoja wa wenzi hao hufanya ni kushindwa kuonyesha upendo kwa kuwa mwenye uthamini.”

Wewe na mwenzi wako mnaweza kufanya nini ili kuepuka mtego huo?

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Kuonyeshana uthamini kunaweza kupunguza mkazo katika ndoa. Mume na mke wanapojitahidi kutambua na kuonyesha wanathamini sifa nzuri za mwenzi wao, uhusiano wao utasitawi. Mkazo, hata uwe mkubwa namna gani, unaweza kupungua ikiwa kila mmoja anahisi kwamba mwenzi wake anamthamini.

Kwa wake. Kitabu Emotional Infidelity kinasema kwamba, “kwa kawaida wanawake wengi hawatambui mkazo mkubwa ambao wanaume hukabili wanapojitahidi kuandaa mahitaji ya familia zao.” Katika maeneo mengine, mkazo huo unaweza kuwepo hata kwa familia zinazotegemea kipato cha mume na mke.

Kwa waume. Mara nyingi waume hawathamini jitihada za wake zao katika familia, kama vile kutafuta pesa, kulea watoto, au kufanya kazi za nyumbani. Fiona, * ambaye ameolewa kwa karibu miaka mitatu, anasema hivi: “Kila mtu hukosea, na ninapokosea, mimi huhisi vibaya sana. Hivyo, mume wangu anaponipongeza kwa kufanya jambo fulani vizuri, labda kuhusu kazi za nyumbani, ninatambua kwamba bado ananipenda licha ya kasoro zangu. Pia, ninahisi ananiunga mkono na ninafurahia zaidi kile ninachotimiza!”

Kinyume cha hilo, uaminifu katika ndoa unaweza kuwa hatarini ikiwa mwenzi mmoja anahisi hathaminiwi. Mke fulani anayeitwa Valerie, anasema hivi: “Unapohisi kwamba mwenzi wako hakuthamini, ni rahisi kuanza kuvutiwa na mtu anayekufanya uhisi unathaminiwa.”

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Uwe macho. Katika juma linalokuja, jitahidi kuona sifa nzuri ambazo mwenzi wako ataonyesha. Pia, uwe macho kuona yale ambayo mwenzi wako anafanya ili kuhakikisha hali ya familia inaendelea kuwa nzuri, mambo ambayo huenda hukuyathamini hapo awali. Mwishoni mwa juma, orodhesha (1) sifa za mwenzi wako unazothamini na (2) mambo ambayo alifanya kwa manufaa ya familia.—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 4:8.

Kwa nini ni muhimu kuwa macho? Mke fulani anayeitwa Erika anasema hivi: “Miaka michache inapopita baada ya kufunga ndoa, uthamini kumwelekea mwenzi wako unaweza kuanza kupungua. Unaacha kuona mambo mazuri anayotimiza, na kuanza kukazia fikira zaidi mambo ambayo hafanyi.”

Jiulize hivi: ‘Je, mimi huthamini mambo ambayo mwenzi wangu hufanya?’ Kwa mfano, mume wako anaporekebisha baadhi ya vifaa vya nyumbani, je, unajiambia kwamba huo ni wajibu wake na hivyo hakuna haja ya kumshukuru kwa kile alichofanya? Ikiwa wewe ni mume, je, unahisi kwamba hakuna sababu ya kuonyesha uthamini wowote kuelekea kazi ya kulea watoto ambayo mke wako anafanya, eti kwa kuwa huo ni wajibu wake? Uwe na lengo la kuona na kuthamini jambo lolote ambalo mwenzi wako anafanya kwa ajili ya familia, liwe dogo au kubwa.—Kanuni ya Biblia: Waroma 12:10.

Mpongeze mwenzi wako. Biblia haituambii tu kwamba tuwe wenye shukrani, badala yake inasema tunapaswa [Kujionyesha] kuwa wenye shukrani.” (Wakolosai 3:15) Kwa hiyo, uwe na mazoea ya kumshukuru mwenzi wako. Mume fulani anayeitwa James anasema: “Mke wangu anaponishukuru kwa yale ninayofanya, ninachochewa kujitahidi hata zaidi kuwa mume mzuri na kuongeza bidii yangu katika kuboresha ndoa yetu.”—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 4:6.

Kwa kweli, wenzi wa ndoa ambao huonyeshana kwamba wanathaminiana, huwa na uhusiano imara. Mume fulani anayeitwa Michael anasema hivi: “Ninaamini kwamba ndoa nyingi zingeokolewa ikiwa kila mmoja angekazia sifa anazopenda kutoka kwa mwenzi wake. Matatizo yanapotokea, haitakuwa rahisi kwao kufikiria kuvunja ndoa kwa kuwa watakumbuka thamani ya kile walicho nacho.”

^ fu. 9 Baadhi ya majina yamebadilishwa.