Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mafundisho ya Muumba Wetu Hutupatia Tumaini la Maisha Bora

Mafundisho ya Muumba Wetu Hutupatia Tumaini la Maisha Bora

Mungu ameahidi kwamba hivi karibuni kutakuwa na mabadiliko duniani. Ataondoa kuteseka na kufanya maisha duniani yawe yenye kufurahisha kwa kila mwanadamu. (Zaburi 37:11) Kwa nini uamini ahadi hii? Kwa sababu “Mungu si mwanadamu anayesema uwongo.” (Hesabu 23:19) Fikiria baadhi ya mambo mazuri ambayo Muumba wetu atafanya.

Mungu Atawaangamiza Watu Waovu

“Waovu wanapochipuka kama magugu na watenda mabaya wote wanapositawi, ni ili waangamizwe milele.”​​—ZABURI 92:7.

Kama tulivyoona kwenye makala iliyotangulia, mambo mabaya yanazidi kuongezeka. Hili halipaswi kutushangaza. Biblia ilitabiri kwenye 2 Timotheo 3:1-5 kwamba katika “siku za mwisho” watu wangekuwa wabaya sana. Siku za mwisho za nini? Za ulimwengu huu wa watu wasiomwogopa Mungu. Hivi karibuni, Mungu atawaangamiza wale wanaokataa kuacha mambo mabaya. Kisha, watu wazuri tu—wale wanaomtii Mungu—ndio watakaobaki duniani. “Waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.”​—Zaburi 37:29.

Mungu Atamwangamiza Shetani

“Mungu anayetoa amani atamponda Shetani.”​​—WAROMA 16:20.

Waovu wote wakiondolewa kutia ndani Shetani na roho waovu, amani itaenea duniani pote. Muumba wetu anaahidi hivi: “Hakuna yeyote [atakayekuogopesha].”—Mika 4:4.

Mungu Atakomesha Magonjwa na Kifo

“Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”​​—UFUNUO 21:3, 4.

Kuteseka na magonjwa yatakwisha kwa sababu Mungu ataondoa madhara yote yaliyosababishwa na Shetani, Adamu, Hawa, na hali yetu ya kutokuwa wakamilifu. Matokeo ni kwamba, hata “kifo hakitakuwapo tena.” Wanadamu wanaompenda na kumtii Muumba wetu wataishi milele. Lakini, wataishi wapi?

Muumba Wetu Atafanya Dunia Iwe Paradiso

“Nyika na nchi iliyokauka zitafurahi, na jangwa tambarare litashangilia na kuchanua maua kama zafarani.”​​—ISAYA 35:1.

Mungu atawaondoa waovu na dunia itakuwa paradiso! Kutakuwa na bustani nyingi maridadi na zenye kuvutia, na dunia itazalisha chakula kingi sana. (Zaburi 72:16) Maji ya bahari, maziwa, na mito yatakuwa safi na yatajaa viumbe hai. Hata tutasahau kabisa maneno kama vile, “uchafuzi wa mazingira!” Kila mtu atajenga nyumba na kuishi ndani yake. Na hakuna mtu yeyote atakayekosa makao, atakayekuwa na njaa, au kuwa maskini.​—Isaya 65:21, 22.

Mungu Atawafufua Watu Waliokufa

“Kutakuwa na ufufuo.”​​—MATENDO 24:15.

Je, ungependa kuwaona tena wapendwa wako waliokufa? Mungu mweza-yote atawarudishia uhai​—atawafufua—​waishi kwenye dunia Paradiso. Utawatambua, nao watakutambua pia. Wazia furaha mtakayokuwa nayo! Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba kutakuwa na ufufuo? Kwa sababu Biblia ina mifano ya watu wazima na watoto ambao walifufuliwa, nao walijiunga tena na familia zao. Zaidi ya hayo, mara nyingi Yesu aliwafufua watu waliokufa mbele za watu wengi.​—Luka 8:49-56; Yohana 11:11-14, 38-44