Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hekima Inayotusaidia Kuwa na Maisha ya Familia Yenye Furaha

Hekima Inayotusaidia Kuwa na Maisha ya Familia Yenye Furaha

Ndoa na watoto ni zawadi bora kutoka kwa Muumba wetu. Anataka tuwe na familia zenye furaha. Hivyo, kupitia kitabu chake kitakatifu kilichoandikwa zamani, ametupatia mwongozo wa kuwa na maisha bora ya familia na yenye furaha. Fikiria ushauri ufuatao wenye hekima.

Waume, Wapendeni Wake Zenu

“Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Mwanamume anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza.”​​—WAEFESO 5:28, 29.

Mume ni kichwa cha familia. (Waefeso 5:23) Lakini mume bora si mkali au mwenye kudai mengi. Anamthamini mke wake na kumwandalia mahitaji ya kimwili na ya kihisia. Pia, anajitahidi kumfurahisha mke wake, na hang’ang’anii kufanya mambo anayotaka yeye tu. (Wafilipi 2:4) Mume bora anamweleza mke wake waziwazi hisia zake na mawazo yake na anamsikiliza mke wake anapozungumza. Hamkasirikii kwa uchungu au kumuumiza kimwili au kihisia.​—Wakolosai 3:19.

Wake, Waheshimuni Waume Zenu

“Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”​​—WAEFESO 5:33.

Mke anapomheshimu mume wake na kumuunga mkono, anasaidia familia iwe na amani. Mume wake akikosea, hamdharau, bali anaendelea kuwa mpole na mwenye heshima. (1 Petro 3:4) Ikiwa atahitaji kuzungumza na mume wake kuhusu tatizo fulani, atachagua wakati unaofaa na atazungumza naye kwa heshima.—Mhubiri 3:7.

Uwe Mwaminifu kwa Mwenzi Wako

“Mwanamume . . . atashikamana na mke wake, nao watakuwa mwili mmoja.”​​—MWANZO 2:24.

Mwanamume na mwanamke wanapooana, wanaanzisha uhusiano wa karibu sana. Hivyo, kila mmoja wao anapaswa kujitahidi kuimarisha ndoa yao kwa kuzungumza kutoka moyoni na kutendeana matendo madogo-madogo ya fadhili. Na pia wanapaswa kuwa waaminifu kwenye ndoa yao kwa kutokuwa na mahusiano ya kingono nje ya ndoa. Usaliti ni ukatili. Unafanya wenzi wa ndoa wasiaminiane na unaweza kuvunja familia.—Waebrania 13:4.

Wazazi, Wazoezeni Watoto Wenu

“Mzoeze mtoto njia anayopaswa kuifuata; hata atakapozeeka hataiacha.”​​—METHALI 22:6, maelezo ya chini.

Mungu amewapa wazazi jukumu la kuwazoeza watoto wao. Hilo linatia ndani kuwafundisha wawe na tabia nzuri na kuwawekea mfano bora. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Mtoto anapokosea, mzazi mwenye hekima hatakasirika kupita kiasi. Atakuwa “mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa hasira.” (Yakobo 1:19) Ikiwa mzazi ataamua kwamba mtoto wake anahitaji kuadhibiwa, atamwadhibu kwa upendo si kwa hasira.

Watoto, Watiini Wazazi Wenu

“Watoto, watiini wazazi wenu . . . ‘Mheshimu baba yako na mama yako.’”​​—WAEFESO 6:1, 2.

Watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao na kuwaheshimu sana. Watoto wanapowaheshimu wazazi wao wanafanya familia iwe na furaha na wanachangia amani na umoja katika familia. Watoto ambao ni watu wazima wanawaheshimu wazazi wao kwa kuhakikisha kwamba wanawatunza vizuri. Hilo linatia ndani kuwasaidia kutunza nyumba na kuwapa msaada wa kifedha inapohitajika.​—1 Timotheo 5:3, 4.