Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwongozo wa Kutusaidia Kuwa na Uhusiano Mzuri na Wengine

Mwongozo wa Kutusaidia Kuwa na Uhusiano Mzuri na Wengine

Muumba wetu anatueleza jinsi tunavyoweza kuwa na uhusiano mzuri na watu wengine, iwe ni nyumbani, kazini, au na marafiki. Fikiria baadhi ya ushauri wa hekima ambao watu wengi wametumia na kufanikiwa.

Uwe Mwenye Kusamehe

“Endeleeni . . . kusameheana kwa hiari hata ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”​​—WAKOLOSAI 3:13.

Sisi sote hufanya makosa. Tunaweza kuwaudhi wengine, nao wanaweza kutuudhi pia. Vyovyote vile, tunahitaji kuwasamehe na tungependa watusamehe pia. Tunaposamehe, tunaacha kuwa na kinyongo kumwelekea mtu aliyetukosea. Hatumlipi mtu aliyetukosea “uovu kwa uovu,” na hatumkumbushi mara kwa mara kuhusu mambo aliyotukosea au udhaifu wake. (Waroma 12:17) Lakini namna gani ikiwa mtu fulani ametuumiza sana na hatuwezi kuacha kufikiria jambo hilo? Ikiwa hali iko hivyo, kwa heshima, zungumza na mtu aliyekukosea faraghani. Tunapaswa kuwa na lengo la kufanya amani na si kutafuta ni nani aliyekosea.​—Waroma 12:18.

Uwe Mnyenyekevu na Mwenye Heshima

“Kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi.”​​—WAFILIPI 2:3.

Tukiwa wanyenyekevu na wenye heshima, watu watafurahia kuwa pamoja nasi. Wanajua kwamba tutawatendea kwa fadhili na kuwajali na hatutaumiza hisia zao kimakusudi. Hata hivyo, ikiwa tutajiona sisi kuwa bora kuliko wengine au sikuzote tukisisitiza kwamba njia yetu ya kufanya mambo ndiyo bora, tutasababisha migogoro na mikazo. Ikiwa tutakuwa na tabia hizo, watu watatuepuka na tutakuwa na marafiki wachache, au hatutakuwa na marafiki kabisa.

Usiwe na Ubaguzi

“Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.”​​—MATENDO 10:34, 35.

Muumba wetu hawabagui watu kwa sababu ya taifa lao, lugha yao, hadhi yao katika jamii, au rangi yao. “Alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja.” (Matendo 17:26) Kwa sababu hiyo, wanadamu wote ni ndugu na dada. Tukiwatendea wengine kwa heshima na fadhili, tutawafanya wawe na furaha, nasi tutakuwa na furaha na kumpendeza Muumba wetu.

Uwe Mpole

“Jivikeni. . . upole.”​—WAKOLOSAI 3:12.

Tukiwa wapole, tutafanya wengine wahisi vizuri. Watajihisi huru kuzungumza nasi na hata kuturekebisha kwa sababu wanajua hatutakasirika. Na mtu akitukasirikia, jibu letu la upole linaweza kumtuliza. Methali 15:1 inasema hivi: “Jibu la upole hutuliza hasira, lakini neno kali huchochea hasira.”

Uwe Mkarimu na Mwenye Shukrani

“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​​—MATENDO 20:35.

Watu wengi leo wana pupa na wanajifikiria wenyewe tu. Lakini watu wakarimu huwa na furaha ya kweli. (Luka 6:38) Watu wakarimu wana furaha kwa sababu wanawapenda watu kuliko vitu. Upendo huo unawachochea kuwa wenye shukrani na wanaonyesha hilo wanapotendewa kwa ukarimu na watu wengine. (Wakolosai 3:15) Jiulize hivi, ‘Ningependa kushirikiana na mtu wa aina gani​—mchoyo na asiye na shukrani au mtu mkarimu na mwenye shukrani?’ Jambo kuu ni hili: Watendee wengine mambo unayotaka wakutendee wewe.​—Mathayo 7:12.