Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tabia Pole Ndiyo Njia ya Hekima

Tabia Pole Ndiyo Njia ya Hekima

Toñi, ambaye ni muuguzi, alibonyeza kengele na mwanamke wa makamo akafungua mlango. Mwanamke huyo alimtukana Toñi na kumkemea kwa kutofika mapema ili amtunze mama yake aliyezeeka. Lakini Toñi hakuwa amechelewa. Hata hivyo, alikuwa mtulivu na kumwomba msamaha kwa kutoelewana.

ALIPORUDI siku nyingine kumtunza mama huyo, mwanamke huyo alimkemea tena. Toñi alitendaje? Anakiri hivi: “Haikuwa rahisi hata kidogo. Hakuwa na sababu yoyote ya kunitukana.” Hata hivyo, Toñi aliomba msamaha tena na kumwambia mwanamke huyo kwamba alielewa hali ngumu aliyokuwa akikabili.

Ungekuwa Toñi, ungetendaje? Je, ungejitahidi kuwa na tabia pole? Au je, ingekuwa vigumu kudhibiti hisia zako? Ni kweli kwamba si rahisi kuwa mtulivu katika hali kama hiyo. Ni vigumu kuendelea kuwa wenye tabia pole tunapokuwa chini ya mkazo au tunapokasirishwa.

Hata hivyo, Biblia inawatia moyo Wakristo wawe wenye tabia pole. Kwa kweli, Neno la Mungu linahusianisha tabia pole na kuwa wenye hekima. Mwanafunzi Yakobo anauliza hivi: “Ni nani aliye na hekima na mwenye uelewaji kati yenu? Na aonyeshe kutokana na mwenendo wake mzuri matendo yake kwa upole ulio wa hekima.” (Yak. 3:13) Ni katika njia gani tabia pole ni uthibitisho wa kuwa na hekima kutoka juu? Ni nini kinachoweza kutusaidia kusitawisha sifa hiyo ya kimungu?

HEKIMA YA KUONYESHA TABIA POLE

Tabia pole inaweza kupunguza mkazo. “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.”Met. 15:1.

Jibu la hasira linaweza kufanya hali iwe mbaya hata zaidi kwa sababu ni kama kuongeza kuni kwenye moto. (Met. 26:21) Kinyume cha hilo, mara nyingi jibu la upole hutuliza hali. Huenda hata likabadili mtazamo wa mtu mwenye hasira.

Toñi alijionea jambo hilo. Mwanamke huyo alipoona upole wa Toñi, aliangua kilio. Akasema kwamba alikuwa na matatizo ya kibinafsi na ya familia. Toñi alimhubiria, na akaanza kujifunza Biblia na mwanamke huyo kwa sababu ya kubaki mtulivu na kudumisha amani.

Kuwa na tabia pole kunaweza kufanya tuwe wenye furaha. “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.”Mt. 5:5.

Kwa nini watu wenye tabia pole wana furaha? Kwa kujivika upole, watu wengi ambao pindi moja walikuwa wajeuri, sasa ni wenye furaha. Maisha yao yamekuwa bora, nao wanatazamia wakati ujao ulio mzuri. (Kol. 3:12) Adolfo, ambaye ni mwangalizi wa mzunguko nchini Hispania, anakumbuka jinsi maisha yake yalivyokuwa kabla ya kujifunza kweli.

Adolfo anasema hivi: “Sikuwa na kusudi maishani. Mara nyingi nilishindwa kudhibiti hasira yangu kiasi cha kwamba rafiki zangu waliogopa jinsi nilivyotenda kijeuri. Mwishowe jambo fulani lilifanya nibadili maisha yangu kabisa. Pindi moja nilipokuwa nikipigana, nilichomwa kisu mara sita na karibu nife kwa sababu ya kuvuja damu.”

Lakini sasa, kwa maneno na matendo, Adolfo huwafundisha wengine kuwa wenye tabia pole. Watu wengi huvutiwa na utu na uchangamfu wake. Adolfo anasema kwamba anafurahia mabadiliko ambayo amefanya. Na anamshukuru Yehova kwa kumsaidia asitawishe sifa ya upole.

Tabia pole humfurahisha Yehova. “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.”Met. 27:11.

Yehova anadhihakiwa na Ibilisi, ambaye ndiye adui yake mkuu. Mungu ana kila sababu ya kukasirika anapodhihakiwa kimakusudi, hata hivyo Biblia inasema kwamba Yehova “si mwepesi wa hasira.” (Kut. 34:6) Tunapojitahidi kuiga sifa ya Mungu ya kutokuwa wepesi wa hasira na kuwa wapole, tunafanya jambo la hekima ambalo linamfurahisha Yehova sana.—Efe. 5:1.

Ulimwengu tunamoishi umejaa jeuri. Huenda tukakutana na watu ambao ni “wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, . . . wachongezi, wasiojizuia, wakali.” (2 Tim. 3:2, 3) Hata hivyo, hilo halipaswi kumzuia Mkristo kusitawisha sifa ya upole. Neno la Mungu linatukumbusha kwamba “hekima inayotoka juu . . . [ni] yenye kufanya amani, yenye usawaziko.” (Yak. 3:17) Kwa kufanya amani na kuwa na usawaziko, tunathibitisha kwamba tuna hekima kutoka kwa Mungu. Hekima hiyo itatuchochea tuwe wapole tunapokasirishwa na itatusaidia kumkaribia hata zaidi Yehova, ambaye ndiye Chanzo cha hekima yote.