Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nilipokea Kweli ya Biblia Bila Kuwa na Mikono

Nilipokea Kweli ya Biblia Bila Kuwa na Mikono

Kwa kawaida watu hushikilia kitu fulani wanapokuwa na woga. Siwezi kufanya hivyo kwa kuwa sina mikono. Nilikuwa na umri wa miaka saba nilipokatwa mikono ili nisife.

Mama yangu alikuwa na umri wa miaka 17 nilipozaliwa mwaka wa 1960. Baba alimwacha mama kabla ya mimi kuzaliwa. Mimi na mama tuliishi pamoja na babu na bibi (nyanya) katika mji mdogo wa Burg, nchini Ujerumani Mashariki ambayo zamani ilikuwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani. Watu wengi katika mji huo hawakuamini Mungu, hata familia yetu ilikuwa na maoni hayo. Hatukuona umuhimu wa kumwamini Mungu.

Nilipoendelea kukua, nilifurahia kutunzwa vizuri na Babu. Babu alinituma kufanya kazi mbalimbali, kama vile kukata matawi kwenye miti. Nikiwa mtoto, nilipenda sana mambo hayo. Maisha yangu yalikuwa yenye shangwe na furaha.

AKSIDENTI YABADILI MAISHA YANGU

Tukio fulani la kutisha lilitokea nilipokuwa na umri wa miaka saba. Ilikuwa mwanzoni mwa mwaka wangu wa pili tangu nianze shule. Nilipokuwa njiani nikirudi nyumbani, nilipanda katika nguzo ya umeme. Nikiwa urefu wa futi 25 (mita 8) kutoka chini, nilipigwa na shoti kubwa ya umeme na kupoteza fahamu. Nilipoamka nikiwa hospitalini, sikuhisi uwepo wa mikono yangu. Mikono iliungua vibaya sana hivi kwamba ilihitaji kukatwa ili kuzuia sumu isiingie kwenye damu. Unaweza kuwazia jinsi tukio hilo lilivyokuwa pigo kubwa kwa mama, babu, na bibi yangu. Kwa kuwa nilikuwa mtoto, sikuelewa vizuri jinsi ambavyo kutokuwa na mikono kungeathiri maisha yangu.

Baada ya kulazwa hospitali kwa muda, nilianza tena kwenda shuleni. Watoto walinitania, walinisukuma, na kunirushia vitu kwa kuwa sikuweza kujilinda. Maneno yao ya ukatili na kutojali yalinifanya niumie sana. Hatimaye, nilihamishiwa Shule ya Watu Wenye Ulemavu ya Birkenwerder, ni shule ya bweni kwa watoto wenye ulemavu. Kwa kuwa shule ilikuwa mbali sana na nyumbani, mama, babu, na bibi yangu hawakuweza kunitembelea. Nilionana nao wakati wa likizo pekee. Kwa miaka kumi iliyofuata, nilikua bila malezi yao.

KUISHI BILA MIKONO

Nilijifunza kutumia miguu yangu kufanya kazi mbalimbali. Wazia ukila chakula kwa uma au kijiko, ukitumia vidole vya miguu! Kwa kiasi fulani nilifaulu kujifunza ustadi huo. Pia, nilijifunza kupiga mswaki na kuchana nywele kwa kutumia miguu. Hata nilitoa ishara kwa miguu nilipozungumza na watu. Naam, miguu ikawa kama mikono yangu.

Nilipokuwa tineja, nilipenda kusoma machapisho ya sayansi. Nyakati fulani nilijiwazia nikiwa na mikono bandia ambayo ingeniwezesha kufanya kila kitu. Nilipokuwa na umri wa miaka 14 nilianza kuvuta sigara. Nilihisi kwamba kuvuta sigara kulifanya nijiamini na kuwa sawa na watu wengine. Ni kama nilisema: ‘Bila shaka, mimi pia ninaweza kufanya hivyo. Sigara huvutwa na watu wazima iwe wana mikono au hawana.’

Nilikuwa mwenye shughuli nyingi na nilijihusisha na utendaji wa kijamii. Nilijiunga na Free German Youth, chama cha Kisoshalisti kilichofadhiliwa na serikali, nikawa karani, cheo cha juu katika chama. Pia, nilijiunga na kikundi cha uimbaji, nilitunga mashairi, na kushiriki michezo ya watu wenye ulemavu. Baada ya kuhitimu masomo ya ufundi, nilianza kazi katika kampuni fulani kwenye mji wetu. Nilipoendelea kukua, mara kwa mara nilivaa viungo vya bandia ili nionekane mtu kamili.

KUPOKEA KWELI YA BIBLIA

Siku moja nilipokuwa ninasubiri treni ili kwenda kazini, mwanaume fulani alikuja na kuzungumza nami. Aliniambia niwazie wakati ambao Mungu atanirudishia tena mikono yangu miwili. Nilishangaa! Kwa kweli, nilitamani kuwa na mikono, lakini wazo hilo lilikuwa kama hadithi na jambo lisilowezekana! Mimi niliamini kwamba hakuna Mungu. Kuanzia siku hiyo, nilianza kumwepuka mtu huyo.

Baada ya muda fulani, mfanyakazi mwenzangu alinialika kuitembelea familia yao. Tulipokuwa tukinywa kahawa, wazazi wake walianza kuongea kuhusu Mungu, yaani, Yehova. Kwa mara ya kwanza nilisikia kwamba Mungu ana jina. (Zaburi 83:18) Hata hivyo, niliwaza hivi: ‘Ingawa wametaja jina la Mungu, bado naamini hakuna Mungu. Nitawathibitishia kwamba huo ni uwongo.’ Nikiwa na uhakika na maoni yangu, nilikubali tuwe na mazungumzo ya Biblia. Kwa kushangaza, nilishindwa kuthibitisha kwamba hakuna Mungu.

Kadiri tulivyochunguza unabii wa Biblia, maoni yangu kwamba hakuna Mungu yalianza kubadilika. Unabii mwingi umetimia, ingawa uliandikwa mamia au hata maelfu ya miaka mapema. Wakati fulani, tulilinganisha hali ya ulimwengu na unabii wa Mathayo sura ya 24, Luka sura ya 21, na 2 Timotheo sura ya 3. Kama vile dalili fulani zinavyoweza kumsaidia daktari kutambua ugonjwa, mambo yaliyo katika unabii huo yalinisaidia kutambua kwamba tunaishi katika kipindi ambacho Biblia hukiita “siku za mwisho.” * Nilishangaa sana. Ninajionea unabii huo ukitimia.

Niliamini kwamba yale niliyojifunza ni kweli. Nilianza kusali kwa Yehova Mungu na nikaacha kuvuta sigara, ingawa nilikuwa mvutaji wa sigara kwa zaidi ya miaka kumi. Niliendelea kujifunza Biblia kwa karibu mwaka mmoja. Aprili 27, 1986, nilibatizwa kwa siri katika kidimbwi cha bafu, kwa kuwa wakati huo Mashahidi walikuwa chini ya marufuku Ujerumani Mashariki.

KUWAHUBIRIA WENGINE

Kwa sababu ya marufuku, tulifanya ibada katika vikundi vidogo kwenye nyumba za watu, na niliwajua waamini wachache tu. Bila kutarajia, nilikubaliwa na serikali kusafiri kwenda Ujerumani Magharibi, ambako Mashahidi hawakuwa wamepigwa marufuku. Kwa mara ya kwanza, nilihudhuria kusanyiko na kukutana na maelfu ya ndugu na dada. Hilo lilikuwa tukio la pekee sana.

Baada ya Ukuta wa Berlin kubomolewa, Mashahidi wa Yehova waliondolewa marufuku. Hatimaye, tulimwabudu Yehova Mungu kwa uhuru. Nilitamani kufanya mengi zaidi katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, niliogopa sana kuzungumza na watu nisiowafahamu. Nilijiona dhaifu kwa sababu ya ulemavu na kwa kuwa niliishi kwa miaka mingi katika shule ya watu wenye ulemavu. Lakini mwaka wa 1992, nilijaribu kuhubiri saa 60 kwa mwezi. Nilifaulu kufanya hivyo na nilipata shangwe kubwa. Kwa hiyo, niliamua kufanya hivyo kila mwezi na niliendelea kwa karibu miaka mitatu.

Mimi hukumbuka maneno haya ya Biblia: “Ni nani aliye dhaifu, nami si dhaifu?” (2 Wakorintho 11:29) Kwa kuwa bado nina akili na sauti, ninajitahidi kuwasaidia wengine licha ya ulemavu wangu. Kwa sababu sina mikono, ninaelewa vizuri hali ya watu wengine wenye udhaifu. Ninajua jinsi ambavyo wao huhisi wanaposhindwa kufanya jambo fulani wanalotaka kufanya. Ninajitahidi kuwatia moyo. Kuwasaidia wengine kwa njia hiyo hunifurahisha.

Kuwahubiria wengine habari njema hunipa furaha

YEHOVA HUNISAIDIA KILA SIKU

Kusema kweli, nyakati nyingine mimi hushuka moyo. Ninatamani kuwa mtu kamili. Ingawa ninaweza kufanya kazi nyingi za kila siku, ninatumia muda, jitihada, na nguvu nyingi kuliko ilivyo kawaida. Ninakumbuka wazo hili kila siku: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Kila siku Yehova hunipa nguvu ili kufanya kazi za “kawaida.” Nimejifunza kwamba Yehova ataendelea kunisaidia. Hiyo ndiyo sababu sitaacha kumtumikia.

Yehova amenibariki kwa kunipatia familia, jambo ambalo sikufurahia nilipokuwa mtoto na kijana. Nina mke mzuri sana, Elke, ambaye ana upendo na huruma. Kwa kuongezea, nipo kwenye familia ya ulimwenguni pote ya mamilioni ya Mashahidi wa Yehova ambao ni ndugu na dada zangu wa kiroho.

Nikiwa na mke wangu mpendwa, Elke

Pia, ninafarijiwa sana na ahadi ya Mungu ya Paradiso, atakapofanya “vitu vyote kuwa vipya,” kutia ndani mikono yangu. (Ufunuo 21:5) Ninaelewa ahadi hiyo vizuri sana ninapotafakari mambo ambayo Yesu alifanya alipokuwa duniani. Kwa muda mfupi tu, alimponya kilema na kurudisha sikio la mtu lililokuwa limekatwa. (Mathayo 12:13; Luka 22:50, 51) Ahadi za Yehova na miujiza ya Yesu hunipa uhakika kwamba hivi karibuni nitakuwa tena mtu kamili.

Hata hivyo, baraka kubwa zaidi ni kumjua Yehova Mungu. Yeye amekuwa baba na rafiki yangu, nguvu na mfariji wangu. Ninahisi kama Mfalme Daudi aliyeandika hivi: “Yehova ni nguvu zangu . . . Nami nimesaidiwa, hivi kwamba moyo wangu unashangilia.” (Zaburi 28:7) Hii ndio kweli ambayo ninataka kuishikilia maishani mwangu. Nimeipokea bila kuwa na mikono.

^ fu. 17 Kwa habari zaidi kuhusu siku za mwisho, soma sura ya 9, “Je, Tunaishi Katika ‘Siku za Mwisho’?” ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, na kinachopatikana kwenye tovuti ya www.mr1310.com/sw.