Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA TISA

Je, Tunaishi Katika “Siku za Mwisho”?

Je, Tunaishi Katika “Siku za Mwisho”?
  • Ni mambo gani yanayotokea leo yaliyotabiriwa katika Biblia?

  • Neno la Mungu linasema watu wangekuwaje katika “siku za mwisho”?

  • Biblia inatabiri mambo gani mazuri kuhusu “siku za mwisho”?

1. Ni wapi tunapoweza kupata habari kuhusu wakati ujao?

JE, UMEWAHI kusikiliza habari kwenye redio au televisheni na kujiuliza ‘Ulimwengu huu unaelekea wapi?’ Misiba hutokea ghafula na bila kutarajiwa hivi kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kutabiri mambo ya kesho. (Yakobo 4:14) Hata hivyo, Yehova anajua mambo ya wakati ujao. (Isaya 46:10) Zamani, Neno lake, Biblia, lilitabiri mambo mabaya ambayo yangetukia siku zetu na pia likatabiri mambo mazuri ya wakati ujao.

2, 3. Wanafunzi walimuuliza Yesu swali gani, naye alijibuje?

2 Yesu Kristo alizungumza kuhusu Ufalme wa Mungu ambao utakomesha uovu na kuifanya dunia iwe paradiso. (Luka 4:43) Watu walitaka kujua wakati ambapo Ufalme huo ungekuja. Hata wanafunzi wa Yesu walimuuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Kwa kujibu Yesu aliwaambia kwamba ni Yehova Mungu peke yake anayejua kabisa wakati ambapo mwisho wa mfumo huu wa mambo utakuja. (Mathayo 24:36) Lakini Yesu alitabiri mambo ambayo yangetokea duniani kabla tu ya Ufalme huo kuwaletea wanadamu amani na usalama wa kweli. Mambo aliyotabiri yanatukia leo!

3 Kabla ya kuzungumzia mambo yanayothibitisha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” na tuzungumzie kwa ufupi vita ambavyo hakuna mwanadamu yeyote angeweza kuviona. Vilitukia katika makao yasiyoonekana ya roho, na matokeo yake yanatuathiri.

VITA MBINGUNI

4, 5. (a) Ni nini kilichotokea mbinguni mara tu baada ya Yesu kutawazwa kuwa Mfalme? (b) Kulingana na Ufunuo 12:12, matokeo ya vita mbinguni yangekuwa nini?

4 Sura iliyotangulia ya kitabu hiki ilieleza kwamba Yesu Kristo alitawazwa kuwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914. (Danieli 7:13, 14) Muda mfupi baada ya kupokea mamlaka ya Ufalme, Yesu alichukua hatua. Biblia inasema kwamba “Vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli [jina lingine la Yesu] na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa [Shetani Ibilisi], naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana.” * Shetani na malaika zake waovu, yaani, roho waovu, walishindwa katika vita hivyo na kutupwa duniani kutoka mbinguni. Malaika waaminifu wa Mungu walifurahi kwamba Shetani na roho wake waovu walikuwa wametupwa nje. Hata hivyo, wanadamu hawangepata furaha hiyo. Biblia ilitabiri hivi: “Ole wa dunia . . . kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:7, 9, 12.

5 Tafadhali ona matokeo ya vita hivyo vya mbinguni. Kwa hasira, Shetani angeleta ole au taabu duniani. Kama utakavyoona, sasa tunaishi katika kipindi hicho cha taabu. Lakini hakitakuwa kirefu, ni “kipindi kifupi cha wakati.” Hata Shetani anajua hivyo. Biblia inakiita kipindi hicho “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Tunafurahi sana kujua kwamba karibuni Mungu ataondoa matatizo ambayo Ibilisi husababisha duniani. Hebu tuchunguze mambo fulani yaliyotabiriwa katika Biblia ambayo yanatendeka leo. Mambo hayo yanaonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho na karibuni Ufalme wa Mungu utawaletea baraka za milele wale wanaompenda Yehova. Kwanza, tuchunguze mambo manne katika ishara ambayo Yesu alisema ingeonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho.

MATUKIO MAKUBWA YA SIKU ZA MWISHO

6, 7. Maneno ya Yesu kuhusu vita na upungufu wa chakula yanatimizwaje leo?

6 “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Mamilioni ya watu wameuawa vitani katika miaka 100 iliyopita. Mwanahistoria mmoja Mwingereza aliandika hivi: “Watu wengi zaidi waliuawa katika karne ya 20 kuliko wakati mwingine wowote. . . . Katika karne hiyo kulikuwa na mfululizo wa vita, kukiwa na vipindi vifupi vichache vya wakati ambapo hakukuwa na vita mahali fulani ulimwenguni.” Ripoti ya Taasisi ya Worldwatch ilisema hivi: “Idadi ya watu walioathiriwa na vita vya karne [ya 20] ilizidi mara tatu ile ya watu walioathiriwa na vita vyote vilivyopiganwa tangu karne ya kwanza W.K., hadi mwaka wa 1899.” Zaidi ya watu milioni 100 wamekufa kwa sababu ya vita tangu mwaka wa 1914. Hata ikiwa tunahisi maumivu kwa sababu mtu mmoja tunayempenda ameuawa vitani, hatuwezi kuelewa kikamili taabu na maumivu ya mamilioni ya watu wanaofiwa.

7 “Kutakuwa na upungufu wa chakula.” (Mathayo 24:7) Watafiti wanasema kwamba kiasi cha chakula kimeongezeka sana katika miaka 30 iliyopita. Hata hivyo, bado kuna upungufu wa chakula kwa sababu watu wengi hawana pesa za kutosha kununua chakula au mashamba ya kukuza vyakula. Katika nchi zinazoendelea, watu zaidi ya bilioni moja ni maskini hohehahe. Wengi wao hawapati chakula. Shirika la Afya Ulimwenguni linakadiria kwamba watoto zaidi ya milioni tano hufa kila mwaka kutokana na utapiamlo.

8, 9. Ni nini kinachoonyesha kwamba unabii wa Yesu kuhusu matetemeko ya nchi na tauni unatimia?

8 “Kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi.” (Luka 21:11) Kulingana na Uchunguzi wa Kijiolojia wa Marekani, kwa wastani, matetemeko 19 makubwa ya nchi yanatazamiwa kila mwaka. Matetemeko hayo yana nguvu za kutosha kuharibu majengo na kupasua ardhi. Na kwa wastani, kila mwaka kumekuwa na matetemeko yenye nguvu za kutosha kuharibu majengo kabisa. Rekodi zinazopatikana zinaonyesha kwamba matetemeko ya nchi yamesababisha vifo vya watu zaidi ya milioni mbili tangu mwaka wa 1900. Shirika fulani linasema: “Maendeleo ya kitekinolojia yamepunguza vifo kwa kiwango kidogo tu.”

9 “Kutakuwa na tauni.” (Luka 21:11) Licha ya maendeleo ya kitiba, magonjwa ya zamani na mapya yamewakumba wanadamu. Ripoti moja inasema kwamba magonjwa 20 yanayojulikana sana—kutia ndani kifua kikuu, malaria, na kipindupindu—yameanza tena kuenea katika miaka ya karibuni, na inazidi kuwa vigumu kuponya aina fulani za magonjwa hayo kwa dawa. Angalau magonjwa 30 mapya yamezuka. Baadhi yake ni hatari na hayawezi kutibiwa kwa dawa yoyote.

WATU WA SIKU ZA MWISHO

10. Ni mambo gani yaliyotabiriwa katika 2 Timotheo 3:1-5 unayoona watu wakifanya leo?

10 Biblia haielezi tu mambo ambayo yangetukia ulimwenguni bali pia ilitabiri kwamba jamii ya wanadamu ingebadilika katika siku za mwisho. Mtume Paulo alieleza jinsi hali ya watu kwa ujumla ingekuwa. Tunasoma hivi katika 2 Timotheo 3:1-5: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Kwa sehemu, Paulo alisema kwamba watu wangekuwa

  • wenye kujipenda wenyewe

  • wenye kupenda pesa

  • wasiotii wazazi

  • wasio washikamanifu

  • wasio na upendo wa asili

  • wasiojizuia

  • wakali

  • wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu

  • wenye namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake

11. Kulingana na Zaburi 92:7 ni nini kitakachowapata waovu?

11 Je, hivyo ndivyo watu walivyo katika eneo lenu? Bila shaka. Watu walio na tabia hizo mbovu wako kila mahali. Hilo linaonyesha kwamba hivi karibuni Mungu atachukua hatua kwa kuwa Biblia inasema: “Wakati waovu wanapochipuka kama majani na wote wanaotenda mambo yenye kuumiza wanapochanuka, ni ili wao wapate kuangamizwa milele.”—Zaburi 92:7.

MABADILIKO MAZURI!

12, 13. “Ujuzi wa kweli” umekuwaje mwingi katika hizi “siku za mwisho”?

12 Kwa kweli siku za mwisho zimejaa ole, kama vile Biblia ilivyotabiri. Hata hivyo, katika ulimwengu huu wenye matatizo mengi, kuna mabadiliko mazuri kati ya waabudu wa Yehova.

13 Kitabu cha Danieli kilitabiri hivi: “Ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.” Hilo lingetimia wakati gani? “Wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Hasa tangu 1914, Yehova amewasaidia wale ambao kwa kweli wanatamani kumtumikia wapate ujuzi zaidi wa Biblia. Wamepata kuelewa zaidi kweli kuhusu jina la Mungu na kusudi lake, dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, hali ya wafu, na ufufuo. Isitoshe, waabudu wa Yehova wamejifunza kuwa na maisha yanayowafaidi na kumletea Mungu sifa. Pia, wameelewa vizuri zaidi jukumu la Ufalme wa Mungu na jinsi utakavyorekebisha hali duniani. Wanautumiaje ujuzi huo? Swali hilo linatukumbusha unabii mwingine ambao unatimizwa katika siku hizi za mwisho.

“Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.”—Mathayo 24:14

14. Habari njema ya Ufalme imehubiriwa kwa kiwango gani leo, na ni nani wanaoihubiri?

14 Kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu Kristo alitabiri hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.(Mathayo 24:3, 14) Habari njema ya Ufalme inahubiriwa duniani pote katika nchi zaidi ya 230, na kwa zaidi ya lugha 400. Habari hizo zinatia ndani: Ufalme ni nini, utafanya nini, na jinsi tunavyoweza kupata baraka zake. Mamilioni ya Mashahidi wa Yehova huhubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme. Wanatoka katika “mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” (Ufunuo 7:9) Mamilioni ya watu wanaotaka kujua yale ambayo Biblia hufundisha hasa, hujifunza Biblia pamoja na Mashahidi bila malipo. Kwa kweli, huo ni utimizo wenye kuvutia wa unabii hasa kwa kuwa Yesu alitabiri kwamba Wakristo wa kweli ‘wangechukiwa na watu wote’!—Luka 21:17.

UTAFANYA NINI?

15. (a) Je, unaamini kwamba tunaishi katika siku za mwisho, kwa nini? (b) “Mwisho” utamaanisha nini kwa wale wanaompinga Yehova na kwa wale wanaojitiisha kwa Ufalme wa Mungu?

15 Kwa kuwa mambo mengi yaliyotabiriwa katika Biblia yanatimia leo, je hukubali kwamba tunaishi katika siku za mwisho? Baada ya Yehova kuridhika na kuhubiriwa kwa habari njema, hapana shaka kwamba “mwisho” utakuja. (Mathayo 24:14) “Mwisho” ni wakati ambapo Mungu ataondoa uovu duniani. Yehova atamtumia Yesu na malaika wenye nguvu kuwaharibu wote wanaompinga kimakusudi. (2 Wathesalonike 1:6-9) Shetani na roho wake waovu hawatayapotosha mataifa tena. Kisha Ufalme wa Mungu utawaletea baraka nyingi wote wanaojitiisha kwa utawala wake mwadilifu.—Ufunuo 20:1-3; 21:3-5.

16. Unapaswa kufanya nini?

16 Kwa kuwa mwisho wa mfumo wa Shetani u karibu, tunahitaji kujiuliza, ‘Ninapaswa kuwa nikifanya nini?’ Unapaswa kuendelea kujifunza mengi kumhusu Yehova na mambo anayotaka tufanye. (Yohana 17:3) Jifunze Biblia kwa bidii. Uwe na mazoea ya kushirikiana kwa ukawaida pamoja na wale wanaojitahidi kufanya mapenzi ya Yehova. (Waebrania 10:24, 25) Pata ujuzi mwingi ambao Yehova Mungu amewaandalia watu ulimwenguni pote, na ufanye marekebisho yanayohitajiwa maishani mwako ili upate kibali cha Mungu.—Yakobo 4:8.

17. Kwa nini kuharibiwa kwa waovu kutawashtua watu wengi?

17 Yesu alitabiri kwamba watu wengi wangepuuza uthibitisho kwamba tunaishi katika siku za mwisho. Waovu wataharibiwa ghafula na bila kutarajia. Siku hiyo itakuja kama mwizi wakati wa usiku na kuwashtua watu wengi. (1 Wathesalonike 5:2) Yesu alionya hivi: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama vile walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:37-39.

18. Ni onyo gani la Yesu tunalopaswa kuchukua kwa uzito?

18 Kwa hiyo, Yesu aliwaambia hivi watu waliokuwa wakimsikiliza: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama [kupata kibali] mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:34-36) Tunapaswa kuyachukua maneno ya Yesu kwa uzito. Kwa nini? Kwa sababu wale walio na kibali cha Yehova Mungu na cha “Mwana wa binadamu,” Yesu Kristo, wana tumaini la kuokoka mwisho wa mfumo wa mambo wa Shetani na kuishi milele katika ulimwengu mpya ulio karibu sana!—Yohana 3:16; 2 Petro 3:13.

^ fu. 4 Unaweza kupata habari zinazoonyesha kwamba Mikaeli ni jina lingine la Yesu Kristo katika nyongeza “Yule Malaika Mkuu Mikaeli Ni Nani?