Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazee, Mna Maoni Gani Kuhusu Kuwazoeza Wengine?

Wazee, Mna Maoni Gani Kuhusu Kuwazoeza Wengine?

“Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.” —MHU. 3:1.

1, 2. Waangalizi wa mzunguko wameona nini katika makutaniko mengi?

MWANGALIZI wa mzunguko alikuwa akimalizia mkutano na baraza la wazee. Aliwatazama usoni na kuonyesha jinsi anavyowapenda wachungaji hao wenye bidii, ambao baadhi yao walikuwa kama baba zake. Lakini pia kuna jambo lililomhangaisha, hivyo akawauliza, “Akina ndugu, mmefanya nini ili kuwazoeza wengine kushughulikia majukumu kutanikoni?” Walikumbuka vizuri kuwa mwangalizi wa mzunguko aliwasihi katika ziara yake iliyopita watumie muda mwingi zaidi kuwazoeza wengine. Mwishowe, mzee mmoja akasema, “Kusema kweli, hatujafanya mengi.” Wazee wengine wakatikisa vichwa kuonyesha wanakubaliana naye.

2 Ikiwa wewe ni mzee Mkristo, je, umewahi kujikuta katika hali kama hiyo? Huenda umewahi. Waangalizi wa mzunguko wameona kwamba kwenye makutaniko mengi duniani kote kuna uhitaji wa kuwazoeza akina ndugu, vijana kwa wazee, ili wasaidie kulichunga kundi. Lakini si rahisi kufanya hivyo. Kwa nini?

3. (a) Maandiko yanaonyeshaje umuhimu wa kuwazoeza wengine, na kwa nini sote tunapaswa kupendezwa na jambo hilo? (Tazama maelezo ya chini.) (b) Kwa nini wazee fulani huona ni vigumu kuwazoeza wengine?

3 Ukiwa mchungaji, bila shaka unajua kuwa ni muhimu kuwazoeza akina ndugu. * Unajua kwamba ndugu wengi zaidi wanahitajika ili kuyaimarisha kiroho makutaniko na kusaidia kuanzisha makutaniko mapya. (Soma Isaya 60:22.) Pia, unajua kuwa Neno la Mungu linakuhimiza ‘uwafundishe wengine.’ (Soma 2 Timotheo 2:2.) Ingawa hivyo, kama ilivyokuwa kwa wazee waliotajwa mwanzoni, huenda ukaona ni vigumu kuwazoeza wengine. Baada ya kutimiza mahitaji ya familia, majukumu ya kazi, wajibu wa kutaniko, na mambo mengine yanayohitaji kushughulikiwa haraka, huenda ikaonekana kwamba hakuna wakati wa kuwazoeza wengine kutanikoni. Hivyo basi, acheni tuchunguze kwa nini ni muhimu kuwazoeza wengine.

NI MUHIMU SANA KUWAZOEZA WENGINE

4. Ni sababu gani inayoweza kuwafanya wazee waahirishe kuwazoeza wengine?

4 Ni sababu gani inayoweza kuwafanya wazee waone ni vigumu kutenga wakati ili kuwazoeza wengine? Labda wengine hufikiri hivi: ‘Ni muhimu kuwazoeza wengine, lakini kuna mambo mengine ya kutaniko ambayo yanahitaji kushughulikiwa haraka. Hata nikiahirisha kuwazoeza wengine kwa muda fulani, kutaniko litasonga mbele tu.’ Ijapokuwa ni kweli kwamba una mambo mengi yanayohitaji kushughulikiwa haraka, kuahirisha kuwazoeza wengine kunaweza kudhuru hali ya kiroho ya kutaniko.

5, 6. Tunajifunza nini katika mfano wa dereva na maoni yake kuhusu kubadilisha oili kwenye injini ya gari? Na mfano huo unahusianaje na kuwazoeza wengine kutanikoni?

5 Fikiria mfano huu: Dereva anajua kwamba ni lazima abadilishe oili kwa ukawaida ili injini ya gari ifanye kazi vizuri, na gari lake libaki katika hali nzuri. Lakini huenda akafikiri kwamba kubadilisha oili si jambo la haraka sana kama kujaza mafuta kwenye gari. Isitoshe, asipojaza mafuta, gari lake halitatembea kabisa. Kwa hiyo anaweza kujiambia hivi, ‘Nisipopata muda wa kubadilisha oili, bado injini itaendelea kufanya kazi, angalau kwa muda fulani.’ Lakini kuna hatari gani? Ikiwa dereva ataendelea kuahirisha kubadilisha oili, mwishowe gari lake litaharibika kabisa. Hilo linapotokea, atahitaji kutumia muda na pesa nyingi sana kutengeneza gari ili lifanye kazi tena. Tunajifunza nini?

6 Wazee hushughulikia mambo mengi yanayohitaji kufanywa haraka; wasipofanya hivyo kutaniko litaathirika sana. Kwa hiyo, kama vile dereva anavyohakikisha kuwa anajaza gari mafuta kwa ukawaida, vivyo hivyo ni lazima wazee ‘wahakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Flp. 1:10) Hata hivyo, baadhi ya wazee wanatumia muda mwingi kushughulikia mambo ya haraka hivi kwamba wanakosa wakati wa kuwazoeza wengine, yaani, ni kana kwamba wanapuuza kubadilisha oili kwenye injini ya gari. Lakini ikiwa wazee wataendelea kuahirisha kuwazoeza wengine, hatimaye kutaniko litakosa ndugu wa kutosha wanaostahili kushughulikia majukumu kutanikoni.

7. Tunapaswa kuwaonaje wazee wanaotenga muda ili kuwazoeza wengine kutanikoni?

7 Hivyo basi, hatupaswi kufikiri kwamba mambo mengine ni muhimu zaidi kuliko kuwazoeza wengine. Wazee wanaofikiria wakati ujao na kutumia muda wao kuwazoeza ndugu wasio na uzoefu, ni wasimamizi-nyumba wenye hekima na ni baraka kutanikoni. (Soma 1 Petro 4:10.) Kutaniko linafaidikaje?

KUTUMIA WAKATI VIZURI

8. (a) Ni sababu gani zinazowachochea wazee wawazoeze wengine? (b) Wazee wanaotumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wanahitaji kutimiza wajibu gani wa haraka? (Tazama sanduku lenye kichwa “ Kazi ya Haraka.”)

8 Hata wazee wenye uzoefu mwingi wanapaswa kuwa wenye kiasi na kutambua kwamba umri unaposonga, pole kwa pole watashindwa kutimiza mambo mengi kutanikoni. (Mika 6:8) Pia, wanapaswa kuzingatia kwamba ‘wakati na matukio yasiyotazamiwa’ yanaweza kubadili mambo ghafla, na kuwafanya washindwe kutimiza majukumu yao kutanikoni. (Mhu. 9:11, 12; Yak. 4:13, 14) Kwa sababu wanawapenda sana kondoo wa Yehova, wazee wanaofikiria wakati ujao wanawazoeza ndugu vijana na kuwafundisha mambo ambayo wamejifunza kwa miaka mingi.—Soma Zaburi 71:17, 18.

9. Ni tukio gani la wakati ujao linalofanya kazi ya kuwazoeza wengine iwe muhimu sana?

9 Isitoshe, wazee wanaowazoeza wengine ni baraka kutanikoni kwa sababu wanaimarisha ulinzi wa kutaniko. Jinsi gani? Mazoezi hayo yanawasaidia ndugu wengi wawe tayari kulisaidia kutaniko libaki imara na lenye umoja katika siku hizi za mwisho, na yatawasaidia zaidi wakati wa dhiki kuu inayokuja. (Eze. 38:10-12; Mika 5:5, 6) Kwa hiyo, wazee wapendwa, tunawasihi muanze leo kuwazoeza wengine kutanikoni kwa ukawaida.

10. Huenda mzee akahitaji kufanya nini ili apate wakati wa kuwazoeza wengine?

10 Bila shaka, tunaelewa kwamba mnatumia muda mwingi sana kutimiza utendaji muhimu kutanikoni. Hata hivyo, huenda mkahitaji kupunguza wakati mnaotumia katika utendaji huo na muutumie kuwazoeza wengine. (Mhu. 3:1) Hiyo ni njia nzuri sana ya kutumia wakati wenu.

TAYARISHA MOYO WA NDUGU UNAYEMZOEZA

11. (a) Ni jambo gani linalovutia kuhusiana na mapendekezo yaliyotolewa na wazee kutoka nchi mbalimbali? (b) Kulingana na Methali 15:22, kuna faida gani kuzungumzia mapendekezo ya wazee wengine?

11 Hivi karibuni, kikundi cha wazee ambao wamefanikiwa kuwasaidia ndugu wengine wakue kiroho waliulizwa wanatumia njia gani kufanya hivyo. * Ijapokuwa hali za wazee hao zinatofautiana sana, ushauri waliotoa unafanana sana. Hilo linaonyesha nini? Mazoezi yanayotegemea Biblia yanaweza kutumiwa kuwazoeza wale wasio na uzoefu “kila mahali katika kila kutaniko”—kama ilivyokuwa katika siku za Paulo. (1 Kor. 4:17) Hivyo, katika makala hii na ile inayofuata, tutazungumzia baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na wazee hao.—Met. 15:22.

12. Mzee anahitaji kutayarisha nini, na kwa nini?

12 Mzee anahitaji kuutayarisha kwanza moyo wa ndugu anayemzoeza. Kama vile mtunza bustani anavyohitaji kulima au kutifua udongo kabla ya kupanda mbegu, ndivyo ambavyo mzee anahitaji kuutayarisha moyo wa ndugu anayemzoeza kabla ya kuanza kumfundisha mbinu mpya. Hivyo, wazee wanaweza kuitayarishaje mioyo ya wale wanaowazoeza? Kwa kutumia njia kama ile aliyotumia nabii fulani wa kale. Ni njia gani hiyo?

13-15. (a) Samweli alipewa mgawo gani? (b) Samweli alitimizaje mgawo wake? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 3.) (c) Kwa nini wazee wanapaswa kupendezwa na simulizi la Samweli?

13 Siku moja, zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Yehova alimwambia hivi Samweli aliyekuwa amezeeka: “Karibu wakati kama huu kesho nitatuma mtu kwako kutoka katika nchi ya Benyamini, nawe umtie mafuta awe kiongozi juu ya watu wangu Israeli.” (1 Sam. 9:15, 16) Samweli alitambua kwamba hangeendelea kuliongoza taifa la Israeli, na Yehova alimwagiza amtie mafuta mtu ambaye angechukua nafasi yake. Labda Samweli alijiuliza, ‘Nitamtayarishaje mtu huyo kwa ajili ya mgawo wake?’ Alipata wazo na akapanga jinsi atakavyofanya.

14 Siku iliyofuata, Samweli alipomwona Sauli, Yehova alimwambia hivi: “Huyu ndiye.” Kisha Samweli akafanya kama alivyopanga. Alimwalika Sauli wale mlo pamoja katika jumba la kulia chakula. Halafu akampa Sauli na mtumishi wake sehemu nzuri ya kuketi na vipande bora vya nyama, naye akasema: “Ule, kwa maana wamekuwekea hicho akiba.” Baada ya hapo, Samweli alimkaribisha Sauli nyumbani kwake. Walipokuwa njiani walizungumza mambo mbalimbali. Samweli alimstarehesha Sauli kwa kumwandalia mlo mzuri na kuzungumza naye kirafiki walipokuwa wakitembea, naye alitaka kutumia vizuri hali hiyo. Hivyo walipofika, Samweli akamkaribisha Sauli darini. Upepo mwanana wa jioni ulipokuwa ukivuma, Samweli “akaendelea kusema na Sauli darini” hadi walipoenda kulala. Siku iliyofuata, Samweli alimtia mafuta Sauli, akambusu, na kumpa maagizo zaidi. Kisha, akamruhusu Sauli aende—akiwa tayari kwa ajili ya matukio yatakayofuata.—1 Sam. 9:17-27; 10:1.

15 Bila shaka kumtia mtu mafuta ili awe kiongozi wa taifa, si sawa na kumzoeza ndugu ili awe mzee au mtumishi wa huduma kutanikoni. Hata hivyo, wazee wanaweza kujifunza mambo kadhaa kutokana na njia aliyotumia Samweli. Acheni tuchunguze mambo mawili.

MARAFIKI WA KWELI NA WALIO TAYARI KUWAZOEZA WENGINE

16. (a) Samweli alihisije Waisraeli walipoomba wapewe mfalme? (b) Samweli alitendaje alipoambiwa amtie mafuta Sauli?

16 Uwe tayari, usisite. Mwanzoni, Samweli aliposikia kwamba Waisraeli wanataka mfalme, alivunjika moyo na alihisi watu wake wamemkataa. (1 Sam. 8:4-8) Alisita kufanya kile ambacho watu walitaka hivi kwamba Yehova akamwambia mara tatu awasikilize. (1 Sam. 8:7, 9, 22) Hata hivyo, Samweli hakumwekea kinyongo yule atakayechukua nafasi yake. Yehova alipomwambia amtie mafuta Sauli, nabii huyo alitii, si kwa shingo upande au ili tu kutimiza wajibu, bali kwa kupenda.

17. Wazee leo huigaje mtazamo wa Samweli, nao huridhika wanapoona nini?

17 Kama Samweli, wazee wenye uzoefu leo wanawaonyesha fadhili wale wanaowazoeza. (1 Pet. 5:2) Wazee hao wako tayari kuwazoeza wengine na hawaogopi kwamba wale wanaozoezwa watachukua baadhi ya mapendeleo yao kutanikoni. Wazee wenye mtazamo mzuri huwaona wale wanaozoezwa kuwa “wafanyakazi wenzi” wenye thamani kutanikoni na si washindani wao. (2 Kor. 1:24; Ebr. 13:16) Wazee hao wasio na ubinafsi huridhika sana wanapowaona wale wanaowazoeza wakitumia uwezo wao kunufaisha kutaniko.—Mdo. 20:35.

18, 19. Mzee anaweza kuutayarishaje moyo wa yule anayemzoeza, na kwa nini ni muhimu kufanya hivyo?

18 Jenga urafiki. Siku ambayo nabii Samweli alikutana na Sauli, angeweza kumtia mafuta mara moja ili awe mfalme kwa kuchukua mafuta, kummiminia kichwani, na kisha kumwacha aende. Mfalme huyo angekuwa ametiwa mafuta, lakini hangekuwa ametayarishwa kuwaongoza watu wa Mungu. Badala yake, Samweli alitumia wakati kuutayarisha moyo wa Sauli hatua kwa hatua. Baada ya kula mlo mzuri, kutembea pamoja, kuzungumza kwa muda mrefu, na kupumzika vizuri ndipo nabii huyo aliona kuwa wakati umefika wa kumtia mafuta Sauli.

Kusitawisha urafiki wa karibu ni hatua ya kwanza katika kuwazoeza wengine (Tazama fungu la 18, 19)

19 Vivyo hivyo, mzee anapaswa kuanza kumzoeza ndugu kwa kutumia wakati kutayarisha mazingira mazuri yenye kustarehesha, na kujenga urafiki kati yake na anayemzoeza. Hatua hususa ambazo mzee anachukua kujenga urafiki zinaweza kutofautiana kati ya nchi moja na nyingine, ikitegemea hali na desturi za eneo hilo. Lakini, hata iwe unaishi wapi au una shughuli nyingi kadiri gani, ukitumia wakati pamoja na yule unayemzoeza, atajua kwamba unamwona kuwa mtu muhimu. (Soma Waroma 12:10.) Kwa hakika, wale unaowazoeza watathamini sana upendo na uangalifu unaowapa.

20, 21. (a) Mzee anapaswa kufanya nini ili afanikiwe? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

20 Wazee, kumbukeni hili: Ili mzee afanikiwe, ni lazima apende kuwazoeza wengine na awapende wale anaowazoeza. (Linganisha na Yohana 5:20.) Ndugu anayezoezwa atatambua haraka mtazamo huo mzuri wa mzee na utamfanya akubali mazoezi anayopata. Kwa hiyo, wazee wapendwa, mnapowazoeza wengine, jitahidini kujenga urafiki pamoja nao.—Met. 17:17; Yoh. 15:15.

21 Baada ya kuutayarisha moyo wa ndugu anayetaka kumzoeza, mzee ataanza kumzoeza ndugu huyo. Mzee anaweza kutumia njia gani? Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

^ fu. 3 Makala hii na ile inayofuata zimeandaliwa hasa kwa ajili ya wazee, hata hivyo wengine kutanikoni wanapaswa kupendezwa na mambo yanayozungumziwa. Kwa nini? Kwa sababu itawachochea wanaume waliobatizwa watambue kwamba wanahitaji kuzoezwa ili wasaidie majukumu mbalimbali kutanikoni. Ndugu wengi wanapozoezwa, sisi sote tutafaidika.

^ fu. 11 Wazee hao wanaishi nchini Afrika Kusini, Australia, Bangladesh, Brazili, Guiana ya Ufaransa, Japani, Korea, Marekani, Mexico, Namibia, Nigeria, Réunion, Ubelgiji, Ufaransa, na Urusi.