Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mchukue Mwana Wako”

“Mchukue Mwana Wako”

Mkaribie Mungu

“Mchukue Mwana Wako”

2 WAFALME 4:8-37

KIFO cha mtoto ni chenye kuumiza sana kwa mzazi. Yehova Mungu ana nguvu za kumfufua mtoto aliyekufa. Tunajua hivyo kwa sababu katika nyakati za Biblia, aliwawezesha wanaume wachache kuwafufua wafu. Kisa kimoja ambacho kimesimuliwa katika 2 Wafalme 4:8-37, kinamhusu mvulana aliyefufuliwa na nabii Elisha.

Kisa hiki kinatokea jijini Shunemu. Mwanamke fulani ambaye ni tasa, pamoja na mume wake wanamwonyesha Elisha fadhili kwa kumwandalia chakula na mahali pa kulala kwa ukawaida. Siku moja, nabii huyo mwenye shukrani anamwambia mwanamke huyo hivi: “Mwaka ujao wakati huu uliowekwa utakuwa unamkumbatia mwana.” Baadaye, kama Elisha alivyokuwa amesema, mwanamke huyo anapata mwana ingawa hakufikiria angekuja kupata mtoto. Lakini shangwe yake haidumu. Miaka michache baadaye, mvulana huyo anapatwa na maumivu makali ya kichwa akiwa shambani na anabebwa mpaka nyumbani ambamo anakufa “juu ya magoti [ya mama] yake.” (Mistari ya 16, 19, 20) Mama huyo aliyefiwa anaichukua maiti ya mvulana wake mdogo na kuilaza juu ya kitanda ambacho nabii Elisha alikuwa akilalia mara nyingi.

Bila kupoteza wakati, mwanamke huyo anamwomba ruhusa mume wake na kusafiri umbali wa kilomita 30 mpaka Mlima Karmeli ili kumwona Elisha. Anapokutana na Elisha, mwanamke huyo halii, wala kutokwa na machozi, au kutenda jambo lolote kuonyesha huzuni kubwa. Je, ni kwa sababu amesikia kuwa Eliya, nabii aliyemtangulia Elisha, alikuwa amemfufua mwana wa mjane fulani? (1 Wafalme 17:17-23) Je, mwanamke huyo Mshunamu ana imani kwamba Elisha anaweza kumfufua mvulana wake? Vyovyote vile, anakataa kurudi nyumbani mpaka Elisha anapokubali kwenda naye.

Baada ya kurudi Shunemu, Elisha anaingia peke yake katika chumba alichokuwa akikaa mara nyingi na kuuona mwili usio na uhai ukiwa “juu ya kitanda chake.” (Mstari wa 32) Nabii anasali kwa Yehova na kumsihi sana kwa dua. Kisha, Elisha akiwa anainama juu ya mtoto huyo, ‘hatua kwa hatua mwili wake unakuwa na joto.’ Na moyo wa mtoto huyo mdogo unaanza kupiga tena! Elisha anamwita mama ya mtoto na kusema maneno ambayo bila shaka yanaondoa huzuni yake na kumfanya afurahi sana. Anamwambia: “Mchukue mwana wako.”—Mistari ya 34, 36.

Kisa hicho cha ufufuo wa mwana wa mwanamke Mshunamu kinatupa tumaini na faraja. Yehova anaelewa huzuni ya mzazi ambaye amefiwa na mtoto. Zaidi ya hilo, anatamani kuwafufua watoto hao. (Ayubu 14:14, 15) Visa vya watu waliofufuliwa na Elisha na pia watu wengine katika nyakati za Biblia vinaonyesha kwamba Yehova atawafufua watu wengi zaidi katika ulimwengu mpya wenye uadilifu unaokuja. *

Ahadi ya Biblia kuhusu ufufuo haiondoi uchungu wa kufiwa na mpendwa wetu. Mwanamume mmoja Mkristo aliyefiwa na mtoto wake wa pekee alisema hivi: “Uchungu wangu hautaisha kabisa mpaka nitakapomkumbatia mwana wangu tena.” Wazia tarajio la kuungana tena na wapendwa wako waliokufa. Kujua tu kwamba unaweza kuwakumbatia tena kunaweza kupunguza uchungu wako. Je, ungependa kujifunza kumhusu Mungu ambaye anatoa tumaini hilo zuri?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa habari zaidi kuhusu ahadi ya Biblia ya ufufuo, ona sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.