Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Seremala”

“Seremala”

Wakristo wa Karne ya Kwanza Walivyoishi

“Seremala”

“Je, huyu si mwana wa yule seremala?”—MATHAYO 13:55.

YESU hakufahamika tu kama “mwana wa yule seremala,” bali pia kama “yule seremala.” (Marko 6:3) Huenda alijifunza kazi hiyo kutoka kwa Yosefu, aliyekuwa baba-mlezi wake.

Yesu alihitaji kujifunza ustadi gani na kutumia vifaa gani katika kazi ya useremala? Ni kazi gani za useremala ambazo huenda Yesu aliwafanyia wakaaji wa Nazareti? Na huenda mafunzo ya useremala aliyopata akiwa bado kijana yalikuwa na uvutano gani katika maisha yake ya baadaye?

Biashara ya Familia Picha iliyo chini inaonyesha baba akimfundisha mwana wake wa kwanza jinsi ya kutumia aina fulani ya kekee. Mwana wake mwingine anasikiliza na kutazama kwa makini.

Mara nyingi wavulana walianza kuzoezwa ufundi wa useremala walipokuwa na umri wa kati ya miaka 12 na 15. Kwa kawaida, walifundishwa ufundi huo na baba yao. Kuzoezwa huko kuliendelea kwa miaka mingi, na wavulana hao walijitahidi sana kupata ustadi uliohitajika ili kuwa seremala bora. Wazia vipindi vingi vizuri ambavyo Yosefu alitumia pamoja na Yesu akifanya kazi naye, akizungumza naye, na kumfundisha ili awe stadi wa kazi. Bila shaka Yosefu alifurahi sana kuona maendeleo ya Yesu alipokuwa akijifunza kufanya kazi hiyo kwa ustadi.

Ujuzi, Ustadi, na Nguvu Zilihitajika Seremala alihitaji kujua aina ya mbao aliyokuwa akitumia. Angechagua mbao za miti iliyopatikana karibu na kwao kama vile mvinje, mwaloni, mwerezi, mkuyu, na mzeituni. Hata hivyo, wakati huo hakukuwa na maduka ambayo yaliuza mbao zilizokuwa zimekatwa vipande-vipande, tayari kutumiwa. Hivyo, seremala alihitaji kwenda msituni ili achague miti aliyotaka, aikate, na kisha aikokote mpaka kwenye karakana yake.

Seremala alitengeneza vitu gani kwa mbao alizokusanya? Huenda alisaidia katika ujenzi wa nyumba. Angekata mbao za boriti kwa ajili ya paa, na kutengeneza ngazi za vyumba vya juu, milango, madirisha, na nguzo za ukuta.

Seremala aliunda fanicha pia. Picha ifuatayo inaonyesha baadhi ya vitu hivi—kabati zenye rafu na milango (1); aina mbalimbali za viti (2, 3), na meza (4) za aina tofauti-tofauti; na vitanda vya watoto. Ili fanicha fulani zionekane maridadi, alizipamba kwa vipande vya mbao vilivyochongwa kwa njia yenye kupendeza. Nta, vanishi, au mafuta yalitumiwa ili kuhifadhi fanicha hizo na kuzifanya zipendeze.

Vifaa vya wakulima vilivyotengenezwa na seremala vilitia ndani nira (5) zilizochongwa kwa mbao ngumu, na majembe, reki, na sepetu (6). Majembe ya kukokotwa (7) yenye ncha za chuma aliyotengeneza yalihitaji kuwa thabiti kwa sababu yalitumiwa kulima udongo wenye mawe-mawe. Aliunda mikokoteni (8) na magari ya kukokotwa yenye magurudumu ya mbao. Pia, huenda kazi ya seremala ilitia ndani kurekebisha na kudumisha fanicha, vifaa, na magari yaliyoharibika.

Je, unaweza kuwazia jinsi mwili wa Yesu ulivyokuwa kwa sababu ya kazi ya useremala? Wazia ngozi yake iliyogeuka rangi kwa kupigwa na jua la Mashariki ya Kati, misuli yake yenye nguvu kwa sababu ya kufanya kazi ngumu kwa miaka mingi, na ngozi ngumu ya mikono yake kwa kuwa alibeba mbao zisizo laini na kutumia mashoka, nyundo, na misumeno.

Chanzo cha Mifano Yesu alitumia mifano rahisi na iliyojulikana na wengi kwa ustadi ili kufundisha kweli muhimu za kiroho. Je, alitumia mifano iliyotokana na ujuzi wake wa useremala? Fikiria mifano ifuatayo. Aliuambia umati hivi: “Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe?” Bila shaka seremala alijua ukubwa wa boriti. (Mathayo 7:3) Baadaye, Yesu aliwaambia watu wengine hivi: “Hakuna mutu akiweka mukono wake juu ya jembe la kukokotwa, na kisha kutazama nyuma, anayefaa kwa ufalme wa Mungu.” Yaelekea Yesu alikuwa ameunda majembe mengi ya kukokotwa. (Luka 9:62, Zaire Swahili Bible) Mwaliko mmoja wa Yesu wenye fadhili sana ulihusisha kifaa ambacho kiliundwa na seremala. Alisema hivi: ‘Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.’ (Mathayo 11:29, 30) Hapana shaka kwamba Yesu alijua kutengeneza nira iliyokuwa “laini,” yenye kutoshea vizuri na ambayo haikuchubua ngozi.

Huenda wapinzani wa Yesu walimrejelea kwa dhihaka kuwa “mwana wa yule seremala.” Lakini, licha ya dhihaka hizo, Wakristo katika karne ya kwanza na leo pia, huthamini pendeleo la kuwa wafuasi wa mtu huyu mnyenyekevu ambaye hapo awali alikuwa seremala.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

Sanduku la Vifaa vya Seremala

Seremala aliyeishi katika karne ya kwanza kama Yesu alihitaji kujua jinsi ya kutumia vifaa vinavyoonyeshwa hapa. Msumeno wake (1) ulikuwa na kishikio cha mbao kilichoshikilia sehemu ya chuma yenye meno ambayo yalikuwa yameundwa ili yakate kwa kuvutwa tu. Alitumia filifili (2) kupima na kuchora, na timazi (3) ili kupima sehemu zilizo wima. Vilevile, ndani ya sanduku lake kulikuwa na pimamaji (4), fimbo ya kupimia (5), randa yenye sehemu ya chuma iliyo na makali ya kulainisha mbao (6), na shoka (7) la kukatia miti.

Kerezo ya seremala (8) pamoja na bobari (9) zilitumiwa kukata na kutengeneza mikono ya kusokotea nyuzi. Juu ya kifuniko cha sanduku kuna nyundo ya mti (10) iliyotumiwa kupigilia patasi au vijiti vilivyotumiwa kama misumari ya kushikanisha mbao. Pia, kuna msumeno mdogo (11), aina fulani ya kisu (12) cha kukatia maumbo, na misumari (13). Mbele ya sanduku hilo, kuna nyundo ya chuma (14) na tezo (15) ya kuchongea mbao. Vilevile, juu ya kifuniko kuna kisu kingine (16) na pia patasi (17) zenye upana tofauti-tofauti. Kekee yenye umbo la uta (18) imeegemezwa kwenye sanduku.