Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya Furaha ya Familia

Jinsi ya Kufaulu Katika Mwaka wa Kwanza wa Ndoa

Jinsi ya Kufaulu Katika Mwaka wa Kwanza wa Ndoa

Mume anasema: “Nimeshangaa kutambua kwamba mimi na mke wangu tuna mapendezi yanayotofautiana sana! Kwa mfano, mimi ninapenda kuamka mapema, yeye naye anapenda kukaa mpaka usiku sana. Na, sielewi hisia zake zinazobadilika-badilika! Vilevile, ninapopika, ananichambua sana, hasa kwa sababu ninatumia kitambaa cha kupanguzia vyombo kupanguza mikono yangu.”

Mke anasema: “Mume wangu hapendi kuongea sana. Mimi nami nimezoea watu wa familia yetu. Wanaongea sana, hasa nyakati za milo. Na mume wangu anapopika, anatumia kitambaa kilekile kupanguza vyombo na mikono yake! Tabia hiyo inaniudhi! Kwa nini ni vigumu sana kuwaelewa wanaume? Watu wanafaulu jinsi gani kuwa na ndoa yenye furaha?”

IWAPO umefunga ndoa hivi karibuni, je, umekabili matatizo kama hayo? Je, sasa inaonekana kuwa mume au mke wako ana udhaifu na tabia za kigeni ambazo hukuona mlipochumbiana? Unaweza kupunguza jinsi gani ‘matatizo ya dunia hii ambayo watu ambao wameoana wanapata’?—1 Wakorintho 7:28, Biblia Habari Njema.

Kwanza, usifikiri kwamba wewe na mume au mke wako mnajua kila kitu kuhusiana na maisha ya ndoa kwa sababu tu mmefunga ndoa. Ulipokuwa mseja, yaelekea, ulisitawisha ustadi muhimu wa kushirikiana na watu, na huenda ustadi huo uliboreka mlipokuwa mnachumbiana. Hata hivyo, baada ya kufunga ndoa unahitaji kuutumia katika hali mpya na huenda ikakubidi usitawishe ustadi ambao hukuwa nao hapo awali. Je, utakosea? Ndiyo! Je, unaweza kusitawisha ustadi ambao unahitaji? Bila shaka!

Njia bora ya kuboresha ustadi wowote ule ni kumwomba mtaalamu akusaidie, na kisha ufuate mashauri anayotoa. Mtaalamu mkuu wa ndoa ni Yehova Mungu. Yeye ndiye aliyetuumba tukiwa na tamaa ya kuoa au kuolewa. (Mwanzo 2:22-24) Ona jinsi Neno lake, Biblia, linavyoweza kukusaidia kutatua matatizo na kusitawisha ustadi unaohitajika ili ndoa yako idumu zaidi ya mwaka mmoja.

USTADI WA KWANZA. JIFUNZENI KUSHAURIANA

Kwa nini ni vigumu?

Keiji * ni mume anayeishi Japani. Mara kwa mara alisahau kwamba maamuzi yake yalihusisha mke wake pia. Anasema hivi: “Nilizoea kukubali mialiko bila kushauriana na mke wangu. Baadaye niligundua kwamba mialiko hiyo haikufaa ratiba yake.” Allen, mume anayeishi barani Australia, anasema: “Nilifikiri kwamba haifai kwa mwanamume kushauriana na mke wake kabla ya kufanya uamuzi.” Alikuwa na tatizo hilo kwa sababu ya malezi yake. Dianne anayeishi Uingereza, alikuwa na tatizo kwa sababu ya malezi yake pia. Dianne anasema hivi: “Nilikuwa nimezoea kuwaomba watu wa familia yetu mashauri. Kwa hiyo, mwanzoni nilipohitaji kufanya uamuzi, nilishauriana nao, bali si na mume wangu.”

Suluhisho ni nini?

Kumbuka kwamba Yehova Mungu anawaona mume na mke kuwa “mwili mmoja.” (Mathayo 19:3-6) Machoni pake, hakuna uhusiano kati ya wanadamu ambao ni muhimu kuliko uhusiano kati ya mume na mke! Ili uhusiano huo udumu, mazungumzo mazuri ni muhimu.

Mume na mke wanaweza kujifunza mengi kwa kuchunguza jinsi Yehova Mungu alivyozungumza na Abrahamu. Kwa mfano, tafadhali soma mazungumzo yanayosimuliwa katika Mwanzo 18:17-33. Mungu alimheshimu Abrahamu kwa njia tatu. (1) Yehova alimweleza Abrahamu alichokusudia kufanya. (2) Alimsikiliza Abrahamu alipotoa maoni yake. (3) Kwa kadiri alivyoweza, Yehova alibadili njia yake ya kutimiza kile alichokusudia kufanya ili Abrahamu aridhike. Unaweza kuiga mfano huu jinsi gani unaposhauriana na mume au mke wako?

JARIBU KUFANYA HIVI: Unapozungumzia mambo yanayohusisha mume au mke wako, (1) mweleze jinsi ambavyo ungependa kuyashughulikia, lakini utoe maoni yako kama mapendekezo, si kama mambo ambayo yameshaamuliwa, au kwa kumtisha; (2) mwombe mume au mke wako atoe maoni yake, na utambue haki yake ya kuwa na maoni yanayotofautiana na yako; na (3) acha ‘usawaziko wako ujulikane’ kwa kukubali mapendezi ya mume au mke wako kila inapowezekana.—Wafilipi 4:5.

USTADI WA PILI. JIFUNZENI KUSEMA KWA BUSARA

Kwa nini ni vigumu?

Labda una tabia ya kutoa maoni yako kwa uthabiti, bila busara, kwa kuwa jambo hilo ni la kawaida katika familia yako au utamaduni wako. Kwa mfano, Liam anayeishi Ulaya anasema hivi: “Watu wengi wa nchi yangu ya asili wanaongea bila busara. Mara nyingi, njia yangu ya kuongea ilimuudhi mke wangu. Ilinibidi kujifunza kuongea kwa upole.”

Suluhisho ni nini?

Usikate kauli kwamba mume au mke wako anafurahi unapoongea naye kwa njia ambayo umezoea tangu utotoni. (Wafilipi 2:3, 4) Shauri ambalo mtume Paulo alimpa mmishonari fulani linawafaa pia watu ambao wameoana hivi karibuni. Aliandika hivi: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.” Neno la Kigiriki cha awali linalotafsiriwa “mpole” linaweza pia kumaanisha “mwenye busara.” (2 Timotheo 2:24) Busara ni uwezo wa kuona umuhimu wa kushughulikia hali fulani kwa uangalifu na kwa fadhili bila kumuudhi mtu.

JARIBU KUFANYA HIVI: Mnapokoseana, wazia kwamba unaongea na rafiki wa karibu au mwajiri wako, bali si mume au mke wako. Je, bado ungetumia maneno yaleyale, au ungesema kwa njia iyo hiyo? Halafu, jiulize kwa nini inafaa uongee na mume au mke wako kwa heshima hata zaidi kuliko unavyoongea na rafiki au mwajiri wako.—Wakolosai 4:6.

USTADI WA TATU. JIFUNZENI KUTIMIZA MAJUKUMU YENU MAPYA

Kwa nini ni vigumu?

Mwanzoni huenda mume, bila kukusudia, akafanya maamuzi yanayomuumiza mke wake, au mke anashindwa kutoa mapendekezo yake kwa busara. Kwa mfano, Antonio, mume anayeishi Italia, anasema: “Baba yangu hakuwa na zoea la kushauriana na mama yangu kabla ya kufanya maamuzi yaliyohusu familia. Kwa hiyo, mwanzoni nilitawala familia yangu kama mfalme.” Debbie, ambaye ni mke nchini Kanada, anasema: “Nilitaka mume wangu awe nadhifu zaidi. Lakini kwa sababu nilizungumza naye kana kwamba nilikuwa ninamwamuru, alishikilia tabia zake hata zaidi.”

Mume anaweza kufanya nini?

Baadhi ya waume wanafikiri kuwa kile ambacho Biblia inasema kuhusu ujitiisho wa mke kwa mume ni sawa na ujitiisho wa mtoto kwa mzazi wake. (Wakolosai 3:20; 1 Petro 3:1) Hata hivyo, Biblia inasema mume “atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja”; haisemi hivyo kuhusu mzazi na mtoto. (Mathayo 19:5) Yehova anamfafanua mke kuwa kikamilisho, au mwenzi, wa mume wake. (Mwanzo 2:18) Hasemi kamwe kuwa mtoto ni kikamilisho, au mwenzi, wa mzazi. Mume akimtendea mke kana kwamba yeye ni mtoto, je, anaheshimu mpango wa ndoa? Maoni yako ni nini?

Neno la Mungu linakuhimiza umtendee mke wako kama Yesu anavyolitendea kutaniko la Kikristo. Unaweza kufanya iwe rahisi kwa mke wako kukuheshimu kama kichwa chake ikiwa (1) hutazamii ajitiishe kwako mara moja bila kukosea hata kidogo, na (2) ukimpenda kama unavyoupenda mwili wako mwenyewe, hata wakati matatizo yanapotokea.—Waefeso 5:25-29.

Mke anaweza kufanya nini?

Tambua kwamba mume wako ni kichwa chako katika mpango wa Mungu. (1 Wakorintho 11:3) Ukimheshimu mume wako, unamheshimu Mungu. Ukimkataa mume wako kuwa kichwa, unaonyesha maoni yako kumhusu na pia maoni yako kuhusu matakwa ya Mungu.—Wakolosai 3:18.

Unapozungumzia matatizo magumu, jitahidi kuzungumzia tatizo lenyewe tu, bali si kuchambua sifa za mume wako. Kwa mfano, Malkia Esta, alitaka mume wake Mfalme Ahasuero asahihishe kisa fulani cha ukosefu wa haki. Hakumchambua mume wake, bali aliongea naye kwa busara. Mume wake alikubali pendekezo lake na hatimaye alifanya yaliyofaa. (Esta 7:1-4; 8:3-8) Yaelekea mume wako atakupenda sana (1) ukimpa muda ili azoee kuwa kichwa cha familia na (2) ukimtendea kwa heshima hata anapokosea.—Waefeso 5:33.

JARIBU KUFANYA HIVI: Badala ya kukazia mabadiliko ambayo unafikiri mume wako anapaswa kufanya, fikiria mabadiliko ambayo wewe unahitaji kufanya. Waume: Mke wako anapoudhika kwa sababu hukutekeleza majukumu yako kama kichwa cha familia kwa njia inayofaa, muulize jinsi unavyoweza kufanya maendeleo, kisha uandike pendekezo lake. Wake: Mume wako anapohisi kwamba umekosa kumheshimu, muulize jinsi unavyoweza kufanya maendeleo, na uandike pendekezo lake.

Usitarajie Mengi Mno

Kujifunza kudumisha uhusiano wenye furaha na usawaziko katika ndoa ni kama kujifunza kuendesha baiskeli. Unatarajia kuanguka mara kadhaa unapozoea kuiendesha. Vivyo hivyo, bila shaka mara nyingine utaaibika kwa sababu ya kukosea unapoendelea kuzoea maisha ya ndoa.

Jifunze kujicheka unapokosea, lakini usipuuze mahangaiko ya mume au mke wako. Katika mwaka wa kwanza wa ndoa, tafuta nafasi za kumfurahisha mwenzako. (Kumbukumbu la Torati 24:5) Zaidi ya yote, fuata mashauri ya Neno la Mungu katika ndoa yenu. Ukifanya hivyo, ndoa yako itaimarika mwaka baada ya mwaka.

^ fu. 9 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

JIULIZE . . .

  • Je, ninapenda kushauriana na mwenzi wangu wa ndoa kuliko mtu mwingine yeyote?

  • Nimefanya nini katika muda wa saa 24 zilizopita kinachoonyesha kwamba ninampenda na kumheshimu mwenzi wangu wa ndoa?