Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 Mkaribie Mungu

“Mungu Hupenda Mtoaji Mchangamfu”

“Mungu Hupenda Mtoaji Mchangamfu”

Ungethamini zaidi zawadi ya aina gani? Bila shaka, sote tungefurahia kupokea zawadi kutoka kwa mtu anayechochewa na upendo badala ya yule anayetoa ili tu kutimiza wajibu. Inapohusu kutoa zawadi, nia ya mtu ni muhimu sana. Tunapendezwa na nia yake. Na jambo muhimu zaidi ni kwamba Mungu huchunguza nia. Fikiria maneno ya mtume Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu katika kitabu cha 2 Wakorintho 9:7.

Kwa nini mtume Paulo aliandika maneno hayo? Alitaka kuwatia moyo Wakristo huko Korintho wawasaidie waamini wenzao wa Yudea waliokuwa na uhitaji. Je, aliwalazimisha Wakorintho kutoa? La, badala yake aliandika: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” Acheni tuchunguze ushauri wake kwa undani.

“Kama alivyoazimia moyoni mwake.” Paulo anasema kwamba Mkristo mnyoofu hutoa kwa sababu ameamua kutoka “moyoni mwake.” Wakati huo huo, Mkristo hufikiria kwa uzito mahitaji ya waabudu wenzake. Msomi mmoja anasema neno la awali linalomaanisha “azimia” “lina wazo la kukusudia.” Kwa hiyo, Mkristo anafikiria kwa uzito mahitaji ya waamini wenzake na kujiuliza afanye nini ili kuwasaidia.1 Yohana 3:17.

“Si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa.” Paulo alionyesha aina mbili ya utoaji ambao Wakristo wa kweli wanapaswa kuepuka, yaani, kwa kutopenda au kwa kulazimishwa. Neno la Kigiriki linalomaanisha “kutopenda” kihalisi linamaanisha “kwa huzuni (au, majonzi).” Kitabu kimoja cha marejezo kinasema mtu anayetoa kwa kutopenda hutoa “akiwa amehuzunika anapofikiria kwamba anapoteza pesa.” Mtu anayetoa kwa kutopenda hufanya hivyo kwa sababu anahisi kwamba analazimishwa. Ni nani kati yetu ambaye angependa kupokea zawadi kutoka kwa mtu asiyetaka au aliyelazimishwa?

“Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.Paulo anasema kwamba Mkristo anapoamua kutoa anapaswa kutoa kwa uchangamfu, au kwa shangwe. Ndiyo, furaha inatokana na kutoa. (Matendo 20:35) Shangwe ya mtu anayetoa kwa uchangamfu huonekana wazi. Neno “changamfu” linaweza kufafanua shangwe ambayo mtu anahisi na jinsi anavyoonekana kuwa mwenye shangwe. Mtu anayetoa kwa uchangamfu hugusa mioyo yetu. Pia, anaufurahisha moyo wa Mungu. Tafsiri fulani ya Biblia inasema: “Mungu hupenda watu wanaopenda kutoa.”Contemporary English Version.

“Mungu hupenda watu wanaopenda kutoa”

Maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu ni kanuni inayopaswa kuwaongoza Wakristo inapohusu kutoa. Iwe tunatoa muda, nguvu, au mali zetu, acheni tufanye hivyo kwa hiari na kwa sababu tunafurahi kuwaonyesha wengine ukarimu, hasa wale walio na uhitaji. Tukitoa kwa njia hiyo, tutakuwa wenye furaha na pia tutampendeza Mungu kwa kuwa Mungu “humpenda mtoaji mchangamfu.”

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Septemba

Wakorintho wa 1 na wa 2