Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 IGENI IMANI YAO | ELIYA

Alivumilia Licha ya Ukosefu wa Haki

Alivumilia Licha ya Ukosefu wa Haki

ELIYA alitembea kando ya Bonde la Yordani. Alikuwa amesafiri kwa majuma kadhaa akielekea upande wa kaskazini kutoka Mlima Horebu. Sasa, akiwa Israeli, aliona mabadiliko fulani. Ukame ulikuwa umekwisha na hali haikuwa mbaya sana. Majira ya mvua yalikuwa yameanza, na wakulima walikuwa wakilima mashamba yao. Huenda nabii huyo alipata kitulizo kuona mabadiliko hayo, lakini aliwahangaikia hasa watu. Hawakuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Bado ibada ya Baali ilikuwa imeenea, na hivyo Eliya alikuwa na kazi nyingi. *

Akiwa karibu na mji wa Abel-mehola, Eliya aliona watu wakilima katika shamba kubwa. Kulikuwa na ng’ombe-dume 24 waliokuwa wamefungwa wawili-wawili, na vikundi hivyo 12 vilikuwa vikilima kwa pamoja na kuacha mitaro kwenye udongo uliokuwa na unyevunyevu. Eliya alikuwa akimtafuta mwanamume aliyeongoza kundi la mwisho. Aliitwa Elisha, mwanamume ambaye alikuwa amechaguliwa na Yehova achukue mahali pa Eliya. Pindi fulani, Eliya alidhani kwamba yeye tu ndiye mtumishi mshikamanifu wa Mungu aliyekuwa amebaki, kwa hiyo alitamani sana kukutana na mwanamume huyo.—1 Wafalme 18:22; 19:14-19.

Je, Eliya alisita kumpa Elisha majukumu na mapendeleo fulani, au kuhisi vibaya kwa sababu ndiye angechukua mahali pake? Hatujui; wala hatuwezi kusema Eliya hakuhangaishwa na mawazo kama hayo, kwani alikuwa “mtu mwenye hisia kama zetu.” (Yakobo 5:17) Vyovyote vile, Biblia inasema: “Eliya akavuka mpaka pale alipokuwa, akalitupa vazi lake rasmi juu yake.” (1 Wafalme 19:19) Vazi rasmi la Eliya, lililotengenezwa kwa ngozi ya kondoo au mbuzi, lilivaliwa kama joho ili kuonyesha alichaguliwa rasmi na Yehova. Basi, kulitupa juu ya mabega ya Elisha kulikuwa na maana kubwa. Eliya alijitiisha kwa hiari na kukubali amri ya Yehova ya kumchagua rasmi Elisha achukue mahali pake. Eliya alimtegemea na kumtii Mungu wake.

Kwa unyenyekevu, Eliya alimweka rasmi Elisha achukue mahali pake

Elisha alikuwa tayari kumsaidia nabii huyo mwenye umri mkubwa zaidi. Elisha hangechukua mahali pa Eliya mara moja. Badala yake, kwa miaka sita hivi, aliandamana kwa unyenyekevu na nabii huyo mzee akimsaidia, na baadaye akajulikana kama yule “aliyemimina maji juu ya mikono ya Eliya.” (2 Wafalme 3:11) Bila shaka, Eliya alifarijika sana kusaidiwa na mtumishi huyo mwenye uwezo! Inaelekea kwamba wanaume hao wawili walisitawisha urafiki wa karibu! Walitiana moyo na hivyo wakafaulu kuvumilia licha ya ukosefu wa haki uliokuwa umeenea katika nchi hiyo. Hasa walivumilia uovu wa mfalme Ahabu uliozidi kuwa mbaya sana.

Je, umewahi kutendewa isivyo haki? Sote tumewahi kukabili hali hiyo katika ulimwengu huu wenye ufisadi. Ni rahisi zaidi kuvumilia ukiwa na rafiki anayempenda Mungu. Pia, unaweza kujifunza mengi kutoka kwa imani ya Eliya unapokabili ukosefu wa haki.

“ONDOKA, NENDA UKUTANE NA AHABU”

Eliya na Elisha walijitahidi kuwaimarisha watu kiroho. Bila shaka, wao ndio waliozoeza manabii wengine, ambao huenda walikuwa wamepangwa katika vikundi fulani. Hata hivyo, baada ya muda Eliya alipewa jukumu lingine na Yehova: “Ondoka, nenda ukutane na Ahabu mfalme wa Israeli.” (1 Wafalme 21:18) Ahabu alikuwa amefanya nini?

Tayari mfalme huyo alikuwa mwasi-imani na kufikia wakati huo yeye ndiye aliyekuwa mfalme mwovu zaidi katika Israeli. Alikuwa amemwoa Yezebeli, na alikuwa amefanya ibada ya Baali isitawi nchini, hata mfalme mwenyewe alishiriki katika ibada hiyo. (1 Wafalme 16:31-33) Ibada ya Baali ilitia ndani sherehe za mambo ya uzazi, ukahaba, na kuwatoa watoto kuwa dhabihu. Isitoshe, Ahabu alikuwa ametoka tu kupuuza agizo la Yehova la kumwangamiza Ben-hadadi, mfalme mwovu wa Siria. Ahabu alikaidi agizo hilo kwa sababu alitazamia kufaidika kifedha. (1 Wafalme, sura ya 20) Hata hivyo, sasa pupa, tamaa ya kupata mali, na ujeuri wa Ahabu na Yezebeli ulikuwa umekita mizizi.

Ahabu alikuwa na makao ya kifalme huko Samaria— na lilikuwa jengo kubwa kwelikweli! Pia, alikuwa na makao mengine huko Yezreeli, kilomita 37 hivi kutoka Samaria. Kando ya makao yake huko Yezreeli, kulikuwa na shamba la mizabibu. Ahabu alitamani sana shamba hilo lililokuwa la mwanamume aliyeitwa Nabothi. Ahabu alimwita na akaahidi kumpa pesa au shamba lingine. Lakini Nabothi alimwambia: “Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba mimi nikupe fungu la urithi la mababu zangu.” (1 Wafalme 21:3) Je, Nabothi alikuwa na kichwa kigumu? Au alikuwa akihatarisha uhai wake? Wengi wamefikiri hivyo. Kwa kweli, alikuwa akitii Sheria ya Yehova ambayo iliwakataza Waisraeli kuuza mashamba waliyokuwa wamerithi kutoka kwa mababu zao. (Mambo ya Walawi 25:23-28) Nabothi hangeweza kamwe kuvunja Sheria ya Mungu. Alikuwa mwanamume mwenye imani na ujasiri, kwani alijua lilikuwa jambo hatari kukataa ombi la Ahabu.

Bila shaka, Ahabu alipuuza Sheria ya Yehova. Alirudi nyumbani “akiwa mwenye kinyongo na mwenye huzuni” kwa sababu hakupata alichotaka. Tunasoma hivi: “Akalala kitandani pake, akakaa akiwa amegeuza uso wake, naye hakula mkate.” (1 Wafalme 21:4) Yezebeli alipoona mumewe akiwa amenuna kama mtoto, alitunga njama mara moja ili amsaidie kupata alichotaka, na wakati huohuo kuangamiza familia isiyo na hatia.

Tunaposoma kuhusu njama yake, tunashangaa kuona jinsi alivyokuwa mwovu. Malkia Yezebeli alijua kwamba Sheria ya Mungu ilitaka ushahidi wa watu wawili ili kuthibitisha makosa mazito. (Kumbukumbu la Torati 19:15) Basi, akaandika barua kwa jina la Ahabu, akiwaagiza wanaume wenye vyeo wa Yezreeli watafute wanaume wawili ambao wangetoa mashtaka ya uwongo dhidi ya Nabothi, kwamba alikuwa amekufuru, kosa ambalo adhabu yake ilikuwa kifo. Kwa kusikitisha, njama yake ilifaulu. Wanaume wawili “wasiofaa kitu”  walitoa ushahidi wa uwongo dhidi ya Nabothi, na akapigwa mawe hadi akafa. Isitoshe, wana wa Nabothi waliuawa pia! * (1 Wafalme 21:5-14; Mambo ya Walawi 24:16; 2 Wafalme 9:26) Ahabu alikuwa amepuuza majukumu yake na kumruhusu mkewe afanye alivyotaka kwa kuangamiza watu wasio na hatia.

Wazia jinsi Eliya alivyohisi baada ya Yehova kumfunulia jambo ambalo mfalme na malkia walikuwa wamefanya. Inasikitisha kuona watu waovu wakifanikiwa na kuwakandamiza wasio na hatia. (Zaburi 73:3-5, 12, 13) Leo, mara nyingi tunaona ukosefu mkubwa wa haki ukifanywa na watu wenye nguvu ambao wanadai wanamwakilisha Mungu. Hata hivyo, simulizi hili linaweza kutufariji. Biblia inatukumbusha kwamba hakuna kitu kilichojificha machoni pa Yehova. Anaona kila kitu. (Waebrania 4:13) Anachukua hatua gani kuelekea uovu?

“JE, UMENIPATA, EWE ADUI YANGU?”

Yehova alimtuma Eliya kwa Ahabu. Mungu alisema hivi waziwazi: “Tazama, yupo katika shamba la mizabibu la Nabothi.” (1 Wafalme 21:18) Yezebeli alipomwambia Ahabu kwamba sasa shamba la mizabibu ni lake, aliinuka na kwenda kufurahia mali hiyo. Hakudhani kwamba Yehova alikuwa akitazama. Hebu mwazie akiwa katika shamba hilo, akiwazia jinsi ambavyo angetengeneza bustani maridadi. Lakini ghafula, Eliya akatokea! Mara moja Ahabu akakasirika na kuuliza: “Je, umenipata, ewe adui yangu?”1 Wafalme 21:20.

“Je, umenipata, ewe adui yangu?”

Maneno ya Ahabu yanafunua makosa mawili. Kwanza alipomwambia Eliya “Umenipata,” Ahabu alifunua kwamba hakuwa akimfikiria Yehova. Tayari Yehova alikuwa ‘amempata.’ Alikuwa ameona Ahabu akifanya uovu kwa hiari na kufurahia matokeo ya njama ya Yezebeli. Mungu alikuwa amechunguza moyo wa Ahabu na kuona kwamba alipenda vitu vya kimwili, na hakuwa na huruma wala haki. Pili, alipomwita Eliya “ewe adui yangu,” Ahabu alifunua jinsi alivyomchukia mwanamume aliyekuwa rafiki ya Yehova Mungu na ambaye angemsaidia Ahabu abadili njia yake mbaya.

Tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na makosa ya Ahabu. Sikuzote tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova anaona kila kitu. Akiwa Baba mwenye upendo, anajua tunapoiacha njia  inayofaa, na anatamani kuona tukifanya mabadiliko. Ili kutusaidia, mara nyingi anatumia rafiki zake, yaani, wanadamu waaminifu ambao, kama Eliya, wanatangaza ujumbe wa Mungu. Kwa hiyo, ni kosa kuwaona rafiki za Mungu kama adui zetu!—Zaburi 141:5.

Mwazie Eliya akimjibu hivi Ahabu: “Nimekupata.” Alijua Ahabu alikuwa mwizi, muuaji, na alikuwa amemwasi Yehova Mungu. Alihitaji ujasiri mwingi ili kuzungumza na mwanamume huyo mwovu! Hata hivyo, Eliya alimtangazia Ahabu hukumu ya Mungu. Yehova aliona jinsi uovu ulivyokuwa ukianzia kwenye familia ya Ahabu na kuenea kwa watu wengine. Basi, Eliya akamwambia Ahabu kwamba Mungu alikusudia ‘kufagia kabisa,’ yaani, kuangamiza familia hiyo ya kifalme. Yezebeli pia angeadhibiwa.—1 Wafalme 21:20-26.

Eliya hakuwazia watu wanaweza kuepuka adhabu wanapotenda maovu au kutenda isivyo haki. Ni rahisi kufikiria hivyo katika ulimwengu huu. Simulizi hili la Biblia linatufundisha kwamba Yehova Mungu anaona mambo yote na atatekeleza hukumu hivi karibuni. Neno lake linatuhakikishia kwamba hivi karibuni atakomesha kabisa ukosefu wote wa haki! (Zaburi 37:10, 11) Huenda ukajiuliza hivi: ‘Je, hukumu ya Mungu inahusisha adhabu tu? Au inahusisha pia rehema?’

“JE, UMEONA JINSI AMBAVYO AHABU AMEJINYENYEKEZA?”

Labda Eliya alishangaa kuona jinsi Ahabu alivyotenda aliposikia hukumu ya Mungu. Simulizi hilo linasema: “Mara tu Ahabu alipoyasikia maneno hayo, akayararua mavazi yake, akavaa nguo za magunia mwilini mwake; naye akaanza kufunga, akaendelea kulala katika nguo za magunia, akatembea kwa huzuni.” (1 Wafalme 21:27) Je, Ahabu alikuwa akitubu makosa yake?

Tunachoweza kusema ni kwamba alichukua hatua inayofaa. Ahabu alikuwa akijinyenyekeza, naam, lilikuwa jambo gumu kwa mtu mwenye kiburi na majivuno. Lakini je, alitubu kikweli? Hebu mlinganishe na Manase, mfalme aliyetawala baadaye ambaye huenda alikuwa mwovu kuliko Ahabu. Yehova alipomwadhibu Manase, alijinyenyekeza na kumwomba Mungu amsaidie. Alifanya mengi zaidi. Alibadili njia zake kwa kuondoa sanamu alizokuwa ametengeneza, akajitahidi kumtumikia Yehova, na hata aliwahimiza watu wafanye vivyo hivyo. (2 Mambo ya Nyakati 33:1-17) Je, Ahabu alitenda hivyo? La, hasha.

Je, Yehova aliona jinsi Ahabu alivyoonyesha huzuni yake hadharani? Yehova alimwambia hivi Eliya: “Je, umeona jinsi ambavyo Ahabu amejinyenyekeza kwa ajili yangu? Kwa sababu amejinyenyekeza kwa ajili yangu, sitauleta ule msiba katika siku zake. Katika siku za mwana wake nitauleta msiba ule juu ya nyumba yake.” (1 Wafalme 21:29) Je, Yehova alikuwa akimsamehe Ahabu? La, angemsamehe ikiwa tu angetubu kikweli. (Ezekieli 33:14-16) Lakini kwa vile Ahabu alijuta kwa kadiri fulani, Yehova alimwonyesha rehema kwa kadiri hiyohiyo. Ahabu hangeona familia yake yote ikiangamizwa.

Lakini bado Yehova angemwadhibu Ahabu. Baadaye Yehova alizungumza na malaika kuhusu njia bora ya kumdanganya Ahabu ili aende vitani ambako angeuawa. Hatimaye, adhabu ya Yehova juu ya Ahabu ikatekelezwa. Ahabu alijeruhiwa vitani, akavuja damu na kufa akiwa kwenye gari lake la vita. Simulizi hilo linaongezea jambo hili lenye kuhuzunisha: Gari hilo la vita lilipooshwa, mbwa waliiramba damu ya mfalme. Hivi ndivyo hukumu ya Yehova iliyotangazwa na Eliya juu ya Ahabu ilivyotimizwa, alikuwa amesema: “Mahali ambapo mbwa waliiramba damu ya Nabothi, mbwa watairamba damu yako.”1 Wafalme 21:19; 22:19-22, 34-38.

Kwa Eliya, Elisha, na kwa watumishi waaminifu wa Yehova leo, mwisho wa Ahabu unatuhakikishia kwamba Yehova hakusahau kamwe ujasiri na imani ya Nabothi. Mungu wa haki hakosi kamwe kuwaadhibu waovu, iwe ni papo hapo au baadaye; wala hakosi kuonyesha rehema katika hukumu yake kunapokuwa na sababu ya kufanya hivyo. (Hesabu 14:18) Hilo lilikuwa somo muhimu kama nini kwa Eliya, aliyekuwa amevumilia kwa miaka mingi utawala wa mfalme huyo mwovu! Je, umewahi kutendewa isivyo haki? Je, unatamani kuona Mungu akitekeleza haki? Ni jambo la hekima kuiga imani ya Eliya. Akiwa pamoja na nabii mwenzake mwaminifu Elisha, aliendelea kutangaza ujumbe wa Mungu, huku akivumilia ukosefu wa haki!

^ fu. 3 Yehova alikuwa ametumia ukame wa miaka mitatu na nusu kufunua kwamba Baali hakuwa na nguvu, kwa kuwa waabudu wa Baali waliamini yeye ndiye aliyeleta mvua na mazao. (1 Wafalme, sura ya 18) Ona makala “Igeni Imani Yao”katika Januari 1 na April 1, 2008, gazeti Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 13 Kama Yezebeli aliogopa shamba hilo la mizabibu lingepewa warithi wa Nabothi, basi huenda hilo ndilo lililomchochea kupanga wana wa Nabothi wauawe. Ili kujua kwa nini Mungu anaruhusu ukandamizaji, soma makala “Wasomaji Wetu Wanauliza” katika gazeti hili.