Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI

Alitetea Ibada Safi

Alitetea Ibada Safi

1, 2. (a) Watu katika siku za Eliya walitesekaje? (b) Eliya alikabili upinzani gani kwenye Mlima Karmeli?

ELIYA aliutazama umati uliokuwa ukipanda polepole Mlima Karmeli. Ingawa ilikuwa asubuhi na mapema, watu walionekana kuwa maskini na wenye njaa. Hali yao ilizorota sana kwa sababu ya ukame wa miaka mitatu na nusu.

2 Kati yao manabii 450 wa Baali walitembea kwa majivuno, wakiwa na chuki kali kumwelekea Eliya, nabii wa Yehova. Ingawa Malkia Yezebeli alikuwa amewaua watumishi wengi wa Yehova, bado mwanamume huyo alipinga ibada ya Baali kwa uthabiti. Lakini angeendelea kupinga kwa muda gani? Huenda makuhani hao walifikiri kwamba mtu mmoja hangeweza kamwe kuwashinda. (1 Fal. 18:4, 19, 20) Mfalme Ahabu pia alikuwa amekuja kwa gari lake la kifalme. Yeye vilevile hakumpenda Eliya.

3, 4. (a) Kwa nini huenda Eliya alihisi woga siku muhimu ilipozidi kupambazuka? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Siku hiyo ingekuwa ya pekee sana kwa nabii huyo aliyekuwa peke yake. Eliya alitazama watu wakikusanyika ili kujionea mapambano yenye kustaajabisha zaidi kati ya wema na uovu. Alihisije siku ilipozidi kupambazuka? Aliogopa kwa sababu alikuwa “mtu mwenye hisia kama zetu.” (Soma Yakobo 5:17.) Tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hili: Akiwa amezungukwa na watu wasio na imani, mfalme wao mwasi, na makuhani wauaji, Eliya alijihisi akiwa peke yake kabisa.​—1 Fal. 18:22.

4 Hata hivyo, ni nini kilichowaingiza Waisraeli katika msiba huo? Na simulizi hili linakuhusuje? Chunguza jinsi Eliya alivyoonyesha imani na vile tunavyoweza kumwiga leo.

Mapambano ya Muda Mrefu Yafikia Upeo

5, 6. (a) Waisraeli walijipata katika mapambano gani? (b) Mfalme Ahabu alikuwa amemkoseaje Yehova?

5 Kwa muda mrefu, Eliya alitazama jambo bora zaidi katika nchi yao likipuuzwa na kudharauliwa, na hangeweza kufanya chochote. Waisraeli walikuwa katika mapambano ya muda mrefu, vita kati ya ibada safi na ibada ya uwongo, kati ya ibada ya Yehova Mungu na ibada ya sanamu za mataifa yaliyowazunguka. Katika siku za Eliya, mapambano hayo yalikuwa makali zaidi.

6 Mfalme Ahabu alikuwa amemkosea sana Yehova. Alimwoa Yezebeli, binti ya mfalme wa Sidoni. Yezebeli aliazimia kueneza ibada ya Baali katika nchi ya Israeli na kuifagilia mbali ibada ya Yehova. Ahabu alikubali haraka kushawishiwa na Yezebeli. Alijenga hekalu na madhabahu kwa ajili ya Baali naye akaongoza katika kumwinamia mungu huyo wa kipagani.—1 Fal. 16:30-33.

7. (a) Kwa nini ibada ya Baali ilichukiza sana? (b) Kuhusiana na urefu wa ukame katika siku za Eliya kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Biblia haijipingi? (Tia ndani sanduku.)

7 Kwa nini ibada ya Baali ilichukiza sana? Iliwashawishi Waisraeli, na kufanya wengi wamwache Mungu wa kweli. Pia, ilikuwa dini yenye upotovu na ukatili. Ilihusisha makahaba wa kiume na wa kike wa hekaluni, sherehe za ngono, na hata kuwatoa watoto dhabihu. Yehova alichukua hatua kwa kumtuma Eliya kwa Ahabu amtangazie kwamba kungekuwa na ukame mpaka nabii wa Mungu atakapotangaza mwisho wake. (1 Fal. 17:1) Miaka kadhaa ilipita kabla Eliya kujitokeza mbele ya Ahabu na kumwambia awakusanye watu na manabii wa Baali kwenye Mlima Karmeli. *

Kwa njia fulani, mambo mengi yaliyohusiana na ibada ya Baali yanasitawi leo

8. Simulizi kuhusu Baali lina maana gani kwetu leo?

8 Lakini, mapambano hayo yana maana gani kwetu leo? Huenda watu fulani wakafikiri kwamba hadithi kuhusu ibada ya Baali haituhusu leo, kwa kuwa hatuzungukwi na mahekalu na madhabahu ya Baali. Lakini simulizi hili si historia ya zamani tu. (Rom. 15:4) Neno “Baali” linamaanisha “mmiliki” au “bwana.” Yehova aliwaambia watu wake kwamba wanapaswa kumchagua kuwa “baali” wao, au mume wao. (Isa. 54:5) Je, hukubali kwamba bado watu hutumikia mabwana wengi badala ya Mungu Mweza-Yote? Iwe watu wanatumia maisha yao kutafuta pesa, kazi, burudani, raha ya ngono, au kutumikia miungu mingi sana inayoabudiwa leo badala ya Yehova, kwa kweli wanamchagua bwana fulani. (Mt. 6: 24; soma Waroma 6: 16.) Hivyo, kwa njia fulani, mambo mengi yaliyohusiana na ibada ya Baali yanasitawi leo. Kutafakari mapambano hayo ya zamani kati ya Yehova na Baali yanaweza kutusaidia kuchagua kwa hekima yule tutakayemtumikia.

‘Kuyumba-Yumba’—Jinsi Gani?

9. (a) Kwa nini Mlima Karmeli ulikuwa mahali panapofaa pa kufunua wazi ibada ya Baali? (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Eliya aliwaambia watu nini?

9 Mtu akiwa kwenye kilele cha Mlima Karmeli, angeweza kuona mbali sana—kuanzia bonde la Kishoni mpaka kwenye Bahari Kuu (Bahari ya Mediterania) iliyo karibu, na milima ya Lebanoni upande wa mbali wa kaskazini. * Lakini jua lilipochomoza siku hiyo ya pekee, nchi ilikuwa katika hali mbaya sana. Nchi yenye rutuba ambayo Yehova alikuwa amewapa wazao wa Abrahamu ilikuwa imekauka. Sasa nchi hiyo ilikuwa imepigwa na jua kali na kuharibika kwa sababu ya upumbavu wa watu wa Mungu! Watu hao walipokusanyika, Eliya aliwakaribia na kusema: “Mtayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti mpaka wakati gani? Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni yeye; lakini ikiwa ni Baali, mfuateni yeye.”​—1 Fal. 18:21.

10. Ni jinsi gani watu katika siku za Eliya ‘waliyumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti,’ na walikuwa wamesahau kweli gani muhimu?

10 Eliya alimaanisha nini aliposema kuhusu ‘kuyumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti’? Watu hao hawakutambua kwamba walipaswa kuchagua kati ya ibada ya Yehova na ibada ya Baali. Walifikiri wangeweza kushiriki ibada zote mbili, yaani, kumfurahisha Baali kwa desturi zao zenye kuchukiza na bado waombe baraka kutoka kwa Yehova Mungu. Labda walifikiri kwamba Baali angebariki mimea na mifugo yao, huku “Yehova wa majeshi” akiwalinda vitani. (1 Sam. 17:45) Walikuwa wamesahau kweli fulani ya msingi—ambayo bado wengi leo hawaitambui. Yehova hachanganyi ibada yake na ibada nyingine. Anataka na anastahili ujitoaji kamili. Kuchanganya ibada yake na ibada nyingine ni jambo lisilokubalika machoni pake na hata linamchukiza!​—Soma Kutoka 20:5.

11. Unafikiri himizo la Eliya kwenye Mlima Karmeli linaweza kutusaidiaje kuchunguza tena ibada yetu na mambo tunayotanguliza?

11 Hivyo, Waisraeli hao ‘waliyumba-yumba’ kama mtu anayejaribu kufuata barabara mbili wakati uleule. Leo watu wengi hufanya kosa hilo, kwa kuruhusu “mabaali” wengine waingilie maisha yao, na kupuuza ibada ya Mungu wa kweli. Kufuata himizo la Eliya la kuacha kuyumba-yumba linaweza kutusaidia kuchunguza tena ibada yetu na mambo tunayotanguliza.

Jaribu la Kukata Maneno

12, 13. (a) Eliya alipendekeza wafanye jaribio gani? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba tuna uhakika kama wa Eliya?

12 Kisha, Eliya akapendekeza wafanye jaribu fulani. Lilikuwa rahisi sana. Makuhani wa Baali walipaswa kujenga madhabahu na kuweka dhabihu juu yake; kisha wamwombe mungu wao awashe moto. Eliya angefanya vivyo hivyo. Alisema hivi: ‘Mungu atakayejibu kupitia moto, huyo ndiye Mungu wa kweli.’ Eliya alijua ni nani aliyekuwa Mungu wa kweli. Alikuwa na imani yenye nguvu sana. Hata aliwaruhusu wapinzani wake watangulie. Basi, wakachagua ng’ombe-dume kwa ajili ya dhabihu yao, na kumwomba Baali. *1 Fal. 18:24, 25.

13 Leo hatuishi katika enzi za miujiza. Hata hivyo, Yehova hajabadilika. Tunaweza kumtegemea kama Eliya alivyofanya. Kwa mfano, watu wanapopinga mafundisho ya Biblia, tunapaswa kuwaruhusu watoe maoni yao. Kama Eliya, tunaweza kumtegemea Mungu wa kweli ashughulikie hali hiyo. Tunafanya hivyo kwa kutojitegemea, bali kwa kutegemea Neno lake lililoongozwa kwa roho, na ambalo limekusudiwa “kunyoosha mambo.”​—2 Tim. 3:16.

Eliya aliiona ibada ya Baali kuwa udanganyifu mtupu, na alitaka watu wa Mungu waone udanganyifu huo

14. Eliya aliwadhihaki jinsi gani manabii wa Baali, na kwa nini?

14 Manabii wa Baali walitayarisha dhabihu yao na kumwita mungu wao. Walirudia-rudia kupaaza sauti hivi: “Ee Baali, tupe jibu!” Walizidi kufanya hivyo kadiri wakati ulivyosonga. “Lakini hapakuwa na sauti yoyote, wala hakuna yeyote aliyetoa jibu,” Biblia inasema. Ilipofika saa sita mchana, Eliya akaanza kuwadhihaki na kuwatania kwamba hapana shaka Baali ana shughuli nyingi asiweze kuwajibu, ameenda chooni, au amelala na hivyo anapaswa kuamshwa. “Iteni kwa sauti kubwa,” Eliya akawahimiza wanafiki hao. Ni wazi kwamba aliiona ibada ya Baali kuwa udanganyifu mtupu, na alitaka watu wa Mungu waone udanganyifu huo.​—1 Fal. 18:26, 27.

15. Kisa cha makuhani wa Baali kinaonyeshaje upumbavu wa kuchagua bwana mwingine badala ya Yehova?

15 Kwa sababu hiyo, makuhani wa Baali wakawa na wazimu hata zaidi, “wakaanza kuita kwa sauti yao yote, wakijikatakata kwa visu na mikuki kulingana na desturi yao, mpaka walipojitiririsha damu.” Lakini hawakufanikiwa! “Hapakuwa na sauti yoyote, wala hapakuwa na yeyote aliyejibu, wala aliyewasikiliza.” (1 Fal. 18:28, 29) Kwa kweli, Baali hakuwepo. Ilikuwa mbinu ya Shetani ya kuwageuza watu wasimwabudu Yehova. Ukweli ni kwamba mtu akichagua bwana mwingine badala ya Yehova atavunjika moyo na hata kuaibika.​—Soma Zaburi 25:3; 115:4-8.

Jibu Lapatikana

16. (a) Huenda Eliya aliwakumbusha watu nini aliporekebisha madhabahu ya Yehova kwenye Mlima Karmeli? (b) Eliya alionyeshaje tena kwamba alikuwa na uhakika na Mungu wake?

16 Baadaye jioni, zamu ya Eliya ya kutoa dhabihu ikafika. Alirekebisha madhabahu ya Yehova ambayo bila shaka ilikuwa imebomolewa na maadui wa ibada safi. Alitumia mawe 12, labda ili kuwakumbusha wengi katika taifa la Israeli lenye makabila 10 kwamba bado walipaswa kutii Sheria ambayo makabila yote 12 yalipewa. Kisha, akatayarisha dhabihu yake na akaagiza imwagiwe maji, ambayo labda yalichotwa katika Bahari ya Mediterania iliyokuwa karibu. Hata aliagiza mtaro uchimbwe kuzunguka madhabahu hiyo na akaujaza maji. Ingawa alirahisisha sana mambo kwa manabii wa Baali, alifanya jaribu la Yehova liwe gumu kabisa—kwa kweli alikuwa na uhakika na Mungu wake.​—1 Fal. 18:30-35.

Sala ya Eliya ilionyesha kwamba bado aliwajali watu, kwa sababu alitamani sana kuona Yehova akigeuza “moyo wao urudi”

17. Sala ya Eliya ilifunuaje mambo aliyotanguliza, na tunawezaje kuiga mfano wake tunaposali?

17 Kila kitu kilipokuwa tayari, Eliya alisali. Ilikuwa sala fupi yenye ufasaha, na ilionyesha wazi mambo ambayo Eliya alitanguliza. Kwanza kabisa, alitaka watu wajue kwamba Yehova ndiye “Mungu katika Israeli” na si Baali. Pili, alitaka kila mtu ajue kwamba alikuwa mtumishi wa Yehova; kwamba Mungu ndiye aliyestahili kupewa sifa na utukufu wote. Mwishowe, alionyesha kwamba bado aliwajali watu, kwa sababu alitamani sana kuona Yehova akigeuza “moyo wao urudi.” (1 Fal. 18:36, 37) Ingawa walikuwa wamejiletea taabu kubwa kwa kukosa uaminifu, bado Eliya aliwapenda. Tunaposali, je, sisi pia tunaweza kuonyesha unyenyekevu kama huo, kuhangaikia jina la Mungu, na kuwahurumia watu wanaoteseka?

18, 19. (a) Yehova alijibuje sala ya Eliya? (b) Eliya aliwaagiza watu wafanye nini, na kwa nini makuhani wa Baali hawakupaswa kuhurumiwa?

18 Kabla Eliya hajasali, huenda umati ulijiuliza kama Yehova angekuwa mdanganyifu kama Baali alivyokuwa. Hata hivyo, jibu lilipatikana mara tu baada ya sala hiyo. Simulizi hilo linasema hivi: “Ndipo moto wa Yehova ukashuka, ukala lile toleo la kuteketezwa na zile kuni na mawe na mavumbi, nao ukaramba maji yaliyokuwa katika mtaro.” (1 Fal. 18:38) Lilikuwa jibu la kustaajabisha kama nini! Nao watu waliitikiaje?

“Ndipo moto wa Yehova ukashuka”

19 “Yehova ndiye Mungu wa kweli! Yehova ndiye Mungu wa kweli!” wote wakapaaza sauti. (1 Fal. 18:39) Mwishowe walijionea ukweli. Hata hivyo, bado hawakuwa wameonyesha imani yao. Kukubali kwa sauti kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli baada ya kuona akishusha moto kutoka mbinguni alipojibu sala, hakukutosha kuthibitisha imani yao. Hivyo, Eliya akawataka waonyeshe imani yao kwa njia nyingine. Aliwaambia wafanye jambo ambalo walipaswa kufanya miaka mingi mapema—kutii Sheria ya Yehova. Sheria ya Mungu ilisema kwamba manabii wa uwongo na waabudu-sanamu walipaswa kuuawa. (Kum. 13: 5-9) Makuhani hao wa Baali walikuwa maadui sugu wa Yehova Mungu, na walimpinga kimakusudi. Je, walistahili kuhurumiwa? Jiulize hivi, je, waliwahurumia watoto wasio na hatia walioteketezwa wakiwa hai kama dhabihu kwa Baali? (Soma Methali 21:13; Yer. 19:5) Wanaume hao hawakustahili kuhurumiwa! Hivyo, Eliya akaagiza wauawe, na kwa kweli waliuawa.​—1 Fal. 18:40.

20. Kwa nini wachambuzi hawana sababu nzuri za kukosoa hatua ya Eliya ya kuwaua makuhani wa Baali?

20 Leo, huenda wachambuzi wakakosoa hatua hiyo ya mwisho kwenye Mlima Karmeli. Huenda wengine wakaogopa kwamba wanadini wenye msimamo mkali wanaweza kutumia kisa hicho kutetea ujeuri unaotegemea imani za kidini. Na inasikitisha kwamba leo kuna wanadini wengi wajeuri. Hata hivyo, Eliya hakuwa mtu mwenye msimamo mkali. Alimtetea Yehova kwa kutekeleza hukumu ya haki. Zaidi ya hilo, Wakristo wa kweli wanajua hawawezi kufuata mfano wa Eliya na kuwaua watu waovu. Badala yake, wanafuata amri ambayo wanafunzi wote wa Yesu walipewa inayopatikana katika maneno haya ya Yesu kwa Petro: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mt. 26:52) Wakati ujao, Yehova atamtumia Mwana wake kutekeleza haki.

21. Kwa nini leo Wakristo wanapaswa kuiga mfano wa Eliya?

21 Wajibu wa Mkristo wa kweli ni kuishi kupatana na imani. (Yoh. 3:16) Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwaiga wanaume waaminifu kama Eliya. Alimwabudu Yehova kikamili na akawahimiza wengine wafanye hivyo pia. Alifunua kwa ujasiri udanganyifu wa dini ambayo Shetani alitumia ili kufanya watu wasimwabudu Yehova. Na alimtegemea Yehova ashughulikie mambo badala ya kujitegemea mwenyewe. Eliya aliitetea ibada safi. Acheni sote tuige imani yake!

^ fu. 9 Kwa kawaida Mlima Karmeli huwa na mimea mingi, kwa sababu pepo zenye unyevunyevu kutoka baharini hupanda juu ya mabonde yake na kutokeza mvua na umande kwa wingi. Kwa kuwa Baali alionwa kuwa ndiye aliyeleta mvua, mlima huo ulikuwa kituo muhimu cha ibada ya Baali. Mlima Karmeli uliokauka ulikuwa mahali panapofaa pa kufunua ibada ya Baali kuwa ya udanganyifu.

^ fu. 12 Inapendeza kwamba Eliya aliwaambia: “Msiwashe moto” ili kuteketeza dhabihu. Wasomi fulani wanasema nyakati nyingine waabudu hao wa sanamu walitumia madhabahu yaliyokuwa na mwanya uliofichika chini ili ionekane kwamba moto uliwaka kimuujiza.