Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 IGENI IMANI YAO | YOSEFU

“Ninawezaje Kufanya Ubaya Huu Mkubwa?”

“Ninawezaje Kufanya Ubaya Huu Mkubwa?”

YOSEFU anavuta hewa nzito yenye joto, anasikia harufu ya maua ya mayungiyungi yanayochanua na mimea mingine ya majini. Alikuwa akiongozwa na msafara wa wafanyabiashara, wakisafiri katika eneo tambarare la delta ya mto Nile. Wazia msururu wa watu wakiongoza ngamia wao kando ya mto kuelekea mji mwingine wa Misri, mara kwa mara wanamshitua ndege wa majini aina ya kulasitara na kusababisha kwarara kuruka. Yosefu anakumbuka tena nyumbani kwao eneo lenye upepo na milima la Hebroni, mamia ya kilomita, sasa alikuwa eneo tofauti kabisa.

Wazia tumbili wakipiga kelele juu ya miti ya mitende na tini. Yosefu hakuelewa lugha ya watu wa nchi hiyo. Huenda alijaribu kuelewa maneno kadiri alivyoweza. Alipaswa kujifunza. Alifikiri hangerudi nyumbani kamwe.

Yosefu alikuwa kijana tu mwenye umri wa miaka 17 au 18—lakini alikabili magumu ambayo yangeweza kuwavunja moyo watu wazima. Ndugu zake, walimwonea wivu kwa sababu Yosefu alipendwa sana na baba yake, hata walikuwa karibu kumuua. Badala ya kumuua walimuuza kwa wafanyabiashara hao. (Mwanzo 37:2, 5, 18-28) Sasa, baada ya kusafiri kwa majuma kadhaa, wafanyabiashara hao wanafurahi wanapozidi kukaribia jiji kubwa mahali wanakokusudia kupata faida kubwa kwa kumuuza Yosefu pamoja na bidhaa zao za thamani. Ni nini kilichomsaidia Yosefu kutovunjika moyo na kukata tamaa? Na tunawezaje kukabiliana na hali ngumu na mambo yenye kuvunja moyo maishani bila kudhoofisha imani yetu? Tuna mambo mengi ya kujifunza kutoka kwa Yosefu.

“YEHOVA ALIKUWA PAMOJA NA YOSEFU”

“Basi Yosefu akapelekwa Misri, na Potifa, ofisa wa makao ya Farao, mkuu wa walinzi, Mmisri, akamnunua kutoka kwa Waishmaeli waliokuwa wamemleta huko.” (Mwanzo 39:1) Kwa maneno hayo machache, simulizi la Biblia linatusaidia kuwazia aibu ya mvulana huyo akiuzwa kwa mara nyingine tena. Alikuwa kama bidhaa tu! Tumfikirie Yosefu akimfuata bwana wake mpya, ofisa wa makao ya mfalme wa Misri, katikati ya jiji lenye shughuli nyingi na mitaa iliyojaa masoko wakielekea makao mapya ya Yosefu.

Hatimaye wakafika! Mahali tofauti kabisa na nyumbani kwao. Alilelewa katika familia yenye kuhama-hama na waliishi kwenye mahema na kuchunga makundi yao ya kondoo. Lakini hapa matajiri Wamisri kama Potifa waliishi katika nyumba zilizopakwa rangi nyangavu. Wachimbuaji wa vitu vya kale wanasema kwamba Wamisri wa kale walipenda anasa, kulikuwa na bustani zilizozungushwa ukuta pamoja na miti ya kivuli na visima vilivyotumiwa kukuza mafunjo, mayungiyungi na mimea mingine ya majini. Nyumba nyingine zilijengwa ndani ya bustani, pamoja na varanda kwa ajili ya kupunga upepo, madirisha makubwa ya kupitishia hewa, na vyumba vingi kutia ndani chumba kikubwa cha kulia chakula na nyumba za watumishi.

Je, Yosefu alivutiwa sana na starehe hizo? Inaonekana sivyo. Zaidi ya yote, inaelekea alijihisi upweke sana. Kulikuwa na tofauti kati yake na Wamisri katika lugha, mavazi na mapambo, na hasa dini. Waliabudu miungu mbalimbali ya uwongo,  walizoea kufanya mazingaombwe na ufundi wa uchawi, na walivutiwa na kifo na maisha baada ya kifo. Hata hivyo kuna jambo lililomfanya Yosefu asilemewe na upweke. Simulizi la Biblia linatuambia hivi: “Yehova alikuwa pamoja na Yosefu.” (Mwanzo 39:2) Kwa hakika Yosefu alimweleza Mungu hisia zake. Biblia inasema kwamba “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.” (Zaburi 145:18) Ni jambo gani lingine lililomfanya Yosefu awe karibu na Mungu wake?

Kijana huyo hakujiruhusu avunjike moyo, alifanya kazi yake kulingana na uwezo wake. Kwa kufanya hivyo alimpa Yehova nafasi ya kumbariki, na Yosefu akapata kibali cha bwana wake mpya. Potifa aliona kwamba mtumishi wake anabarikiwa na Yehova, Mungu wa watu wa Yosefu, na bila shaka baraka hizo zilileta mafanikio makubwa katika nyumba ya Mmisri huyo. Yosefu akazidi kupata heshima machoni pa bwana wake hata Potifa akaviweka vitu vyote mikononi mwa kijana huyo mwenye uwezo.—Mwanzo 39:3-6.

Yosefu ni mfano mzuri sana kwa vijana wanamtumikia Mungu leo. Kwa mfano, wanapokuwa shuleni, nyakati nyingine wanaweza kujikuta katika mazingira magumu na mageni ya watu wanaopenda uchawi na wasio na tumaini maishani. Ikiwa uko katika hali hiyo, kumbuka kwamba Yehova hajabadilika. (Yakobo 1:17) Bado yuko pamoja na wale wote wanaobaki washikamanifu kwake na wale wanaofanya kazi kwa bidii na kwa njia inayompendeza. Yeye huwabariki sana, na atakubariki wewe pia.

Simulizi hilo linatuambia kwamba, Yosefu akakua. Akawa mwanamume, “mwenye umbo zuri na sura ya kupendeza.” Maneno hayo yanadokeza hatari iliyokuwa mbele yake, kuwa na sura nzuri mara nyingi huleta uangalifu usiofaa.

Mke wa Potifa alitambua kwamba Yosefu alikuwa mwaminifu

“HAKUMSIKILIZA KAMWE”

Yosefu alikuwa mshikamanifu; hata hivyo mke wa Potifa hakuwa mshikamanifu. Tunasoma hivi: “Mke wa bwana wake akaanza kuinua macho yake kumwelekea Yosefu na kusema: ‘Lala nami.’” (Mwanzo 39:7) Je, Yosefu alikubali ushawishi wa mwanamke huyo mpagani? Biblia haitupi sababu yoyote ya kufikiri kwamba Yosefu hakuwa na tamaa kama ya vijana wengine, au kwamba mwanamke huyo aliyeendekezwa, aliyekuwa na mume tajiri na mashuhuri, hakuwa mrembo. Je, Yosefu angepunguza uzito wa kosa kwa kusema kwamba bwana wake hangejua kamwe? Je, angeshawishiwa na faida za kimwili ambazo angepata kwa kufanya ngono na mwanamke huyo?

Kwa kweli, hatuwezi kujua mambo yote aliyokuwa akifikiria Yosefu. Lakini tunaweza kuelewa  yale yaliyokuwa moyoni mwake. Jibu lake lilifunua yaliyokuwa moyoni mwake: “Tazama bwana wangu hajui kilicho nami nyumbani, na vyote ameviweka mkononi mwangu. Hakuna yeyote aliye mkubwa zaidi yangu katika nyumba hii, naye hakunizuilia chochote ila wewe, kwa sababu wewe ni mke wake. Basi ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” (Mwanzo 39:8, 9) Wazia kijana huyo akiongea maneno hayo kwa uthabiti. Aliumia sana moyoni alipotafakari kuhusu lengo la mwanamke huyo la kutaka kufanya uasherati naye. Kwa nini?

Kama Yosefu alivyosema, bwana wake alimtumaini. Potifa alikuwa ameviweka vitu vyote mikononi mwa Yosefu, hakumzuilia chochote ila mke wake. Yosefu angewezaje kumsaliti? Alichukia wazo hilo. Alichukizwa zaidi na wazo la kumtendea dhambi Mungu wake, Yehova. Wazazi wake walikuwa wamemfundisha maoni ya Mungu kuhusu ndoa na uaminifu. Alielewa vizuri hisia za Yehova mwanzilishi wa ndoa. Mwanamume angeshikamana na mke wake na kuwa “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Wale waliojaribu kuvunja uhusiano huo walikabili hatari ya kupatwa na ghadhabu ya Mungu. Kwa mfano, wanaume waliokuwa karibu kumnajisi Sara mke wa Abrahamu na pia kumnajisi Rebeka mke wa Isaka, walinusurika kuadhibiwa na Mungu. (Mwanzo 20:1-3; 26:7-11) Yosefu alijifunza somo hilo vizuri, na alikusudia kuishi kulingana nalo.

Mke wa Potifa hakufurahia mambo aliyosikia. Mtumwa huyo wa hali ya chini alimkataa huku akisema kwamba ni “ubaya mkubwa”! Hata hivyo akaendelea kumshawishi. Huenda kiburi na majivuno yake yalimfanya aumie, lakini aliazimia kumfanya Yosefu akubali. Hivyo, alionyesha roho kama ya Shetani, aliyemshawishi Yesu. Ushawishi wa Shetani haukufaulu pia, lakini badala ya kukata tamaa, Shetani alimwacha mpaka “wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Kwa hiyo, watu waaminifu wanahitaji kuazimia kusimama imara. Hivyo ndivyo Yosefu alivyofanya. Ijapokuwa hali hiyo iliendelea “siku baada ya siku,” hakukubali. Tunasoma hivi: “Hakumsikiliza kamwe.” (Mwanzo 39:10) Hata hivyo, mke wa Potifa alikuwa ameazimia.

Alisubiri wakati ambapo watumishi wengine hawakuwepo nyumbani. Alijua kwamba Yosefu angeingia ndani ili afanye kazi yake. Alipoingia tu, akajaribu kumshawishi. Akashika vazi lake, kwa mara nyingine akamsihi akisema: “Lala nami!” Yosefu alitenda haraka. Akamnyang’anya vazi toka mkononi mwake na kuvuta lakini mke wa Potifa akaling’ang’ania. Yosefu akaliacha vazi mikononi mwake, na akakimbia!—Mwanzo 39: 11, 12.

Huenda hilo likatukumbusha shauri la mtume Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu: “Ukimbieni uasherati!” (1 Wakorintho 6:18) Yosefu aliweka mfano mzuri sana kwa Wakristo wote wa kweli! Huenda tukalazimika kuwa karibu na wale ambao hawaheshimu sheria za Mungu za maadili, lakini hilo halimaanishi kwamba ni lazima tuathiriwe na tabia zao mbaya. Licha ya hasara tunayoweza kupata, ni lazima tukimbie.

Katika kisa cha Yosefu, hali ilikuwa mbaya zaidi. Mke wa Potifa alitaka kulipa kisasi. Mara moja akaanza kupiga kelele, na kuwaita watumishi wengine wa nyumba yake. Akawaambia kwamba Yosefu alitaka kumbaka lakini akakimbia alipolia kwa sauti kubwa. Akaliweka vazi lake kando yake mpaka mume wake aliporudi. Potifa aliporudi nyumbani, akamwambia maneno hayohayo, na kudai kuwa lilikuwa kosa la mume wake kumleta mtumishi huyo nyumbani kwao. Potifa alifanya nini? Tunasoma hivi: “Hasira yake ikawaka”! Akamfunga gerezani.—Mwanzo 39:13-20.

“WAKAITESA MIGUU YAKE KWA PINGU”

Hatujui mengi kuhusu magereza ya Misri yalivyokuwa wakati huo. Wachimbuaji wa vitu vya kale walipata magofu ya maeneo hayo—ngome kubwa iliyokuwa na vyumba vya magereza na mapango. Baadaye Yosefu alifafanua eneo hilo kwa neno ambalo kihalisi lilimaanisha “tundu,” ambalo linatoa wazo la eneo lisilo na mwanga wala tumaini lolote. (Mwanzo 40:15) Katika kitabu cha Zaburi, tunajifunza kwamba Yosefu alikuwa akiteseka: “Wakaitesa miguu yake kwa pingu, Nafsi yake ikaingia katika vyuma.” (Zaburi 105:17, 18) Wakati mwingine Wamisri waliweka mikono ya wafungwa mgongoni na kuifunga kwa pingu kwenye  viwiko; wengine walifungwa kola za chuma shingoni. Lazima Yosefu awe aliumia sana kwa kutendewa isivyofaa—kwa kuwa hakuwa amefanya kosa lolote!

Isitoshe, hali hiyo iliendelea kwa muda mrefu. Simulizi hilo linasema kwamba Yosefu “akaendelea kuwa humo katika nyumba ya gereza.” Alikaa kwa miaka mingi mahali hapo penye mateso! * Pia, Yosefu hakujua kama angeachiliwa. Hali hizo zenye kutisha zilipoendelea kwa majuma kadhaa, kisha miezi, Yosefu aliwezaje kuvumilia bila kupoteza tumaini au kukata tamaa?

Simulizi hilo linatupa jibu hili lenye kutia moyo: “Yehova akaendelea kuwa pamoja na Yosefu, akazidi kumfanyia fadhili zenye upendo.” (Mwanzo 39:21) Si kuta za gereza, wala pingu, wala mapango yenye giza vinavyoweza kuzuia fadhili zenye upendo za Yehova zisiwafikie watumishi wake. (Waroma 8:38, 39) Tunaweza kumwazia Yosefu akisali kwa Baba yake mpendwa wa mbinguni akimweleza maumivu yake na kisha anapata amani na utulivu ambavyo hutoka kwa “Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4; Wafilipi 4:6, 7) Yehova alimfanyia Yosefu nini kingine? Tunasoma kwamba akaendelea kumwezesha Yosefu “kupata kibali machoni pa ofisa mkuu wa nyumba ya gereza.”

Ni wazi kwamba wafungwa walipewa kazi za kufanya, na kwa mara nyingine tena Yosefu alimpa Yehova nafasi ya kumbariki. Alifanya kazi kwa bidii, kazi yoyote aliyopewa aliifanya kwa uwezo wake wote na akamtumaini Yehova. Kwa baraka za Yehova, Yosefu aliheshimiwa na kutumainiwa, kama tu alivyokuwa katika nyumba ya Potifa. Tunasoma hivi: “Ofisa mkuu wa nyumba ya gereza akawatia mkononi mwa Yosefu wafungwa wote waliokuwa katika nyumba hiyo ya gereza; na yote waliyokuwa wakifanya humo yeye ndiye aliyekuwa akiagiza yafanywe. Yule ofisa mkuu wa nyumba ya gereza hakuwa akiangalia kitu chochote kilichokuwa mkononi mwake, kwa sababu Yehova alikuwa pamoja na Yosefu na yale aliyokuwa akifanya Yehova aliyafanikisha.” (Mwanzo 39:22, 23) Yosefu alifarijiwa sana kujua kwamba Yehova alimjali!

Yosefu alifanya kazi kwa bidii alipokuwa gerezani, na Yehova alimbariki

Huenda tukapatwa na hali zenye kuhangaisha na hata kutendewa isivyo haki, lakini tunaweza kujifunza kutokana na imani ya Yosefu. Ikiwa tunaendelea kuwa karibu na Yehova kupitia sala, kubaki washikamanifu kwa amri zake, kujitahidi kufanya yaliyo sawa machoni pake, tutampa nafasi ya kutubariki. Katika kisa cha Yosefu, Yehova aliendelea kumbariki, kama tutakavyoona katika makala zitakazofuata katika mfululizo huu.

^ fu. 23 Biblia inaonyesha kwamba Yosefu alikuwa na umri wa miaka 17 au 18 alipoingia katika nyumba ya Potifa na alikaa huko kwa muda mrefu vya kutosha kukua kufikia kuwa mwanamume—huenda miaka kadhaa. Alikuwa na umri wa miaka 30 alipoachiliwa kutoka gerezani.—Mwanzo 37:2; 39:6; 41:46.