Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 WASOMAJI WETU WANAULIZA. . .

Ukweli wa Mambo Ni Nini Kuhusu Krismasi?

Ukweli wa Mambo Ni Nini Kuhusu Krismasi?

Mamilioni ya watu kote duniani husherehekea sikukuu ya Krismasi kwa sababu mbalimbali. Baadhi yao hufurahia wakati huo wa sherehe wakiwa na marafiki na familia. Wengine hutumia kipindi hicho kufikiria kuhusu mambo ya Mungu na kuwasaidia maskini na wenye uhitaji. Bila shaka si vibaya kufanya mambo hayo mazuri. Hata hivyo, kuna mambo yasiyofaa kuhusu sherehe yenyewe.

Kwanza kabisa, watu wengi wanaosherehekea Krismasi wanaamini kwamba wanasherehekea siku ambayo Yesu alizaliwa. Hata hivyo, wanahistoria wengi wanakubaliana kwamba Yesu hakuzaliwa Desemba 25. Kitabu The Christian Book of Why kinasema hivi: “Wakristo wa mapema walikataa kuwa na siku hususa ya kusheherekea kuzaliwa kwa Yesu” kwa sababu walitaka “kuachana kabisa na mazoea yote ya kipagani.” Inapendeza kwamba Biblia haisemi kuwa Yesu alisherehekea siku yake ya kuzaliwa au ya mtu mwingine. Badala yake aliwaagiza wafuasi wake wakumbuke kifo chake.—Luka 22:19.

Jambo la pili ni kwamba wasomi wengi wanakubaliana kuwa desturi nyingi za Krismasi zilitokana na mazoea ya wapagani na dini ambazo si za Kikristo. Mambo hayo yanatia ndani desturi za Baba Krismasi, matumizi ya mlimbo, mti wa Krismasi, kubadilishana zawadi, kuwasha mishumaa na kuchoma magogo ya mti wa Krismasi, kuning’iniza mashada ya maua na kuimba nyimbo za Krismasi. Kitabu The Externals of the Catholic Church kinasema hivi kuhusu desturi za Krismasi: “Tunapotoa na kupokea zawadi za Krismasi, na kuning’iniza maua ya kijani kibichi nyumbani na makanisani, ni wangapi kati yetu wanaojua kwamba wanaiga desturi za kipagani?”

“Tunapotoa na kupokea zawadi za Krismasi, na kuning’iniza maua ya kijani kibichi nyumbani na makanisani, ni wangapi kati yetu wanaojua kwamba wanaiga desturi za kipagani?” —Kitabu The Externals of the Catholic Church

Huenda ukajiuliza kwani kuna ubaya gani wa kuiga desturi au mazoea haya? Jibu linapatikana katika jambo la tatu. Mungu hataki tuchanganye ibada safi na desturi za kipagani. Kupitia nabii Wake Amosi, Yehova aliwaambia hivi waabudu Wake walioasi katika taifa la Israeli la kale: “Nimechukia, nimezikataa sherehe zenu . . . Ondoeni kutoka kwangu mchafuko wa nyimbo zenu.”—Amosi 5:21, 23.

Kwa nini Yehova alitumia maneno hayo makali? Fikiria mambo yaliyofanywa na watu katika ufalme wa kaskazini katika taifa la Israeli la kale. Mfalme wao wa kwanza, Yeroboamu, aliweka ndama wa dhahabu katika miji ya Dani na Betheli na akawashawishi watu waabudu ndama hao badala ya kumwabudu Yehova Mungu kwa njia inayofaa katika hekalu jijini Yerusalemu. Mfalme huyo pia alianzisha sherehe kadhaa na akawaweka rasmi makuhani ili wawasaidie watu kuzisherehekea.—1 Wafalme 12:26-33.

Huenda Waisraeli hao walikuwa na nia nzuri walipofanya mambo hayo. Na kwa kweli waliyatenda kwa jina la Mungu wakisema kwamba walitaka kumpendeza. Hata hivyo maneno makali ambayo Mungu alisema kupitia nabii Amosi na manabii wengine yanaonyesha wazi jinsi alivyoona desturi hizo. Kupitia nabii Malaki, Mungu alisema: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” (Malaki 3:6) Bila shaka maneno hayo yanatusaidia tuone jinsi Mungu anavyohisi kuhusu sikukuu ya Krismasi leo.

Baada ya kuchunguza sababu tulizozungumzia hapo juu, mamilioni ya watu wameacha kusherehekea Krismasi. Isitoshe, wameridhika kwelikweli na kupata shangwe kwa kutenga wakati ili kushirikiana na familia zao na marafiki na hata kuwasaidia wenye uhitaji na maskini wakati wowote ule.