Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

WASOMAJI WETU WANAULIZA . . .

Je, Ista ni Sikukuu ya Kikristo?

Je, Ista ni Sikukuu ya Kikristo?

Kulingana na kitabu Encyclopædia Britannica Ista imefafanuliwa kuwa “sikukuu kubwa ya kanisa la Kikristo ambapo watu husherehekea Kufufuka kwa Yesu Kristo.” Hata hivyo, je, Ista ni sikukuu ya Kikristo?

Ili kuthibitisha ukweli wa jambo fulani, ni vizuri kuchunguza mambo muhimu yanayohusu jambo hilo. Vivyo hivyo, ili kuthibitisha ikiwa Ista ni sikukuu ya Kikristo, ni muhimu tuchunguze mambo yanayohusu sikukuu hiyo.

Kwanza kabisa, Yesu aliwaambia wafuasi wake wakumbuke kifo chake wala si ufufuo wake. Mtume Paulo aliita tukio hilo “mlo wa jioni wa Bwana.”—1 Wakorintho 11:20; Luka 22:19, 20.

Isitoshe, kitabu Britannica kinasema kwamba desturi nyingi za sikukuu ya Ista “hazihusiani” na ufufuo wa Yesu “bali zinatokana na desturi za kale.” Kwa mfano, kitabu The Encyclopedia of Religion kinasema hivi kuhusu matumizi maarufu ya mayai na sungura wakati wa sikukuu ya Ista: “Yai linawakilisha uhai mpya unaotokea baada ya kuvunjika kwa gamba la yai.” Kitabu hicho kinaongeza hivi: “Sungura ni mnyama aliyejulikana kuwa na uwezo mkubwa wa kupata watoto, na hivyo aliwakilisha mwanzo wa majira ya masika.”

Philippe Walter, profesa wa uandishi wa enzi ya kati, anaeleza jinsi desturi hizo zilivyokuja kuwa sehemu ya sikukuu ya Ista. Aliandika kwamba “katika jitihada za kuwageuza wapagani kuwa Wakristo,” ilikuwa rahisi kuhusianisha sherehe ya wapagani ya kusherehekea “mwisho wa msimu wa baridi kali na mwanzo wa msimu wa masika,” na kufufuliwa kwa Yesu. Profesa Walter anasema kwamba hiyo ilikuwa hatua muhimu ya kuziingiza “sherehe za Kikristo” kwenye kalenda za matukio ya wapagani na hivyo kuwashawishi wapagani wengi iwezekanavyo wajiunge na Ukristo.

Jitihada hiyo ya “kuwageuza wapagani kuwa Wakristo” haikufanyika mitume walipokuwa hai, kwa sababu walikuwa “kizuizi” dhidi ya mafundisho ya wapagani. (2 Wathesalonike 2:7) Mtume Paulo alitoa onyo kwamba baada ya yeye “kuondoka . . . watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:29, 30) Pia, mwishoni mwa karne ya kwanza, mtume Yohana alizungumzia kuhusu watu fulani ambao walikuwa wakiwapotosha Wakristo. (1 Yohana 2:18, 26) Hilo lilifanya desturi za wapagani zienee upesi.

“Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.”—2 Wakorintho 6:14

Huenda wengine wakahisi kwamba haikuwa vibaya kuruhusu desturi fulani za Ista kwa kuwa kufanya hivyo kuliwasaidia “wapagani” waelewe vizuri zaidi maana ya ufufuo wa Yesu. Hata hivyo, Paulo hakuunga mkono jambo hilo. Ingawa Paulo alisafiri katika Milki ya Roma iliyokuwa na desturi nyingi za kipagani hakufuata hata desturi moja ya kipagani ili kuwasaidia watu kumwelewa vizuri Yesu. Badala yake aliwaonya Wakristo kwa kusema hivi: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. Kwa maana kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria? Au nuru ina ushirika gani na giza? ‘Kwa hiyo tokeni katikati yao, na mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kilicho najisi.’”—2 Wakorintho 6:14, 17.

Tumejifunza nini baada ya kuchunguza kwa ufupi mambo hayo? Tumejifunza kwamba Ista si sikukuu ya Kikristo.