ENDELEA KUKESHA!
Wanasayansi Wasogeza Mbele Mshale wa Saa ya Mwisho wa Dunia—Biblia Inasema Nini?
Januari 24, 2023, wanasayansi walisogeza mbele mshale wa dakika wa Saa ya Mwisho wa Dunia au Doomsday Clock a na hivyo, mshale huo ulikaribia zaidi saa sita usiku. Kwenye saa hiyo, saa sita usiku inawakilisha mwisho wa dunia.
“‘Saa ya Mwisho wa Dunia’ inawakilisha hatari ambayo wanadamu wanakabili ya kujiangamiza wenyewe. Jumanne, wanasayansi walisogeza mshale wa saa hiyo karibu zaidi na saa sita usiku kwa sababu ya matukio kama vile vita nchini Ukrainia, tishio la vita vya kinyuklia, na hali ya hewa iliyozorota.”—AFP International Text Wire.
“Wanasayansi walitangaza Jumanne kwamba ‘Saa ya Mwisho wa Dunia’ ilisogezwa ikawa sekunde 90 kabla ya saa sita usiku—hilo linaonyesha kwamba wanadamu wapo karibu sana na har-magedoni.”—ABC News.
“Jopo la kimataifa la wanasayansi limeona kwamba kuna uwezekano mkubwa zaidi kuliko wakati mwingine wowote wa wanadamu kujiangamiza wenyewe.”—The Guardian.
Je, sayari yetu na wanadamu waliomo wataangamia kabisa? Je, tunahitaji kuwa na hofu kuhusu mambo ambayo yatatendeka wakati ujao? Biblia inasema nini?
Wakati Ujao Utakuwaje?
Kulingana na Biblia, “dunia inadumu milele” na kuna wanadamu ambao “wataishi humo milele.” (Mhubiri 1:4; Zaburi 37:29) Kwa hiyo, wanadamu hawataiangamiza dunia ama kuifanya kuwa mahali ambapo viumbe hai haviwezi kuishi.
Hata hivyo, Biblia inasema kwamba kutakuwa na mwisho. Kwa mfano, inasema kwamba “ulimwengu unapitilia mbali.”—1 Yohana 2:17.
Ili kujua Biblia inamaanisha nini inapozungumzia mwisho wa dunia, soma makala yenye kichwa “Je, Ulimwengu Utakwisha Karibuni? Apokalipsi Ni Nini?”
Ili kujifunza kile ambacho Biblia inasema kuhusu wakati ambapo matukio mbalimbali ulimwenguni yatatendeka soma makala yenye kichwa “Mwisho wa Ulimwengu Utakuja Lini?”
Kudumisha Mtazamo Mzuri
Biblia inaweza kutusaidia kudumisha mtazamo mzuri licha ya matatizo yaliyopo ulimwenguni sasa. Jinsi gani?
Biblia inatupa ushauri unaoweza kutusaidia katika maisha ya kila siku. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa mfano, soma makala yenye kichwa “Jinsi ya Kudhibiti Wasiwasi” ili kuona jinsi Biblia inavyoweza kukusaidia kuendelea kuwa na mtazamo mzuri licha ya changamoto unazokabiliana nazo maishani.
Biblia inatupatia tumaini lenye kutegemeka la wakati ujao. (Waroma 15:4) Inaeleza waziwazi kuhusu mambo ambayo tunaweza kutarajia yatokee sasa na mambo ya wakati ujao. Hilo linatusaidia tusiwe na hofu licha ya mambo yanayotendeka ulimwenguni leo.
Ili ujifunze mengi zaidi katika Biblia, tunakukaribisha kwa uchangamfu kujifunza Biblia ukiongozwa na mwalimu bila malipo sasa.
a “Saa ya Mwisho wa Dunia ni mchoro wa saa ambao unaonyesha jinsi tunavyokaribia kuharibu kabisa mfumo wa maisha duniani kupitia vifaa hatari vya kisasa tulivyobuni sisi wenyewe. Saa hiyo ni mfano unaotukumbusha hatari ambazo tunahitaji kusuluhisha ili tufaulu kuendelea kuishi katika sayari hii.”—Bulletin of the Atomic Scientists.