Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utangulizi

Utangulizi

“Muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”​—WAEBRANIA 6:12.

1, 2. Mwangalizi fulani anayesafiri aliwaonaje watu waaminifu wanaotajwa katika Biblia, na kwa nini watu hao wanaweza kuwa rafiki wazuri?

“ANAZUNGUMZA kuhusu watu wanaotajwa katika Biblia kana kwamba ni rafiki zake wa tangu zamani.” Dada mmoja alisema maneno hayo baada ya kusikiliza hotuba ya mwangalizi fulani anayesafiri mwenye umri mkubwa. Na ni kweli, kwa sababu ndugu huyo alijifunza Neno la Mungu na kulifundisha kwa miaka mingi, hivi kwamba wanaume na wanawake wenye imani wanaotajwa katika Biblia ni kama rafiki zake ambao amewajua tangu zamani.

2 Bila shaka, ingefurahisha sana kuwa rafiki ya watu hao wanaotajwa katika Biblia. Je, wao ni halisi kwako? Hebu wazia ingekuwaje kama ungetembea na kuzungumza pamoja nao, kufahamiana na wanaume na wanawake kama vile Noa, Abrahamu, Ruthu, Eliya, na Esta. Fikiria jinsi ambavyo ungefaidika kutokana na mashauri yao na maneno yenye kujenga ambayo wangekuambia!​—Soma Methali 13:20.

3. (a) Tunawezaje kufaidika kwa kujifunza kuhusu wanaume na wanawake wenye imani wanaotajwa katika Biblia? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Bila shaka, baada ya “ufufuo wa waadilifu,” itawezekana kuanzisha urafiki na watu hao. (Mdo. 24:15) Lakini, hata sasa tunaweza kufaidika kwa kujifunza kuhusu wanaume na wanawake hao wenye imani wanaotajwa katika Biblia. Jinsi gani? Mtume Paulo anatoa ushauri huu: “Muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” (Ebr. 6:12) Kabla ya kuzungumzia wanaume na wanawake wenye imani, acheni tuchunguze maswali machache yanayohusiana na maneno ya Paulo: Imani ni nini, na kwa nini tunaihitaji? Tunaweza kuwaigaje watumishi waaminifu walioishi zamani?

Imani Ni Nini na kwa Nini Tunaihitaji?

4. Watu wana maoni gani kuhusu imani, na kwa nini wamekosea?

4 Imani ni sifa yenye kupendeza ambayo ilithaminiwa sana na wanaume na wanawake ambao tutajifunza kuwahusu. Watu wengi leo wanadharau imani, wanadhani inamaanisha kuamini kitu bila kuwa na uthibitisho wala ushuhuda wowote. Hata hivyo, maoni yao si sahihi. Imani si kufuata jambo bila kufikiri; si hisia tu; inahusisha mengi zaidi ya kuitikadi. Ni hatari kufuata jambo bila kufikiri. Hisia hubadilika-badilika; na itikadi haitoshi tunapozungumza kuhusu Mungu, kwa kuwa hata “roho waovu nao wanaamini na kutetemeka.”—Yak. 2:19.

5, 6. (a) Imani yetu inahusisha mambo gani mawili ambayo hayaonekani? (b) Imani yetu inapaswa kuwa na msingi gani thabiti? Toa mfano.

5 Imani ya kweli inahusisha mengi zaidi. Kumbuka jinsi Biblia inavyofafanua imani. (Soma Waebrania 11:1.) Paulo alisema kwamba imani inahusisha mambo mawili ambayo hatuwezi kuyaona. Kwanza, inahusisha mambo halisi ya sasa ambayo “hayaonekani.” Hatuwezi kuona kwa macho mambo halisi yaliyo mbinguni—kama vile Yehova Mungu, Mwana wake, au Ufalme ambao sasa unatawala mbinguni. Pili, imani inahusisha “mambo yanayotumainiwa,” yaani, matukio ambayo tunatazamia. Hatuwezi kuona ulimwengu mpya ambao utaletwa hivi karibuni na Ufalme wa Mungu. Je, hilo linamaanisha hatuna msingi wowote wa kuamini mambo hayo halisi na yale tunayotazamia?

6 Sivyo hata kidogo! Paulo alifafanua kwamba imani ya kweli inategemea msingi thabiti. Aliposema imani ni “tarajio lililohakikishwa,” alitumia maneno ambayo pia yanaweza kutafsiriwa “hati ya kumiliki.” Hebu wazia mtu fulani ameamua kukupatia nyumba. Huenda akakupa hati ya kumiliki nyumba hiyo na kukuambia, “Hii ndiyo nyumba yako.” Bila shaka, hamaanishi utaishi juu ya kikaratasi hicho; anamaanisha cheti hicho ni muhimu sana kisheria hivi kwamba kihalisi kinawakilisha nyumba yenyewe. Vivyo hivyo, uthibitisho wa imani yetu ni hakika, wenye nguvu sana, hivi kwamba unaweza kulinganishwa na imani yetu.

7. Imani ya kweli inahusisha nini?

7 Hivyo, imani ya kweli inahusisha uthibitisho hakika na usadikisho thabiti ambao unahusiana kabisa na Yehova Mungu. Imani hutusaidia kumwona Yehova kama Baba yetu mpendwa na kusadiki kwamba ahadi zake zote zitatimia. Lakini imani ya kweli inahusisha mengi zaidi. Kama kiumbe kilicho hai, ni lazima ilishwe ili iendelee kuishi. Ni lazima ionyeshwe kwa matendo, la sivyo itakufa.—Yak. 2:26.

8. Kwa nini imani ni muhimu sana?

8 Kwa nini imani ni muhimu sana? Paulo alitoa jibu lenye kuchochea. (Soma Waebrania 11:6.) Hatuwezi kamwe kumkaribia Yehova wala kumpendeza ikiwa hatuna imani. Basi, imani ni muhimu ikiwa tunataka kutimiza kusudi muhimu na la maana zaidi kwa kiumbe yeyote mwenye akili, yaani, kumkaribia na kumtukuza Baba yetu wa mbinguni, Yehova.

9. Yehova ameonyeshaje kwamba anaelewa tunahitaji kuwa na imani?

9 Yehova anajua kwamba tunahitaji kuwa na imani, hivyo ametupatia mifano ili kutufundisha jinsi ya kusitawisha na kuonyesha imani. Amebariki kutaniko la Kikristo kwa kuwa na mifano ya wanaume waaminifu wanaoongoza. Neno lake linasema: “Igeni imani yao.” (Ebr. 13:7) Na ametupatia mengi zaidi. Paulo aliandika kuhusu “wingu kubwa . . . la mashahidi,” wanaume na wanawake wa zamani walioweka mfano bora wa imani. (Ebr. 12:1) Bila shaka, kuna waaminifu wengine wengi ambao hawako kwenye orodha ya Paulo ya Waebrania sura ya 11. Biblia ina masimulizi mengi ya kweli kuhusu wanaume na wanawake, vijana na wazee wa malezi mbalimbali, ambao walikuwa na imani na tunaweza kujifunza mengi kutoka kwao wakati huu ambao wengi hawana imani.

Tunawezaje Kuiga Imani ya Wengine?

10. Funzo letu la kibinafsi linawezaje kutusaidia kuwaiga wanaume na wanawake waaminifu wanaotajwa katika Biblia?

10 Huwezi kumwiga mtu kabla hujamchunguza kwa makini. Unaposoma kitabu hiki, utaona kwamba utafiti mwingi umefanywa ili kukusaidia uwaelewe wanaume na wanawake wenye imani. Tunakuhimiza wewe pia ufanye utafiti zaidi kuwahusu. Unapojifunza kibinafsi, fanya utafiti zaidi wa Biblia ukitumia vifaa unavyoweza kupata. Unapotafakari kuhusu mambo unayosoma, jaribu kuwazia maeneo yanayotajwa katika masimulizi ya Biblia. Jaribu kusikia sauti, na kunusa harufu zinazosimuliwa. Jambo muhimu zaidi, jaribu kutambua hisia za wahusika. Unapohisi kama walivyohisi wanaume na wanawake hao waaminifu, watakuwa halisi zaidi kwako na utawafahamu zaidi, hata wengine wanaweza kuwa kama rafiki zako wa karibu.

11, 12. (a) Unawezaje kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Abramu na Sarai? (b) Unawezaje kufaidika kutokana na mifano wa Hana, Eliya, au Samweli?

11 Ukiwafahamu vizuri zaidi, utachochewa kuwaiga. Kwa mfano, wazia unapofikiria kukubali mgawo mpya. Katika tengenezo la Yehova tunaweza kupanua huduma yetu kwa njia mbalimbali. Labda unaombwa uhamie eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri, au unaombwa ujaribu njia fulani ya kuhubiri ambayo hujazoea au usiyopenda. Unapofikiria mgawo huo na kusali kuuhusu, je, hungefaidika kwa kutafakari mfano wa Abramu? Yeye na Sarai walikuwa tayari kuacha starehe za Uru na walibarikiwa sana kwa kufanya hivyo. Unapoiga mfano wao, bila shaka utahisi kwamba umewafahamu vizuri zaidi.

12 Vivyo hivyo, namna gani ikiwa mtu aliye karibu nawe angekuchukia na hivyo uvunjike moyo hata uhisi kukaa nyumbani badala ya kwenda mikutanoni? Ukitafakari kumhusu Hana na jinsi alivyoshinda chuki ya Penina, unaweza kufanya uamuzi unaofaa, na labda uhisi kwamba Hana ni kama rafiki yako wa karibu. Pia, ikiwa umevunjika moyo na kuhisi hufai, huenda ukapendezwa na Eliya unaposoma kuhusu matatizo aliyokabili na jinsi Yehova alivyomfariji. Na huenda vijana wanaoshawishiwa kila mara na wanafunzi wenzao waliopotoka kiadili wakapendezwa na Samweli wanapojifunza jinsi alivyokabiliana na uvutano mbaya wa wana wa Eli kwenye maskani.

13. Je, kuiga imani ya watu wanaotajwa katika Biblia kutapunguza thamani ya imani yako? Fafanua.

13 Je, kuiga imani ya watu kama hao wanaotajwa katika Biblia kutapunguza thamani ya imani yako? Hapana! Kumbuka, Neno la Mungu linatuhimiza tuwaige watu wenye imani. (1 Kor. 4:16; 11:1; 2 Thes. 3:7, 9) Hata baadhi ya watu tutakaojifunza kuwahusu katika kitabu hiki, waliiga watu waaminifu walioishi kabla yao. Kwa mfano, katika Sura ya 17 ya kitabu hiki, inaonekana Maria alinukuu maneno ya Hana, kuonyesha kwamba aliiga mfano wake. Je, hilo lilipunguza thamani ya imani ya Maria? La, hasha! Badala yake, mfano wa Hana ulimsaidia Maria kusitawisha imani ili aboreshe uhusiano wake pamoja na Yehova Mungu.

14, 15. Ni mambo gani yaliyo katika kitabu hiki, na unawezaje kuyatumia?

14 Kitabu hiki kimekusudiwa kukusaidia uimarishe imani yako. Sura zifuatazo ni mkusanyo wa makala za mfululizo wenye kichwa “Igeni Imani Yao” zilizochapishwa katika Mnara wa Mlinzi kati ya 2008 na 2013. Hata hivyo, habari fulani zimeongezwa. Kuna maswali kwa ajili ya mazungumzo na matumizi ya habari. Picha nyingi maridadi zimeongezwa kwenye kitabu hiki, na zile zilizokuwepo zikaongezwa ukubwa na kuboreshwa. Habari nyingine muhimu kama vile, mfuatano wa matukio na ramani, zimeongezwa. Kitabu Igeni Imani Yao kimekusudiwa kwa ajili ya funzo la kibinafsi, familia, na kutaniko. Huenda pia familia nyingi zitafurahia kusoma pamoja hadithi hizi kwa sauti.

15 Kitabu hiki na kikusaidie kuiga imani ya watumishi washikamanifu wa Yehova walioishi zamani. Na kikusaidie kuimarisha imani yako unapozidi kumkaribia Baba yetu wa mbinguni, Yehova!