Barua ya Kwanza kwa Wakoritho 11:1-34

  • “Iweni waigaji wangu” (1)

  • Ukichwa na kufunika kichwa (2-16)

  • Kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana (17-34)

11  Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.+  Ninawapongeza kwa sababu katika mambo yote mnanikumbuka na mnayashika mapokeo kama vile nilivyowapa.  Lakini ninataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo;+ nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume;+ nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.+  Kila mwanamume ambaye husali au kutoa unabii akiwa na kitu juu ya kichwa chake hukiaibisha kichwa chake;  lakini kila mwanamke anayesali au kutoa unabii+ bila kufunika kichwa chake anakiaibisha kichwa chake, kwa maana ni kana kwamba yeye ni mwanamke mwenye kichwa kilichonyolewa.  Kwa maana ikiwa mwanamke hajifuniki, anapaswa kukatwa nywele zake; lakini ikiwa ni aibu kwa mwanamke kukatwa nywele au kunyolewa, anapaswa ajifunike.  Kwa maana mwanamume hapaswi kufunika kichwa chake, kwa kuwa yeye ni mfano na utukufu wa Mungu,+ lakini mwanamke ni utukufu wa mwanamume.  Kwa maana mwanamume hakutoka katika mwanamke, bali mwanamke alitoka katika mwanamume.+  Isitoshe, mwanamume hakuumbwa kwa ajili ya mwanamke, bali mwanamke kwa ajili ya mwanamume.+ 10  Ndiyo sababu mwanamke anapaswa kuwa na ishara ya mamlaka juu ya kichwa chake kwa sababu ya malaika.+ 11  Tena, kuhusiana na Bwana, mwanamke hajatenganishwa na mwanamume wala mwanamume hajatenganishwa na mwanamke. 12  Kwa maana kama vile mwanamke alivyotoka katika mwanamume,+ vivyo hivyo pia mwanamume amepitia katika mwanamke; lakini vitu vyote vimetoka kwa Mungu.+ 13  Hukumuni wenyewe: Je, inafaa mwanamke kusali kwa Mungu bila kufunika kichwa chake? 14  Je, maumbile yenyewe hayawafundishi kwamba nywele ndefu ni aibu kwa mwanamume, 15  lakini mwanamke akiwa na nywele ndefu, ni utukufu kwake? Kwa maana amepewa nywele zake ziwe kitu cha kujifunika. 16  Hata hivyo, mtu yeyote akitaka kubishania desturi nyingine, sisi hatuna nyingine, wala makutaniko ya Mungu. 17  Lakini ninapoyatoa maagizo haya, siwapongezi ninyi, kwa sababu mnakutana pamoja, si kwa ajili ya wema, bali kwa ajili ya ubaya. 18  Kwanza kabisa, nasikia kwamba mnapokutana katika kutaniko, kuna migawanyiko kati yenu; na kwa kadiri fulani ninaamini jambo hilo. 19  Kwa maana lazima kutakuwa na madhehebu miongoni mwenu,+ ili wale waliokubaliwa kati yenu waonekane. 20  Mnapokutana mahali pamoja, kwa kweli si kwa sababu ya kula Mlo wa Jioni wa Bwana.+ 21  Kwa maana mnapokula, kila mtu hutangulia kula mlo wake mwenyewe wa jioni, hivi kwamba mmoja ana njaa lakini mwingine amelewa. 22  Je, hamna nyumba ambamo mnaweza kula na kunywa? Au je, mnalidharau kutaniko la Mungu na kuwaaibisha wale wasio na kitu? Niwaambie nini ninyi? Je, niwapongeze? Kuhusu hilo siwapongezi. 23  Kwa maana nilipokea kutoka kwa Bwana kile nilichowapa ninyi pia, kwamba Bwana Yesu katika usiku+ ambao alisalitiwa alichukua mkate, 24  na baada ya kutoa shukrani, akaumega na kusema: “Huu unamaanisha mwili wangu,+ ambao ni kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.”+ 25  Akafanya vivyo hivyo na kile kikombe+ pia, baada ya wao kula mlo wa jioni, akisema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano+ jipya kwa msingi wa damu yangu.+ Endeleeni kufanya hivi, kila mara mnapokinywa, kwa kunikumbuka mimi.”+ 26  Kwa maana kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki, mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapokuja. 27  Kwa hiyo, yeyote anayekula mkate au kukinywa kikombe cha Bwana isivyofaa atakuwa na hatia kuhusiana na mwili na damu ya Bwana. 28  Kwanza, acheni mtu ajichunguze mwenyewe na kuona kama anafaa,+ ndipo ale mkate na anywe kikombe. 29  Kwa maana yule anayekula na kunywa bila kuutambua mwili, anakula na kunywa hukumu dhidi yake mwenyewe. 30  Ndiyo sababu wengi kati yenu ni dhaifu na wagonjwa, na wengi wamelala usingizi katika kifo.*+ 31  Lakini kama tungetambua jinsi sisi wenyewe tulivyo, hatungehukumiwa. 32  Hata hivyo, tunapohukumiwa, Yehova*+ anatutia nidhamu, ili tusihukumiwe pamoja na ulimwengu.+ 33  Kwa hiyo, ndugu zangu, mnapokutana pamoja ili kula mlo huo, mngojeane. 34  Ikiwa yeyote ana njaa, acheni ale nyumbani, ili mnapokutana pamoja isiwe kwa ajili ya kuhukumiwa.+ Lakini kuhusu mambo yaliyobaki, nitayarekebisha nitakapofika.

Maelezo ya Chini

Inaonekana inamaanisha kifo cha kiroho.