Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Ilionekana Kwamba Nilikuwa na Kila Kitu Nilichohitaji”

“Ilionekana Kwamba Nilikuwa na Kila Kitu Nilichohitaji”
  • ALIZALIWA: 1962

  • NCHI: Kanada

  • HISTORIA: Maisha mapotovu

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilizaliwa Montreal, jiji kubwa zaidi katika mkoa wa Quebec nchini Kanada. Mimi, ndugu zangu wawili, na dada yangu tulilelewa na wazazi wenye upendo katika eneo lenye kuvutia la Rosemont. Tulifurahia maisha yenye utulivu na amani.

 Nilipokuwa mvulana, nilipendezwa na Biblia. Nakumbuka nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilisoma katika Agano Jipya kuhusu maisha ya Yesu na nilifurahia sana usomaji huo. Nilitaka kuwa kama Yesu kwa sababu nilivutiwa sana na jinsi alivyowaonyesha wengine upendo na huruma. Kwa kusikitisha, tamaa hiyo ilififia kadiri nilivyokua na kuanza kushirikiana na marafiki wasiofaa.

 Baba yangu alipiga kifaa cha muziki kinachoitwa saksafoni, naye alinipa kifaa chake na pia alinisaidia nipende muziki kama yeye. Hivyo, muziki ukawa jambo kuu maishani mwangu. Nilipenda muziki sana hivi kwamba upesi nilijifunza kupiga gitaa. Baada ya muda, nilianzisha bendi ya muziki wa rock nikiwa na marafiki wangu na bendi yetu ilishiriki katika maonyesho kadhaa. Watayarishaji fulani maarufu katika sekta ya muziki walitambua kipawa changu na wakanifikia. Nilitia sahihi mkataba kwenye kampuni kubwa ya muziki. Nyimbo zangu zilipendwa sana na zilichezwa kwa ukawaida kwenye redio huko Quebec.

 Ilionekana kwamba nilikuwa na kila kitu nilichohitaji. Nilikuwa kijana, maarufu, na nilikuwa nikipata pesa nyingi kwa kufanya kitu nilichopenda. Mchana nilifanya mazoezi, nikafanya mahojiano, nikatia sahihi vitu vya mashabiki wangu, na kuonekana kwenye televisheni. Usiku nilipiga muziki na kula raha. Ili niwe na ujasiri mbele ya watu, nilikuwa nimeanza kunywa kileo nilipokuwa kijana lakini baadaye nikaanza kutumia dawa za kulevya. Pia, nilikuwa na maadili mapotovu na nilifanya mambo bila kujali.

 Watu fulani walitamani maisha yangu kwa sababu nilionekana kuwa mwenye furaha. Lakini nilipokuwa peke yangu, nililemewa na hisia za kwamba sifai kabisa. Nilishuka moyo na nilikuwa na wasiwasi sana. Kwa kusikitisha, nilipopata mafanikio makubwa, watayarishaji wangu wawili wa muziki walikufa kutokana na UKIMWI. Hilo lilinishtua sana. Ingawa nilipenda sana muziki, nilichukizwa na maisha ambayo watu katika sekta hiyo waliishi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Licha ya mafanikio yangu, nilitambua kwamba hali ilikuwa mbaya sana ulimwenguni. Kwa nini kulikuwa na ukosefu mwingi sana wa haki? Nilijiuliza kwa nini Mungu hakuwa akichukua hatua kurekebisha mambo. Nilisali mara nyingi Mungu anisaidie kupata majibu. Nilipokuwa likizo nilianza kusoma tena Biblia. Ingawa sikuelewa mambo mengi niliyosoma, nilifikia mkataa kwamba lazima mwisho wa dunia uko karibu.

 Nilipokuwa nikisoma Biblia, niligundua kwamba pindi moja Yesu alifunga kwa siku 40 akiwa jangwani. (Mathayo 4:​1, 2) Nilijiambia kwamba ikiwa mimi pia nitafanya hivyo, huenda Mungu akanipa majibu, kwa hiyo, nilipanga tarehe ya kuanza. Majuma mawili kabla ya kuanza kufunga, Mashahidi wawili wa Yehova walibisha mlangoni, nami niliwakaribisha kana kwamba nilikuwa nikiwatarajia. Nilimtazama moja kwa moja usoni Shahidi anayeitwa Jacques, na kumuuliza, “Tunajuaje kwamba tunaishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu?” Alinijibu kwa kufungua Biblia yake na kunisomea 2 Timotheo 3:​1-5. Niliwauliza maswali mengi na nilipendezwa na majibu yao yaliyopatana na akili na yenye kuridhisha, ambayo yalitegemea Biblia. Baada ya kunitembelea mara kadhaa, nilitambua kwamba sikuhitaji kufunga.

 Nilianza kujifunza Biblia kwa ukawaida na Mashahidi. Hatimaye, nilinyoa nywele zangu ndefu na nikaanza kuhudhuria mikutano yote kwenye Jumba la Ufalme. Kutokana na jinsi nilivyokaribishwa kwa uchangamfu kwenye hiyo mikutano nilisadikishwa zaidi kwamba hatimaye nilikuwa nimeipata kweli.

 Ili kutumia mambo niliyofundishwa katika Biblia, nilihitaji kufanya mabadiliko makubwa maishani. Nilihitaji kuacha kutumia dawa za kulevya na upotovu wa maadili. Pia, nilihitaji kubadili mtazamo wangu wa ubinafsi na kuwaonyesha wengine ufikirio zaidi. Kwa kuwa nilikuwa mzazi asiye na mwenzi, nilihitaji kujifunza jinsi ya kutunza mahitaji ya kihisia na ya kiroho ya watoto wangu wawili. Kwa hiyo, niliacha kazi yangu ya muziki na kuanza kufanya kazi yenye mshahara mdogo katika kiwanda.

 Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo yote. Nilipojitahidi kuacha kutumia dawa za kulevya, nililazimika kukabiliana na athari za kuacha kuzitumia. Mara chache nilijikuta nikirudia zoea hilo baya. (Waroma 7:​19, 21-​24) Ilikuwa vigumu sana kuacha maisha yangu mapotovu kiadili. Pia, kazi hiyo mpya niliyofanya ilikuwa yenye kuchosha, na mshahara wangu mdogo ulinivunja moyo. Mshahara ambao sasa nilikuwa nikilipwa kwa miezi mitatu ulikuwa sawa na pesa ambazo zamani nilipata kwa kupiga muziki kwa saa mbili tu.

 Sala ilinisaidia nisikate tamaa nilipokuwa nikifanya mabadiliko hayo magumu. Pia, nilijionea umuhimu wa kusoma Biblia kwa ukawaida. Kuna mistari hususa ya Biblia ambayo ilinitia moyo sana. Mmoja ni 2 Wakorintho 7:1, unaowahimiza Wakristo ‘wajisafishe kila unajisi wa mwili na roho.’ Andiko lingine ambalo lilinihakikishia kwamba inawezekana kuacha mazoea yangu mabaya ni Wafilipi 4:13, linalosema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.” Yehova Mungu alijibu sala zangu na kunisaidia kuelewa na kufuata kweli za Biblia. Hilo lilinichochea kujiweka wakfu kwake. (1 Petro 4:​1, 2) Nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mnamo 1997.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Nina hakika kwamba ikiwa ningeendelea kuishi maisha yangu ya zamani, ningalikuwa nimekufa. Hata hivyo, sasa ninafurahia maisha mazuri sana. Mke wangu mpendwa, Elvie, amekuwa baraka kubwa kwangu. Sisi wawili ni wahudumu wa wakati wote, na tunafurahia kuwafundisha watu wengine Biblia. Kufanya hivyo huniletea shangwe kubwa na ninaridhika sana. Ninamshukuru sana Yehova kwa kunivuta kwake.​—Yohana 6:​44.