Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

NJIA YA MAISHA YENYE FURAHA

Upendo

Upendo

WANADAMU WAKO NA LAZIMA SANA YA UPENDO. Bila upendo, hakuna ndoa, familia, ao urafiki wenye unaweza kupata matokeo ya muzuri. Ni wazi kwamba upendo ni wa maana sana ili kuwa na afya ya muzuri ya akili na furaha. Lakini, neno “upendo” linamaanisha nini?

Upendo wenye kuzungumuziwa hapa haiko upendo kati ya mwanaume na mwanamuke, hata kama upendo huo pia ni wa maana. Lakini ni upendo wa hali ya juu wenye unachochea mutu kuhangaikia kabisa faida za wengine, na kumuchochea hata awatie pa nafasi ya kwanza kuliko yeye mwenyewe. Ni upendo wenye kuongozwa na kanuni zenye kutoka kwa Mungu, lakini wenye pia unatia ndani uchangamufu na hisia.

Maelezo yenye kupendeza juu ya upendo yanasema hivi: ‘Upendo ni wenye ustahimilivu [ao, uvumilivu] na wenye fazili. Upendo hauna wivu, haujigambe, haujivune, haujiendeshe bila adabu, hautafute faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweke hesabu ya ubaya. Haushangilie juu ya ukosefu wa uadilifu [ao, haki] bali unashangilia [ao, unafurahi] pamoja na kweli. Unahimili mambo yote, . . . unatumaini mambo yote, unavumilia mambo yote. Upendo haushindwe kamwe [ao, hata kidogo].’​—1 Wakorintho 13:4-8.

Ikiwa upendo kama huo ‘haushindwe kamwe,’ hilo linamaanisha kama utakuwa sikuzote. Kwa kweli, unaweza kuendelea kuwa wenye nguvu zaidi kadiri wakati unapita. Na kwa sababu upendo ni wenye uvumilivu, wenye fazili, na wenye kusamehe, ni “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Kwa hiyo, urafiki wenye kuunganishwa na upendo kama huo ni wenye nguvu na ni wenye furaha hata kama watu wenye kuunganishwa na upendo huo hawakamilike. Kwa mufano, tuzungumuzie ndoa.

KUUNGANISHWA NA “KIFUNGO KIKAMILIFU CHA MUUNGANO”

Yesu alifundisha kanuni za maana juu ya ndoa. Kwa mufano, alisema: “‘Mwanaume atamuacha baba yake na mama yake naye atashikamana na muke [ao, bibi] wake, na hao wawili watakuwa mwili mumoja’ . . . Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mutu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:5, 6) Maneno hayo yanatokeza kanuni mbili hivi.

‘HAO WAWILI WATAKUWA MWILI MUMOJA.’ Ndoa ni mupango wenye unafanya watu wakuwe na urafiki wa sana, na upendo unaweza kulinda wenye kuoana wasiangukie katika hali ya kukosa uaminifu, ni kusema, upendo unaweza kuzuia bibi ao bwana akuwe ‘mwili mumoja’ na mutu mwengine inje ya ndoa. (1 Wakorintho 6:16; Waebrania 13:4) Kukosa uaminifu kunafanya bibi na bwana wasitumainiane na kunaweza kuvunja ndoa. Ikiwa wako na watoto, hilo linaweza kufanya watoto wavurugike, wajisikie kuwa hawapendwe, hawako salama, ao hata kuwafanya wakuwe na kinyongo.

“KILE AMBACHO MUNGU AMEUNGANISHA.” Ndoa pia, ni muungano takatifu. Bibi na bwana wenye wanaheshimia ukweli huo wanajikaza sana ili kutia nguvu ndoa yao. Wakati matatizo yanatokea, hawatafute sababu yenye haina musingi ili kuvunja ndoa yao. Upendo wao ni wenye nguvu na wenye kuendelea hata wakati wa magumu. Upendo kama huo ‘unavumilia mambo yote,’ na unasaidia kumaliza matatizo ili kuendelea kuwa na umoja na amani katika ndoa.

Wakati wazazi wanaonyeshana upendo wa kujitoa, upendo huo unakuwa wenye faida kubwa kwa kila mutoto katika familia. Kijana mumoja mwanamuke mwenye kuitwa Jessica alisema: “Baba na mama wanapendana na kuheshimiana sana. Wakati ninaona mama anamuheshimia baba yangu, hilo linanichochea nimuige.”

Upendo ndiyo sifa kubwa zaidi ya Mungu. Kwa kweli, Biblia inasema hivi: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Kwa hiyo, haishangaze kuona Yehova anaitwa pia “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Sisi pia tutakuwa wenye furaha wakati tunajikaza kuiga sifa za Muumbaji wetu​—zaidi sana upendo. Andiko la Waefeso 5:1, 2 linasema hivi: ‘Mukuwe waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na muendelee kutembea katika upendo.’