Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA: JE, KWELI MUNGU HANA HURUMA?

Sababu Gani Watu Wanasema Kwamba Mungu Hana Huruma?

Sababu Gani Watu Wanasema Kwamba Mungu Hana Huruma?

JE, UNAONA ulizo lililo kwenye jalada la gazeti hili kuwa lenye kushangaza? Watu fulani wanaona ulizo hilo kuwa lenye kushangaza, hata hivyo watu wengi leo wanajiuliza ikiwa Mungu hana huruma ao wanaamini hivyo. Sababu gani?

Watu fulani ambao wanaokoka misiba ya asili wanauliza hivi: “Sababu gani Mungu anaacha mambo hayo yatokee? Je, anatuhangaikia? Ao je, yeye ana huruma?”

Wengine wanavurugika hivyohivyo wanaposoma Biblia. Wanapata masimulizi kama vile simulizi juu ya Noa na Garika, na wanajiuliza, ‘Sababu gani Mungu mwenye upendo aliwaua watu hao wote? Je, yeye ana huruma?’

Je, nyakati fulani unajiuliza maulizo kama hayo? Ao ni vigumu kwako kuwajibu watu ambao wanauliza ikiwa Mungu hana huruma? Juu ya maulizo hayo mawili, chunguza ulizo lingine tofauti ambalo linaweza kukusaidia.

SABABU GANI TUNACHUKIA MATENDO YA KUKOSA HURUMA?

Kwa kifupi, tunachukia matendo ya kukosa huruma kwa sababu tuna uwezo wa kutambua mema na mabaya. Katika hali hiyo tunatofautiana sana na wanyama. Muumbaji wetu alituumba ‘kwa mufano wake.’ (Mwanzo 1:27) Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba alitupatia uwezo wa kuonyesha sifa zake, kanuni zake za mwenendo, na uwezo wake wa kutambua mema na mabaya. Fikiria hili: Ikiwa Mungu alitupatia uwezo wa kutambua mema na mabaya na tuna mwelekeo wa kuchukia matendo ya kukosa huruma, hilo linaonyesha kama Mungu pia anayachukia, sivyo?

Biblia inahakikisha kwamba Mungu anachukia matendo ya kukosa huruma, kwa sababu katika Biblia, Mungu anahakikisha hivi: ‘Njia zangu ziko juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.’ (Isaya 55:9) Ikiwa tunasema kama Mungu hana huruma, hilo litaonekana kuwa kinyume cha mambo ambayo Biblia inafundisha—ni sawa vile tunasema kama njia zetu ziko juu kuliko njia zake. Ni jambo la hekima kabisa kuchunguza mambo mengi mbele ya kuwa na maoni hayo. Labda hatuhitaji kuuliza ikiwa Mungu hana huruma, lakini tunahitaji kuuliza sababu gani matendo yake fulani yanaweza kuonekana kuwa bila huruma. Ili kutusaidia, acheni tuchunguze ikiwa “kukosa huruma” kunamaanisha nini kabisa.

Tunaposema kama mutu fulani hana huruma, tunashakia nia yake. Mutu asiye na huruma ni yule anayefurahia kuona wengine wanateseka ao asiyehangaikia mateso yao. Kwa hiyo, baba anayemuazibu mutoto wake kwa sababu anafurahia kumuumiza moyoni ni baba asiye na huruma. Lakini baba anayemuazibu mutoto wake ili kumufundisha ao kumulinda ni baba muzuri. Ni vyepesi kuelewa vibaya nia iliyomufanya mutu atende kwa njia fulani, unajua hilo vizuri ikiwa mutu fulani amekwisha kukuelewa vibaya.

Acheni tuchunguze sababu mbili kati ya sababu zinazowafanya watu fulani wafikiri kwamba Mungu hana huruma: misiba ya asili tunayoona leo na hukumu za Mungu ambazo tunasoma katika Biblia. Je, mambo yanayotokea yanaonyesha kabisa kwamba Mungu hana huruma?