Danieli 12:1-13

  • “Wakati wa mwisho” na baadaye (1-13)

    • Mikaeli atenda (1)

    • Wenye ufahamu watang’aa (3)

    • Kuenea kwa ujuzi wa kweli (4)

    • Danieli ataamka na kupokea fungu lake (13)

12  “Wakati huo Mikaeli*+ atasimama,* yule mkuu+ anayesimama kwa ajili ya watu wako.* Na kutakuwa na wakati wa taabu ambao haujawahi kamwe kutokea tangu kuanzishwa kwa taifa lolote mpaka wakati huo. Na wakati huo watu wako wataponyoka,+ kila mtu atakayepatikana ameandikwa katika kile kitabu.+  Na wengi kati ya wale wanaolala usingizi katika mavumbi ya dunia wataamka, baadhi yao watapata uzima wa milele na wengine watapata shutuma na chuki ya milele.  “Na wale walio na ufahamu watang’aa sana kama anga la mbingu, na wale wanaowaleta wengi kwenye uadilifu watang’aa kama nyota, milele na milele.  “Lakini wewe, Danieli, yaweke siri maneno haya, na ukifunge kwa muhuri kitabu hiki mpaka wakati wa mwisho.+ Wengi watazunguka huku na huku,* na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.”+  Kisha mimi, Danieli, nikatazama na kuwaona wengine wawili wamesimama mahali hapo, mmoja kwenye ukingo huu wa kijito na yule mwingine kwenye ukingo wa pili wa kijito.+  Kisha mmoja akamuuliza yule mwanamume aliyevaa mavazi ya kitani,+ aliyekuwa juu ya maji ya kijito: “Itachukua muda gani kufikia mwisho wa mambo haya ya kustaajabisha?”  Kisha nikamsikia yule mwanamume aliyevaa mavazi ya kitani, aliyekuwa juu ya maji ya kijito, alipokuwa akiinua mkono wake wa kulia na mkono wake wa kushoto kuelekea mbinguni na kuapa hivi kwa jina la Yule anayeishi milele:+ “Itakuwa ni kwa wakati uliowekwa, nyakati zilizowekwa, na nusu ya wakati.* Mara tu kuvunjwavunjwa kwa nguvu za watu watakatifu kutakapofikia mwisho,+ mambo haya yote yatafikia mwisho wake.”  Basi mimi, nilisikia, lakini sikuweza kuelewa;+ kwa hiyo nikauliza: “Ee bwana wangu, matokeo ya mambo haya yote yatakuwa nini?”  Akajibu: “Nenda, Danieli, kwa sababu maneno haya yanapaswa kuwekwa yakiwa siri na kutiwa muhuri mpaka wakati wa mwisho.+ 10  Wengi watajitakasa na kujifanya weupe nao watasafishwa.+ Na waovu watatenda uovu, na hakuna mwovu yeyote atakayeelewa; lakini wale walio na ufahamu wataelewa.+ 11  “Na tangu wakati wa kuondolewa kwa ile dhabihu inayotolewa daima*+ na kusimamishwa kwa kile kitu kinachochukiza sana kinachosababisha ukiwa,+ kutakuwa na siku 1,290. 12  “Mwenye furaha ni yule anayeendelea kutarajia* na anayefika kwenye zile siku 1,335! 13  “Lakini wewe, endelea mpaka mwisho. Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako* mwishoni mwa zile siku.”+

Maelezo ya Chini

Maana yake “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”
Au “atainuka.”
Tnn., “wana wa watu wako.”
Au “watakichunguza [yaani, kitabu hiki] kwa makini.”
Yaani, nyakati tatu na nusu.
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku.”
Au “anayengojea kwa hamu kubwa.”
Au “mahali pako ulipogawiwa.”