Hamia kwenye habari

Je, Kuna Mungu?

Je, Kuna Mungu?

Jibu la Biblia

 Ndiyo, Biblia inatoa uthibitisho usioweza kutiliwa shaka kwamba kuna Mungu. Inatutia moyo tuwe na imani katika Mungu, si kuamini maoni ya kidini bila sababu, bali kwa kutumia ‘nguvu zetu za kufikiri’ na “uwezo wa akili.” (Waroma 12:1; 1 Yohana 5:​20) Fikiria hoja zifuatazo zinazotegemea Biblia:

  •   Kuwapo kwa ulimwengu ulioumbwa kwa utaratibu wa hali ya juu kunaonyesha kwamba kuna Muumba. Biblia inasema: “Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Ingawa wazo hilo ni rahisi kulielewa, wasomi wengi huliona kuwa ni hoja yenye nguvu sana isiyoweza kukanushwa. a

  •   Tukiwa wanadamu, tuna tamaa ya kiasili ya kutaka kuelewa maana na kusudi la uhai, tamaa ambayo bado huendelea kuwapo hata ikiwa mahitaji yetu ya kimwili yanatoshelezwa. Biblia inafafanua tamaa hiyo kuwa ‘uhitaji wetu wa kiroho,’ uhitaji unaotia ndani tamaa ya kumjua na kumwabudu Mungu. (Mathayo 5:3; Ufunuo 4:​11) Mbali na kuthibitisha kwamba kuna Mungu, uhitaji huo wa kiroho unaonyesha pia kwamba Mungu ni Muumba anayetupenda anayetaka tutosheleze uhitaji huo.​—Mathayo 4:4.

  •   Unabii mbalimbali wa Biblia wenye mambo mengi uliandikwa karne nyingi kabla ya wakati na ulitimia kikamili na kwa wakati barabara kama tu ilivyotabiriwa. Usahihi na vilevile habari nyingi zenye kina kuhusu unabii huo zinatoa uthibitisho wenye nguvu kwamba haukutokana na chanzo cha kibinadamu.​—2 Petro 1:​21.

  •   Waandikaji wa Biblia walikuwa na ujuzi wa kisayansi uliozidi ule wa watu walioishi wakati wao. Kwa mfano, zamani watu wengi waliamini kwamba dunia ilishikiliwa na mnyama, kama vile tembo, nguruwe-mwitu, au ng’ombe-dume. Tofauti na hilo, Biblia inasema kwamba Mungu ‘anaitundika dunia pasipo na kitu.’ (Ayubu 26:7) Vivyo hivyo, Biblia inafafanua umbo la dunia kwa usahihi kuwa “mviringo,” au “duara.” (Isaya 40:22; Union Version) Watu wengi wanahisi kwamba waandikaji wa Biblia walipata habari hizo kutoka kwa Mungu. Kwa maoni yao, hiyo ndiyo njia inayopatana na akili zaidi ya kuelezea walitoa wapi uelewaji huo.

  •   Biblia inajibu maswali mengi magumu, maswali ambayo yasipojibiwa vizuri yanaweza kumfanya mtu aache kuamini kwamba kuna Mungu. Kwa mfano: Ikiwa Mungu anatupenda na ni Mweza-Yote, kwa nini watu wanateseka na kwa nini kuna uovu ulimwenguni? Kwa nini mara nyingi dini husababisha mambo mabaya badala ya mazuri?​—Tito 1:​16.

a Kwa mfano, wakati mmoja mtaalamu wa nyota Allan Sandage alisema hivi kuhusu ulimwengu: “Naona ni jambo lisilowezekana kwamba utaratibu [katika ulimwengu] ulitokana tu na machafuko. Lazima utaratibu huo uwe na chanzo fulani. Mimi humwona Mungu kuwa fumbo, lakini yeye ndiye anayeweza kueleza muujiza wa kuwapo kwa vitu, kueleza vilikotoka.”