Hamia kwenye habari

Wokovu Ni Nini?

Wokovu Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Nyakati nyingine, maneno “okoa” na “wokovu” hutumiwa na waandikaji wa Biblia kuwasilisha wazo la mtu anayeokolewa kutokana na hatari au uharibifu. (Kutoka 14:13, 14; Matendo 27:20) Hata hivyo, mara nyingi maneno hayo humaanisha kuokolewa kutokana na dhambi. (Mathayo 1:21) Kwa kuwa dhambi husababisha kifo, watu wanaookolewa kutokana na dhambi wanatumaini la kuishi milele.​—Yohana 3:16, 17. a

Mtu anapaswa kufanya nini ili aokolewe?

 Ili uokolewe, unapaswa kuwa na imani katika Yesu na kuonyesha imani hiyo kwa kutii amri zake.​—Matendo 4:10, 12; Waroma 10:9, 10; Waebrania 5:9.

 Biblia inaonyesha kwamba unapaswa kuonyesha utii kwa matendo ili uthibitishe kwamba imani yako iko hai. (Yakobo 2:24, 26) Hata hivyo hilo halimaanishi kwamba unaweza kujipatia wokovu kwa matendo yako. Wokovu ni “zawadi ya Mungu” inayotegemea “fadhili zisizostahiliwa” za Mungu.​ —Waefeso 2:8, 9.

Je, unaweza kupoteza wokovu?

 Ndiyo. Kama tu mtu aliyekuwa akizama anavyoweza kuokolewa kisha aanguke au aruke tena ndani ya maji, ndivyo mtu aliyeokolewa kutokana na dhambi lakini anakosa kudumisha imani anavyoweza kupoteza wokovu. Kwa sababu hiyo, Biblia inawasihi Wakristo ambao wameokolewa ‘wafanye pigano kali kwa ajili ya imani.’ (Yuda 3) Pia, inawaonya hivi wale ambao wameokolewa: “Endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.”​—Wafilipi 2:12.

Mwokozi ni nani​—ni Mungu au Yesu?

 Biblia inamtambulisha Mungu kuwa ndiye chanzo cha wokovu, mara nyingi ikimwita “Mwokozi.” (1 Samweli 10:19; Isaya 43:11; Tito 2:10; Yuda 25) Isitoshe, Mungu aliwatumia wanaume mbalimbali kuliokoa taifa la kale la Israeli, na Biblia inatumia neno “waokozi” inapozungumza kuwahusu. (Nehemia 9:27; Waamuzi 3:9, 15; 2 Wafalme 13:5) b Vivyo hivyo, kwa kuwa Mungu huandaa wokovu kutokana na dhambi kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, Biblia inamtaja Yesu kuwa “Mwokozi.”​—Matendo 5:31; Tito 1:4. c

Je, kila mtu ataokolewa?

 Hapana, baadhi ya watu hawataokolewa. (2 Wathesalonike 1:9) Yesu alipoulizwa, “Je, wale wanaookolewa ni wachache?” alijibu akasema: “Jitahidini sana ili mwingie kupitia mlango mwembamba, kwa sababu wengi, ninawaambia ninyi, watajaribu kuingia lakini hawataweza.”​—Luka 13:23, 24.

Maoni yasiyo sahihi kwamba watu wote wataokolewa

 Uwongo: Barua ya 1 kwa Wakorintho 15:22 inafundisha kwamba watu wote wataokolewa inaposema kwamba “katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.”

 Kweli: Muktadha wa mstari huo unazungumzia ufufuo. (1 Wakorintho 15:12, 13, 20, 21, 35) Kwa hiyo, maneno “katika Kristo wote watafanywa kuwa hai” yanamaanisha kwamba watu wote wanaofufuliwa wanapata baraka hiyo kupitia Yesu Kristo.​—Yohana 11:25.

 Uwongo: Tito 2:11 inafundisha kuwa watu wote wataokolewa kwa kusema kwamba Mungu ‘anawaletea watu wa namna zote wokovu.’

 Kweli: Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “zote” katika mstari huo linaweza pia kumaanisha “aina zote.” d Hivyo, uelewaji unaofaa wa Tito 2:11 ni kwamba Mungu anawaandalia wokovu watu wa namna zote, kutia ndani “mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.”​—Ufunuo 7:9, 10.

 Uwongo: Barua ya 2 ya Petro 3:9 inafundisha kwamba watu wote wataokolewa kwa kusema kwamba Mungu “hataki yeyote aangamizwe.”

 Kweli: Mungu anataka watu waokolewe, lakini hawalazimishi wakubali uandalizi wake wa wokovu. ‘Siku yake ya hukumu’ itakuwa pia siku ya “kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.”​—2 Petro 3:7.

a Biblia inaweza kusema kwamba watu tayari ‘wameokolewa’ ingawa bado hawajaokolewa kutokana na dhambi na kifo.​—Waefeso 2:5; Waroma 13:11.

b Katika mistari iliyotajwa, tafsiri fulani zinatumia maneno “mtu wa kuwakomboa,” au “kiongozi.” Hata hivyo, katika maandishi ya awali ya Biblia ya Kiebrania, neno linalotumiwa kuwahusu waokozi linatumiwa pia mahali pengine kumrejelea Yehova Mungu kuwa Mwokozi.​—Zaburi 7:10.

c Jina Yesu linatokana na neno la Kiebrania Yehoh·shuʹaʽ, linalomaanisha “Yehova Ni Wokovu.”

d Ona Vine’s Complete Expository Dictionary of Old and New Testament Words. Neno lilelile la Kigiriki linapatikana kwenye Mathayo 5:11, andiko linaloonyesha maneno ya Yesu kwamba watu wangesema “kila namna ya” jambo baya dhidi ya wafuasi wake.