Kulingana na Mathayo 19:1-30

  • Ndoa na talaka (1-9)

  • Zawadi ya useja (10-12)

  • Yesu awabariki watoto (13-15)

  • Swali la mwanamume kijana tajiri (16-24)

  • Kujidhabihu kwa ajili ya Ufalme (25-30)

19  Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, akaondoka Galilaya na kwenda kwenye mipaka ya* Yudea ng’ambo ya Yordani.+  Pia, umati mkubwa ukamfuata, naye akawaponya huko.  Mafarisayo wakaja wakikusudia kumjaribu Yesu, wakamuuliza: “Je, ni halali mwanamume kumtaliki mke wake kwa sababu yoyote ile?”+  Akawajibu: “Je, hamkusoma kwamba yule aliyewaumba tangu mwanzo aliwaumba mwanamume na mwanamke+  na kusema: ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’?+  Basi wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”+  Wakamuuliza: “Basi, kwa nini Musa aliagiza kutoa cheti cha kumfukuza na kumtaliki?”+  Akawajibu: “Musa aliwaruhusu kuwataliki wake zenu kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu,+ lakini haikuwa hivyo tangu mwanzo.+  Ninawaambia kwamba mtu yeyote anayemtaliki mke wake isipokuwa kwa sababu ya uasherati,* na kumwoa mwingine, anafanya uzinzi.”+ 10  Wanafunzi wakamwambia: “Ikiwa hali iko hivyo kati ya mtu na mke wake, ni afadhali mtu asioe.” 11  Yesu akawaambia: “Si watu wote wanaolipa nafasi jambo hilo, ila tu wale walio na zawadi.+ 12  Kwa maana kuna wale waliozaliwa wakiwa matowashi, wengine wamefanywa matowashi na watu, na wengine wamejifanya wenyewe kuwa matowashi kwa ajili ya Ufalme wa mbinguni. Yule anayeweza kulipa nafasi jambo hilo na afanye hivyo.”+ 13  Ndipo watu wakamletea watoto wadogo ili aweke mikono yake juu yao na kusali, lakini wanafunzi wakawakemea.+ 14  Hata hivyo, Yesu akawaambia: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, na msijaribu kuwazuia, kwa maana Ufalme wa mbinguni ni wa wale walio kama wao.”+ 15  Naye akaweka mikono yake juu yao kisha akaondoka hapo. 16  Sasa tazama! mtu fulani akamjia na kumuuliza: “Mwalimu, ninapaswa kufanya mambo gani mema ili nipate uzima wa milele?”+ 17  Yesu akamwambia: “Kwa nini unaniuliza kuhusu mambo mema? Kuna Mmoja tu aliye mwema.+ Hata hivyo, ikiwa unataka kuingia katika uzima, zishike amri sikuzote.”+ 18  Akamuuliza: “Amri gani?” Yesu akajibu: “Usiue,+ usifanye uzinzi,+ usiibe,+ usitoe ushahidi wa uwongo,+ 19  mheshimu baba yako na mama yako,+ na lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.”+ 20  Yule mwanamume kijana akamwambia: “Nimeyashika yote hayo; nifanye nini zaidi?” 21  Yesu akamwambia: “Ikiwa unataka kuwa mkamilifu,* nenda ukauze mali zako na uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni;+ kisha uje uwe mfuasi wangu.”+ 22  Yule mwanamume kijana aliposikia hivyo, akaenda zake akiwa na huzuni, kwa maana alikuwa na mali nyingi.+ 23  Ndipo Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Kwa kweli ninawaambia, itakuwa vigumu kwa tajiri kuingia katika Ufalme wa mbinguni.+ 24  Tena ninawaambia, ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.”+ 25  Wanafunzi waliposikia hilo, wakashangaa sana na kumuuliza: “Ni nani kwa kweli anayeweza kuokolewa?”+ 26  Yesu akawatazama kwa makini na kusema: “Kwa wanadamu jambo hilo haliwezekani, lakini kwa Mungu mambo yote yanawezekana.”+ 27  Ndipo Petro akamwambia: “Tazama! Tumeacha kila kitu na kukufuata; basi tutapata nini?”+ 28  Yesu akasema: “Kwa kweli ninawaambia, katika uumbaji mpya, Mwana wa binadamu atakapoketi katika kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi ambao mmenifuata mtaketi katika viti vya ufalme 12, mkiyahukumu makabila 12 ya Israeli.+ 29  Na kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara 100 zaidi, naye ataurithi uzima wa milele.+ 30  “Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho na wa mwisho watakuwa wa kwanza.+

Maelezo ya Chini

Au “karibu na mipaka ya.”
Neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.
Au “kamili.”