Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 1

Fuata Mwongozo wa Mungu ili Uwe na Ndoa Yenye Furaha

Fuata Mwongozo wa Mungu ili Uwe na Ndoa Yenye Furaha

“Yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke.”​—Mathayo 19:4

Yehova * Mungu ndiye aliyeanzisha ndoa ya kwanza. Biblia inasema kwamba alimuumba mwanamke wa kwanza kisha ‘akamleta kwa mwanamume.’ Adamu alifurahi sana hivi kwamba akasema: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu.” (Mwanzo 2:22, 23) Bado Yehova anataka watu waliofunga ndoa wawe na furaha.

Unapofunga ndoa, huenda ukafikiri mambo yote yatakuwa shwari. Hata hivyo, ukweli ni kwamba hata mume na mke wanaopendana sana watakuwa na matatizo. (1 Wakorintho 7:28) Katika Broshua hii utapata kanuni za Biblia ambazo ukizifuata, zitakusaidia kuwa na ndoa na familia yenye furaha.​—Zaburi 19:8-11.

1 KUBALI JUKUMU ULILOPEWA NA YEHOVA

BIBLIA INASEMA HIVI: Mume ndiye kichwa cha familia.​—Waefeso 5:23.

Kama wewe ni mume, Yehova anataka umtunze mke wako kwa upendo. (1 Petro 3:7) Alimuumba akiwa kikamilisho chako, na anataka umthamini na kumpenda. (Mwanzo 2:18) Ni lazima umpende sana mke wako na uwe tayari kutanguliza mapendezi yake kabla ya mapendezi yako.​—Waefeso 5:25-29.

Kama wewe ni mke, Yehova anataka umheshimu sana mume wako na kumsaidia kutimiza jukumu lake. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:​33) Unga mkono kabisa maamuzi yake na ushirikiane naye. (Wakolosai 3:18) Ukifanya hivyo, utamfurahisha mume wako na kumpendeza Yehova.​—1 Petro 3:1-6.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Muulize mwenzi wako jinsi unavyoweza kuwa mume au mke mwema. Sikiliza kwa makini na ujitahidi kabisa kufanya marekebisho

  • Uwe mwenye subira. Itachukua muda kwa kila mmoja kujifunza jinsi ya kumfurahisha mwenzake

2 PENDEZWA KIKWELI NA HISIA ZA MWENZI WAKO

BIBLIA INASEMA HIVI: Unapaswa kutanguliza faida za mwenzi wako. (Wafilipi 2:3, 4) Onyesha kwamba unamthamini mwenzi wako, na ukumbuke Yehova anataka watumishi wake wawe ‘wapole kwa wote.’ (2 Timotheo 2:24) Maneno yanayosemwa bila kufikiri ni kama “upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” Kwa hiyo, chagua maneno yako kwa busara. (Methali 12:18) Roho ya Yehova itakusaidia kuzungumza kwa fadhili na upendo.​—Wagalatia 5:22, 23; Wakolosai 4:6.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Mwombe Yehova akupe utulivu na usawaziko kabla ya kuzungumzia jambo lolote zito pamoja na mwenzi wako

  • Fikiria kwa makini mambo utakayosema na jinsi utakavyoyasema

3 FANYENI MAAMUZI PAMOJA

BIBLIA INASEMA HIVI: Unapofunga ndoa, wewe na mwenzi wako mnakuwa “mwili mmoja.” (Mathayo 19:5) Lakini bado nyinyi ni watu wawili na huenda kila mmoja ana mapendezi yake. Kwa hiyo, mnapaswa kujifunza kuunganisha mawazo na hisia zenu. (Wafilipi 2:2) Umoja ni muhimu mnapofanya maamuzi. Biblia inasema: “Kwa shauri mipango yenyewe hufanywa imara.” (Methali 20:18) Fuateni kanuni za Biblia mnapofanya maamuzi muhimu pamoja.​—Methali 8:32, 33.

UNACHOWEZA KUFANYA:

  • Mbali na kumwambia mwenzi wako habari na maoni yako, mweleze pia hisia zako

  • Zungumza na mwenzi wako kabla ya kufanya makubaliano na mtu mwingine

^ fu. 4 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.