Kulingana na Mathayo 13:1-58

  • MIFANO KUHUSU UFALME (1-52)

    • Mpandaji (1-9)

    • Kwa nini Yesu alitumia mifano? (10-17)

    • Mfano wa mpandaji wafafanuliwa (18-23)

    • Ngano na magugu (24-30)

    • Mbegu ya haradali na chachu (31-33)

    • Yesu atumia mifano, atimiza unabii (34, 35)

    • Mfano wa ngano na magugu wafafanuliwa (36-43)

    • Hazina iliyofichwa na lulu nzuri (44-46)

    • Wavu wa kukokota (47-50)

    • Hazina mpya na za zamani (51, 52)

  • Yesu akataliwa katika eneo la nyumbani kwao (53-58)

13  Siku hiyo Yesu akatoka ndani ya nyumba na kuketi kando ya bahari.  Na umati mkubwa sana ukakusanyika karibu naye hivi kwamba akapanda ndani ya mashua na kuketi, na umati wote ulikuwa umesimama ufuoni.+  Ndipo akawaambia mambo mengi kwa kutumia mifano,+ akisema: “Tazama! Mpandaji alienda kupanda mbegu.+  Alipokuwa akipanda, mbegu fulani zikaanguka kando ya barabara, ndege wakaja na kuzila.+  Nyingine zikaanguka kwenye miamba, mahali pasipo na udongo mwingi, na mara moja zikachipuka kwa sababu udongo haukuwa na kina.+  Lakini jua lilipochomoza, ziliungua na kunyauka kwa sababu hazikuwa na mizizi.  Nyingine zikaanguka kwenye miiba, nayo miiba ikakua na kuzisonga.+  Mbegu nyingine zikaanguka kwenye udongo mzuri nazo zikaanza kuzaa matunda, nyingine mara 100 zaidi, nyingine 60, na nyingine 30.+  Aliye na masikio na asikilize.”+ 10  Basi wanafunzi wakaja na kumuuliza: “Kwa nini unazungumza nao kwa kutumia mifano?”+ 11  Akawajibu: “Ninyi mmepewa uwezo wa kuzielewa siri takatifu+ za Ufalme wa mbinguni, lakini wao hawajapewa. 12  Kwa maana yeyote aliye na kitu ataongezewa, naye atazidishiwa; lakini yeyote asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.+ 13  Ndiyo maana ninazungumza nao kwa kutumia mifano, kwa sababu, wanatazama lakini hawaoni, wanasikiliza lakini hawasikii, wala hawaelewi.+ 14  Na unabii wa Isaya unatimia kwao unaosema: ‘Kwa kweli mtasikia lakini hamtaelewa, nanyi kwa kweli mtatazama lakini hamtaona.+ 15  Kwa maana mioyo ya watu hawa imekuwa migumu, nao wamesikia kwa masikio yao bila kuitikia, nao wamefunga macho yao, ili wasione kamwe kwa macho yao na kusikia kwa masikio yao na kuelewa kwa mioyo yao, kisha wageuke nami niwaponye.’+ 16  “Hata hivyo, macho yenu ni yenye furaha kwa sababu yanaona na masikio yenu kwa sababu yanasikia.+ 17  Kwa kweli ninawaambia, manabii wengi na watu waadilifu walitamani kuona mambo mnayoona lakini hawakuyaona,+ na kusikia mambo mnayosikia lakini hawakuyasikia. 18  “Basi, sikilizeni maana ya mfano wa yule mtu aliyepanda mbegu.+ 19  Mtu yeyote anaposikia neno la Ufalme lakini halielewi, yule mwovu+ huja na kunyakua kilichopandwa moyoni mwake; hiyo ndiyo mbegu iliyopandwa kando ya barabara.+ 20  Na mbegu iliyopandwa kwenye miamba, ni yule anayelisikia neno na kulipokea mara moja kwa shangwe.+ 21  Lakini hana mizizi ndani yake bali anaendelea kwa wakati fulani, hata hivyo dhiki au mateso yakitokea kwa sababu ya lile neno mara moja anakwazika. 22  Na mbegu iliyopandwa kwenye miiba, ni yule anayelisikia neno, lakini mahangaiko ya mfumo huu wa mambo*+ na nguvu za udanganyifu za utajiri hulisonga neno, nalo halizai matunda.+ 23  Na mbegu iliyopandwa kwenye udongo mzuri ni wale wanaosikia neno na kulielewa, ambao kwa kweli huzaa matunda, mmoja huzaa mara 100 zaidi, mwingine 60, na mwingine 30.”+ 24  Akawatolea mfano mwingine, akisema: “Ufalme wa mbinguni ni kama mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake. 25  Watu walipokuwa wamelala usingizi, adui yake akaja na kupanda magugu kati ya ngano kisha akaondoka. 26  Ngano ilipoota na kuzaa matunda, magugu pia yalionekana. 27  Kwa hiyo watumwa wa bwana wa nyumba wakaja na kumwambia, ‘Bwana, je, hukupanda mbegu nzuri katika shamba lako? Basi magugu yametoka wapi?’ 28  Akawaambia, ‘Adui, mtu fulani, ndiye aliyefanya hivyo.’+ Watumwa wakamuuliza, ‘Basi, je, unataka twende tukayang’oe?’ 29  Akasema, ‘Hapana, ili mnapong’oa magugu, msije mkang’oa ngano pia. 30  Acheni vikue pamoja mpaka wakati wa mavuno, na katika majira ya mavuno nitawaambia wavunaji: Kusanyeni magugu kwanza na kuyafunga matita-matita ili yateketezwe motoni; kisha mkusanye ngano ghalani mwangu.’”+ 31  Akawatolea mfano mwingine akisema: “Ufalme wa mbinguni ni kama mbegu ya haradali ambayo mtu aliichukua na kuipanda katika shamba lake.+ 32  Kwa kweli, mbegu hiyo ni ndogo kuliko mbegu zote, lakini inapokua huwa kubwa kuliko mimea yote ya mboga na huwa mti, hivi kwamba ndege wa angani huja na kupata makao katika matawi yake.” 33  Akawaambia mfano mwingine: “Ufalme wa mbinguni ni kama chachu* ambayo mwanamke aliichukua na kuchanganya na vipimo vikubwa vitatu vya unga, mpaka unga wote ukachacha.”*+ 34  Yesu alizungumza mambo hayo yote na umati kwa kutumia mifano. Kwa kweli, hakuwa akizungumza nao bila mfano,+ 35  ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii: “Nitafungua kinywa changu kwa mifano; nitatangaza mambo yaliyofichwa tangu kuwekwa msingi.”*+ 36  Baada ya kuuaga umati, akaingia ndani ya nyumba. Wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Tufafanulie ule mfano wa magugu katika shamba.” 37  Akawajibu: “Mpandaji aliyepanda mbegu nzuri ni Mwana wa binadamu; 38  lile shamba ni ulimwengu.+ Nazo mbegu nzuri ni wana wa Ufalme, lakini magugu ni wana wa yule mwovu,+ 39  na adui aliyepanda magugu ni Ibilisi. Mavuno ni umalizio wa mfumo wa mambo,* na wavunaji ni malaika. 40  Kwa hiyo, kama vile magugu hukusanywa na kuteketezwa kwa moto, ndivyo itakavyokuwa katika umalizio wa mfumo wa mambo.*+ 41  Mwana wa binadamu atawatuma malaika zake, nao watakusanya kutoka katika Ufalme wake vitu vyote vinavyosababisha kukwazika na watu wenye mazoea ya kuasi sheria, 42  nao watawatupa ndani ya tanuru la moto.+ Humo ndimo watalia na kusaga meno yao. 43  Wakati huo waadilifu watang’aa kwa uangavu kama jua+ katika Ufalme wa Baba yao. Aliye na masikio na asikilize. 44  “Ufalme wa mbinguni ni kama hazina iliyofichwa katika shamba, ambayo mtu fulani aliipata na kuificha; na kwa sababu ya shangwe aliyo nayo, anaenda na kuuza kila kitu alicho nacho na kununua shamba hilo.+ 45  “Tena Ufalme wa mbinguni ni kama mfanyabiashara anayesafiri akitafuta lulu nzuri. 46  Alipopata lulu moja yenye thamani kubwa, alienda na mara moja akauza vitu vyote alivyokuwa navyo na kuinunua.+ 47  “Tena Ufalme wa mbinguni ni kama wavu wa kukokotwa ulioshushwa baharini, ukavua samaki wa kila aina. 48  Ulipojaa waliuvuta hadi ufuoni, nao wakaketi na kuwaweka samaki wazuri+ ndani ya vyombo, lakini wakawatupa wale wasiofaa.+ 49  Hivyo ndivyo itakavyokuwa katika umalizio wa mfumo wa mambo.* Malaika wataenda kuwatenganisha waovu kutoka kwa waadilifu. 50  Nao watawatupa waovu ndani ya tanuru la moto. Humo ndimo watalia na kusaga meno yao. 51  “Je, mmeelewa mambo hayo yote?” Wakamjibu: “Ndiyo.” 52  Ndipo akawaambia: “Ikiwa ni hivyo, kila mwalimu wa watu wote, anapofundishwa kuhusu Ufalme wa mbinguni ni kama bwana wa nyumba, ambaye hutoa katika hazina yake vitu vipya na pia vya zamani.” 53  Yesu alipomaliza kutoa mifano hiyo akaondoka hapo. 54  Baada ya kuingia katika eneo lake la nyumbani,+ akaanza kuwafundisha katika sinagogi lao, hivi kwamba wakashangaa na kuuliza: “Mtu huyu alipata wapi hekima hii na matendo haya yenye nguvu?+ 55  Je, huyu si mwana wa yule seremala?+ Je, mama yake haitwi Maria, na ndugu zake Yakobo, Yosefu, Simoni, na Yuda?+ 56  Na dada zake, je, wote hawako pamoja nasi? Basi, alipata wapi mambo haya yote?”+ 57  Kwa hiyo, wakaanza kukwazika kwa sababu yake.+ Lakini Yesu akawaambia: “Nabii anaheshimiwa kila mahali isipokuwa katika eneo lake la nyumbani na katika nyumba yake mwenyewe.”+ 58  Naye hakufanya matendo mengi yenye nguvu huko kwa sababu hawakuwa na imani.

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “hamira.”
Au “ukaumuka.”
Au labda, “kuumbwa kwa ulimwengu.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.