Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kudhibiti Hisia Zangu Jinsi Gani?

Ninaweza Kudhibiti Hisia Zangu Jinsi Gani?

“Siku moja ninajihisi nikiwa na furaha, lakini siku inayofuata ninakuwa na majonzi. Mambo ambayo nilifikiri jana ni ya kawaida tu, yanakuwa mambo magumu kushughulika nayo leo.”​—Carissa.

Je, hisia zako zinapanda na kushuka kama barabarani yenye mashimo? a Ikiwa ndivyo, makala hii inaweza kukusaidia!

 Kwa nini hali hii inatokea?

 Kubadilika kwa hisia ni jambo la kawaida unapokabiliana na mabadiliko mbalimbali wakati wa kubalehe. Hata kama wewe ni tineja anayekaribia utu-uzima, huenda ukashangazwa na jinsi hisia zako zinavyoweza kubadilika bila kutarajia.

 Ikiwa unavurugika kwa sababu ya mabadiliko ya hisia, kumbuka kwamba hisia hizo zinatokana na mabadiliko ya homoni katika mwili wako pamoja na kukosa kujiamini na kuwa na mashaka. Mambo hayo ni sehemu ya kawaida ya ukuzi. Habari njema ni kwamba unaweza kuzielewa na kujifunza jinsi ya kukabiliana na hisia zako.

 Ukweli wa mambo: Kujifunza jinsi ya kudhibiti hisia zako ukiwa kijana ni jambo la maana kwa sababu utahitaji ujuzi huo katika hali mbalimbali ukiwa mtu mzima.

Mtazamo usiofaa ni kama mashimo ya barabarani. Unaweza kuepuka kwa ustadi mashimo makubwa na kufurahia safari yako

 Mambo matatu unayoweza kufanya

 Zungumza. Biblia inasema hivi: “Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote, naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”​—Methali 17:17.

 “Nina rafiki wa karibu sana ambaye ninamwona kuwa shangazi. Anasikiliza kwa makini mambo ninayomwambia, na ninahisi huru kumweleza hisia zangu. Ikiwa maoni yangu ni sahihi, ananipongeza, na ikiwa maoni yangu si sahihi ananirekebisha kwa njia bora sana.”​—Yolanda.

 Dokezo: Badala ya kuzungumza na watu wenye umri kama wako​—ambao huenda wanakabiliana na mabadiliko ya hisia kama yako​—zungumza na mzazi au mtu mzima ambaye unamwamini.

 Andika. Biblia inatueleza kuhusu Ayubu, ambaye akiwa amekata tamaa kabisa alisema hivi: “Nitamwaga malalamiko yangu. Nitasema waziwazi katika mateso yangu makali!” (Ayubu 10:1) Licha ya kuzungumza na mtu mwingine, njia nyingine unayoweza ‘kusema waziwazi’ ni kwa kuandika hisia zako.

 “Ninabeba daftari dogo mahali popote niendapo. Kitu chochote kikinikasirisha, ninaandika kukihusu. Kuandika ni dawa kwangu.”​—Iliana.

 Dokezo: Beba daftari ambalo unaweza kuandika mambo unayohisi, mambo yaliyochangia hisia hizo, na jinsi unavyoweza kushughulika nazo. Daftari lililoambatanishwa na makala hii linaweza kukusaidia kufanya hivyo.

 Sali. Biblia inasema hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye atakutegemeza. Hataruhusu kamwe mwadilifu aanguke.”​—Zaburi 55:22.

 “Ninasali kwa Yehova kila mara ninapopata mkazo. Kwa kawaida ninahisi faraja baada ya kumimina moyo wangu kwake.”​—Jasmine.

 Dokezo: Licha ya mahangaiko unayohisi, fikiria mambo matatu katika maisha yako ambayo unathamini. Unaposali kwa Yehova, mwombe msaada​—lakini pia mshukuru kwa baraka ulizopata.

a Makala hii inazungumzia mabadiliko ya hisia ambayo kwa kawaida yanawapata vijana. Ikiwa unakabiliana na ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia au aina nyingine ya kushuka moyo, soma makala yenye kichwa“Ninaweza Kukabilianaje na Kushuka Moyo?”